Manabii (Prophetes)
Neno nabii limetokana
na maneno haya “Pro” yaani mbele, na
“Phemi”
yaani kujulisha wazo la Mungu au mtu, lisilojulikana. Manabii husema mambo ya
mbele na pia ya sasa kwa uvuvio wa Roho Mtakatifu. Kwa maana ya pili niliyoisema
hapo juu, Mchungaji mwalimu au mwinjilisti asemapo Neno wakati wa sasa kwa msukumo na
ufunuo wa Roho Mtakatifu, asemapo Neno hilo la wakati, husimama kama nabii kwa
wakati huo.
HALI HIZI
IKIWA ZINADUMU KWA MTU KATIKA HUDUMA INAWEZEKANA NI NABII AU ANA HUDUMA YA
KINABII
(a) Nabii ni mtu awezaye kujua wazo la Mungu la wakati
na kulisema au kulitenda. Anaweza kuwa haitwi nabii, lakini hali hii ni ya
kinabii.
(b) Nabii anapewa neema ya kujua wazo la moyo wa mtu
na kulisema (Matendo 5:3). Mara nyingine wazo la Mungu kuhusu mtu, watu au hali
ya nchi na anga la kiroho.
(c) Mungu humpa kujua ayaonayo Yeye (Mungu) wakati
ujao, wakati wa sasa au wakati uliopita (Matendo 11:27-30).
(d) Manabii hutengeneza misingi iliyoharibika na
kuimarisha misingi kwa njia ya kufundisha neno la Mungu kwa ufunuo wa Roho. Huduma ya mwalimu
afundishaye neno la wakati kwa ufunuo wa Roho inaweza kuitwa mwalimu wa
kinabii.
(e) Katika Agano jipya nabii hufanya kazi katika timu
ya huduma, sio peke yake, hufanya na viongozi wengine katika huduma tano. Huyu
siye mtu mmoja aliyejuu na wengine wote wako chini yake wakisubiri Mungu aseme
kupitia yeye tu, mfumo huu sio wa Agano Jipya. Katika Agano Jipya manabii
hufanya kazi katika timu (Matendo 13).
(f) Karama kuu katika huduma ya nabii ni neno la
maarifa, unabii, neno la hekima, kupambanua roho, mara nyingine karama za nguvu
kama miujiza, uponyaji na imani maalum. Kuna tofauti kati ya huduma ya nabii na
karama ya unabii, mtu akitumiwa katika karama ya unabii haimfanyi yeye kuwa
nabii.
(g) Mara nyingine huduma ya nabii hujificha katika
huduma nyingine. Kwa mfano mtu anaweza kuwa mwalimu, mchungaji au mwinjilisti na
hapo hapo ni nabii. Mfano wa mtu wa namna hii ni askofu Immanuel Lazaro.
(h) Manabii hupambanua nyakati za kiungu na majira ya
jambo kufanyika na kuwaandaa watu (Matendo 11:28, Matendo 21:10-11).
(i) Kila nabii ni mwombaji, lakini si kila mwombaji ni
nabii (Yeremia 27:18). Haiwezekani kuwa nabii bila kuwa mwombaji, ila
inawezekana kuwa mwombaji bila kuwa nabii.
(j) Utendaji kazi wa kinabii upo tofauti tofauti. Kuna
manabii waalimu (Kenneth Haggin), manabii wainjilisti(Charles Finney), manabii wachungaji,
manabii mitume na manabii walio manabii tu. Kuna manabii waimbaji, pia waombaji
manabii. Wakati wanaomba huona jambo na kulibadilisha kwa mamlaka au
kulisimamisha kwa mamlaka.
(k) Neno la kinabii linaposemwa ni vema lizalishwe
katika ulimwengu wa mwili kwa maombi na maombezi, maana adui hujaribu kuzuia
kusudi ka Mungu lililonenwa kinabii. Mfano mtoto aliyetabiriwa kuwa mtumishi,
Neno hilo latakiwa liatamiwe kwa maombezi limtokee.
(l) Manabii na maneno ya kinabii hujidhihirisha wakati
maalum (Kairos) na si wakati wote wa
masaa ishirini na nne (Kronos). Katika
Agano Jipya huduma hii haionekani sana pengine ni kwasababu ya udhihirisho
wa Roho Mtakatifu na sauti ya Mungu kwa kila mwamini.
(m)Nabii akitoa neno katika kundi wajibu wake huisha.
Wajibu unaofuata ni wa mchungaji, mwalimu au mtume kulithibitisha na kulijaribu
kwa maandiko na kulihakikisha, hata kama ni Mungu anasema (1Wathesalonike
5:20-21). Maandiko yana mamlaka ya mwisho kuliko neno la kinabii. Nabii lazima ajitiishe chini ya mamlaka ya maandiko.
(n) Muhubiri, mwalimu au mchungaji, anapofundisha
Neno la Mungu kwa uvuvio na ufunuo wa Roho Mtakatifu na kunena Neno la wakati,
ujumbe huo ni wa kinabii.
Mgongano
Mara nyingi huduma ya
nabii hugongana na mchungaji kwa sababu zifuatazo:
1. Nabii husema Neno, pasipo kujali hisia za
wasikilizaji.
2. Mchungaji hujali hisia za watu zaidi.
3. Nabii hutazama ujumbe aliopewa, Mchungaji hutazama
watu wanaosikia, inahitajika hekima ya kukaa na kuvumiliana. Katika kundi
mwenye neno la mwisho ni mchungaji, hivyo nabii ajizoeze kujitiisha kwa mchungaji,
wakati huo huo mchungaji asimdharau nabii.
4. Huduma ya nabii hufanya kazi kirahisi kwenye timu
za kitume na kiinjilisti zaidi ya kanisani (Matendo 13:1-3).
5. Huduma hii haionekani sana kwakuwa hatujatii
ipasavyo agizo kuu la kuufikia ulimwengu na injili.
6. Baadhi ya watumishi husema huduma hii haipo katika
Agano Jipya. Huo sio ukweli, huduma hii ipo ila utendaji kazi wake ni tofauti
na Agano la Kale. Ni hatari kanisa au huduma kuwepo bila ufunuo wa kinabii
kuwepo wakati wote kwa njia ya Roho Mtakatifu.
Muhimu: Mengi niliyoandika hapa yanatokana na ufahamu wa maandiko na uzoefu wa sehemu katika huduma, maishani mwangu na watumishi niliowahi kuwasikia au kuwafahamu kihuduma.
No comments:
Post a Comment