Saturday, February 16, 2019

KUTAMBULISHWA, KUJITAMBUA, KUJITAMBULISHA :: [VII] TUJITAMBULISHE::::::II

Mwendelezo wa Sura ya VII kutoka wiki iliyopita...
Jitambulishe Mbele ya Mauti
Mauti ndio silaha kubwa au nguvu kubwa ya Shetani. Kumshinda Shetani na kushinda mauti ni kitu kimoja. Mauti ni uhai wa Shetani. Mtu yeyote mwenye dhambi akifa na kwenda kuzimu hawezi kutoka kwa kuwa mauti itamfunga kuzimu. Yesu hakutenda dhambi aliposhuka kuzimu. Mauti haikuweza kumshika na kumzuia kutoka kuzimu, “24ambaye Mungu alimfufua, akiufungua uchungu wa mauti, kwasababu haikuwezekana ashikwe nao.” (Matendo 2:24).
Alifufuka toka kuzimu akiwa na ‘funguo’, “17Nami nilipomwona, nalianguka miguuni pake kama mtu aliyekufa.  Akaweka mkono wake wa kuume juu yangu, akisema, Usiogope, Mimi ni wa kwanza na wa mwisho, 18na aliye hai, nami nalikuwa nimekufa na tazama, ni hai hata milele na milele.  Nami ninazo funguo za mauti na za kuzimu” (Ufunuo 1:17-18).  Yesu anavyoonekana hapa, ni uwezo wa kudhibiti maamuzi yote ya mauti au kuzimu duniani, hizi ni funguo. Adamu alipotenda dhambi aliifungulia mauti na kuzimu duniani.  Pepo wote na kazi zote za  Shetani wana mauti ndani yao. Kama vile mauti ilivyoshindwa kumzuia Yesu kutoka kuzimu, hata sasa nguvu ya mauti haiwezi kumzuia Yesu kufanya chochote duniani kupitia kanisa. Yesu duniani ni Kanisa!, 22akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwaajili ya kanisa; ambalo 23ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.” (Waefeso 1:22-23). Pepo yeyote hawezi kulizuia kanisa kufanya jambo, maana nguvu ya mauti itendayo kazi ndani ya pepo huyo haikumzuia Yesu kuzimu na Yesu huyo ni kichwa cha kanisa.  Yesu yupo ndani yetu, ni kichwa chetu, kichwa na mwili havitenganishwi, hivyo kanisa halitazuiwa na mauti au kuzimu duniani kwa njia ya Kristo ( Waefeso 1:23).
Jitambulishe katika ulimwengu wa roho mbele za mauti kwa njia ya Kristo aliye ndani yako.  Kwa kuwa mauti ipo ndani ya giza lote ikiwemo pepo wote, utapata njia ya upenyo kutiisha na kupita maeneo yasiyopitika.
Jitambulishe Mbele ya Magonjwa
Kama tulivyoona mwanzoni kujitambulisha ni swala la kufanya wakati wote.  Si wakati unaona tatizo tu.  Wakati wote jijengee mfumo wa kujitambulisha mbele za Shetani, mauti, nk ili kudhihirisha na kuthibitisha kuwa upo juu yake.  Dunia imejaa magonjwa jitambulishe yatakupisha na kukuogoga.  Unaweza tumia maandiko haya: “19Au hamjui ya kuwa mwili wenu ni hekalu la Roho Mtakatifu aliye ndani yenu, mliyepewa na Mungu? Wala ninyi si mali yenu wenyewe;  20maana mlinunuliwa kwa thamani.  Sasa basi, mtukuzeni Mungu katika miili yenu.” (1 Wakorintho 6:19-20). “17ili litimie lile neno lililonenwa na nabii Isaya, akisema, Mwenyewe aliutwaa udhaifu wetu, na kuyachukua magonjwa yetu.” (Mathayo 8:17).24Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa” (1Petro 2:24).
Wakati wote ongea mbele za magonjwa na kujitambulisha mwili wako ni nyumba ya Roho Mtakatifu na si nyumba ya magonjwa.  Jitambulishe udhaifu wako ulitwaliwa na Yesu, huo unaoonekana si wa kwako.  Jitambulishe katika Yesu huna ugonjwa yeye aliubeba.  Magonjwa mengi ni roho ya ugonjwa, ukijitambulisha utapata upenyo wa kupona na kuyatiisha.
Jitambulishe Mbele ya Umaskini
Umaskini sio sehemu ya maaisha yetu katika Yesu Kristo.  Kitu chochote kinachotesa ni sehemu ya laana ya torati, Yesu alifanyika laana ya torati, ili baraka za Ibrahimu zitufikie.  Yesu alikuwa sadaka ya ukombozi alikuwa sisi ili tuwe yeye, eneo mojawapo alilotukomboa au kutulipia ni katika umaskini.  Imeandikwa, “9Maana mmejua neema ya Bwana wetu Yesu Kristo, jinsi alivyokuwa maskini kwaajili yenu, ingawa alikuwa tajiri, ili kwamba ninyi mpate kuwa matajiri kwa umaskini wake.” (2Wakorintho 8:9). Jitambulishe mbele ya umaskini kuwa Yesu alishakuwa maskini, hivyo hutakuwa maskini kwa kuwa Yesu amelipia umaskini wako kwa yeye kuwa maskini badala yako.
Jitambulishe Katika Kristo
Kanisa letu tunaitwa “Word Drillers” kwa maana ya wachimba Neno.  Vito vya thamani huchimbwa haviko juu ya udongo! Askari mzuri hufanya “drill” kwa maana ya zoezi la kuweza kutumia silaha vizuri. Mwanafunzi mzuri naye hufanya “drill” kwa maana ya kujishughulisha akili yake aelewe masomo.  Hata sisi lazima neno la Mungu tulishibe, tulifanyie zoezi nk.  Katika agano jipya Yesu alikuja kutuingiza ndani yake.  Maandiko ya nyaraka hasa za Paulo, yameeleza sana muunganiko wetu na Kristo kwa kutumia maneno kama: Ndani yake, kwa yeye, kwa huyo, katika yeye, pamoja naye nk.  Tushike biblia zetu na kuzisoma, kukopi mistari hiyo na kuitumia kujitambulisha sisi binafsi.  Hamna namna nyingine ya kuishi maisha ya ushindi bila kujitambulisha katika Kristo, na uwezi kujitambulisha, mpaka uone umetambulishwaje, ujitambue na kuanza kujitambulisha.  Ukifanya hivi utajiona kiuthamani katika Yesu na vitu vibaya utaviona vina kupisha, ila tu tafuta kujitambua wewe ni nani katika Yesu, kwa kusoma ulivyotambulishwa katika nyaraka, kisha anza kujitambulisha.
Jitambulishe Ulipoketi
Sasa wanadamu walio katika Kristo Yesu wanaweza kumtawala Shetani,na kuweza kumpinga na kumdhibiti. Yesu alikuja kama mtu mwingine asiye na dhambi ili kuyarejesha aliyoyapoteza Adamu. Yesu amefidia maisha yetu kwa njia ya: 1. Kufa msalabani kwaajili ya dhambi zetu au kukataliwa kwetu 2. Kufufuka kwaajili ya haki au kukubalika kwetu 3. Kuketishwa mkono wa kuume kwa kushinda kwetu.
Yesu alipopaa na kuketi mkono wa kuume vitu vifuatavyo vilitokea, katika yeye vitu hivi unavyo pia:
1.      Alikuwa juu ya yote ikiwemo mamlaka zote za kibinadamu na kishetani , “19na ubora wa ukuu wa uweza wake; 20aliotenda katika Kristo alipomfufua katika wafu; akamweka mkono wake wa kuume katika ulimwengu wa roho; 21juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia; 22akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwaajili ya kanisa; ambalo 23ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote”(Waefeso 1:19-23).

2.      Tuliwekwa juu ya yote pamoja naye, juu ya mamlaka zote za kibinadamu, kishetani na malaika, “5hata wakati ule tulipokuwa wafu kwasababu ya makosa yetu; alituhuisha pamoja na Kristo ; yaani, mmeokolewa kwa neema. 6Akatufufua pamoja naye, akatuketisha pamoja naye katika ulimwengu wa roho, katika Kristo Yesu”(Waefeso 2:5-6).  “22Naye yupo mkono wa kuume wa Mungu, amekwenda zake mbinguni, malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.”(1 Petro 3:22).

3.      Alipewa jina kuu kuliko yote na akakeishwa juu ya majina yote “21juu sana kuliko ufalme wote, na mamlaka, na nguvu, na usultani, na kila jina litajwalo, wala si ulimwenguni humu tu, bali katika ule ujao pia;” (Waefeso 1:21), “Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lipitalo kila jina” (Wafilipi 2:9).

4.      Sisi pia tumepewa pamoja naye jina kuu kuliko yote na tupo juu ya majina yote, “22akavitia vitu vyote chini ya miguu yake, akamweka awe kichwa juu ya vitu vyote kwaajili ya kanisa; ambalo 23ndilo mwili wake, ukamilifu wake anayekamilika kwa vyote katika vyote.” (Waefeso 1:22-23).

5.      Ameonekana mbele za Mungu kwaajili yetu kwa damu yake, “Kwasababu Kristo hakuingia katika patakatifu palipofanyika kwa mikono, ndio mfano wa patakatifu halisi;  bali aliingia mbinguni hasa, aonekane sasa usoni kwa Mungu kwaajili yetu”(Waebrania 9:24). Mbele za Mungu tunakubalika kwa kuwa yupo kwaajili yetu pale, amwonapo anatuona sisi ndani yake ikiwa tumempa maisha yetu .

6.      Ametupa Roho wake toka mkono wa kuume, “Basi yeye, akiisha kupandishwa, hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya Roho Mtakatifu, amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia” (Matendo 2:33).


7.      Malaika na enzi na nguvu zimeshatiishwa chini yake. Malaika wote na enzi na nguvu zipo chini ya waamini maana wapo ndani ya Yesu   22Naye yupo mkono wa kuume wa Mungu, amekwenda zake mbinguni, malaika na enzi na nguvu zikiisha kutiishwa chini yake.”( (1 Petro 3:22).

Endelea Kujifunza Pamoja nami Wiki Ijayo pia ulisha na wengine, Barikiwa

No comments:

Post a Comment