III
ANATUOKOA
ZABURI
91:3
MAANA YEYE
ATAKUOKOA NA MTEGO WA MWINDAJI NA KATIKA TAUNI IHARIBUYO
Atakuokoa
Neno lililotumika ‘Kuokoa’ toka mtego wa
mwindaji hapa ni “deliver” kwa Kingereza. Neno hili pia limetumika Mathayo 6:13,
“… utuokoe na yule mwovu” kwa
Kiyunani Neno hili ni Ryomai, ambalo
maana yake ni kutoa kitu katika hatari, kuvuta kitu haraka kwako, kutoka
mahali. Mfano mtoto anataka kuvuka barabara ukimvuta haraka kwako umemwokoa kwa
maana ya neno hili. Paulo alitumia neno hili (ryomai) alipoandika, “Bwana ataniokoa na kila neno baya, na
kunihifadhi hata nifike ufalme wa mbinguni ……” (2Timotheo 4:18). Tafsiri
yake, Bwana atanivuta haraka kwake nitoke katika kila neno baya na kuniifadhi
hata nifike ufalme wa mbinguni.
Hapa ametajwa mwindaji, lakini kutokana na
Mathayo 6:13 ametajwa Shetani, basi twaweza kusema, mwindaji anayetajwa hapa ni
Shetani ategaye mitego ya mauti.
Mtego
Neno mtego katika andiko hili ni “Snare” kwa lugha ya Kingereza. Katika
2Timotheo 2:26 imeandikwa, “Wapate tena
fahamu zao, na kutoka katika mtego wa Ibilisi, ambao hao wametegwa naye, hata
kuyafanya mapenzi yake.” Katika lugha ya Kiyunani neno Pagis limetumika hapa likimaanisha mtego. Lugha ya picha ya neno hili maana yake ni
mkakati uliofichika wa kukamata kitu. Ni jaribu la kumkamata mtu katika
maangamizi. Mungu katika Yesu Kristo anatuokoa na kila kitu cha kishetani kilichojificha
ambacho kusudi lake kitukamate na kutukosesha uzima wa milele. Sema hivyo, taja
majaribu ya tamaa ya mwili, macho na kiburi cha uzima. Mikakati yoyote ya
shetani maeneo hayo sema Mungu anakuokoa
na mtego wa mwindaji na itakuwa hivyo.
Tauni
Iharibuyo
Tauni ni ugonjwa unaosambaa na kuambukiza.
Tauni inayotajwa hapa ni ugonjwa wa kishetani unaoharibu. Neno iharibuyo hapa
limefanana na Ufunuo 16:2, kwa Kiyunani neno hili ni Kakos, ni kitu kibaya cha kuharibu, hasa kuharibu mwili. Mungu
anakutoa haraka anakuvuta kwake toka hatari ya mtego wa kishetani wa kufanya
umkosee, na magonjwa ya uharibifu wa mwili, sema hivyo.
ZABURI 91:4
KWA MANYOYA YAKE ATAKUFUNIKA CHINI YA MBAWA
ZAKE UTAPATA KIMBILIO. UAMINIFU WAKE NI NGAO NA KIGAO.
Andiko hili yaliyomo ndani yake kwa karibu
yanafanan na msitari wa 1 na wa 2. Ila sehemu ya pili ya uaminifu wake
tutaitazama.
Uminifu
Wake ni Ngao na Kigao
Neno uaminifu wake hapa katika tafsiri ya KJV,
kwa kiingereza ni “Ukweli”, “Ukweli wake ni ngao (shield) na kigao (buckler)”
PICHA NGAO
Ngao ni ktu au kinga
kubwa mfano, Wamaasai ngao zao ni kubwa. Akiiweka chini inaweza kufika hata
kifuani, katika Waefeso 6, ngao iliyotajwa ni ngao kubwa, askari akiishika
ilikuwa inaweza kuzuia au kukinga karibu mwili mzima. Ingeweza kupinga mishale,
panga, mawe nk. Umbo lake lilifanana na pembe tatu pia kwa ukubwa ilifanana na
ngao kubwa za Wamasai wazitumiazo wakipambana na simba.
Kigao ni kinga pia,
ila ilikuwa na umbo la mviringo. Ilitumika zaidi katika mapigano ya mapanga, na
haikuzuia mwili wote.
PICHA KIGAO
Uaminifu (Ukweli)
wa Mungu na Neno lake kwetu ni kinga! Unaweza kusema “Kinga yangu dhidi ya mashambulizi yote ya kishetani ni ukweli wa Mungu
na Neno lake ninalolisema.” Chochote unachokiona kinakushambulia au
kinatisha kinga yake ni ukweli wa kiungu. Ufikirie huo, usema huo
hutaangamizwa.
IV
HATUOGOPI
ZABURI 91:5-6
5 HUTAOGOPA HOFU YA USIKU WALA MSHALE URUKAO
MCHANA.
HUTAOGOPA
Woga ni “Smaku” ya kumvuta Shetani na
uharibifu. Imani ni ‘Smaku’ ya kumvuta Mungu na uzima. Kanuni ya kushindana na
Ibilisi ni kutoogopa. Mambo tuliyoyaona msitari wa kwanza mpaka wan ne
yanatufanya tusiogope. Hatuogopi kwa kuwa tumeketi ndani yake; tunadumu ndani
yake, tumezungukwa naye, hatuonekani na adui, tunapo pa kuponea na tumekingwa!
Kwa kuwa tunajua haya hatuogopi mashambulzi ya mchana au usiku. Hatuogopi jambo
lolote baya la usiku “hofu ya usiku” wala la mchana “mshale urukao mchana”
6 WALA TAUNI IPITAYO GIZANI WALA UELE
(UANGAMIVU) UHARIBUO ADHUHURI.
Tunapotembea tunavuta hewa hatujui kama ina
ugonjwa. Tunapokula hotelini tunatumia vijiko hatujui kama vimeoshwa vizuri.
Tauni ipitayo gizani ni magonjwa tusiyojua yapo yamejificha na hatuyaoni. Yapo
katika hewa, maji nk. Kwa kuwa tunajua ukweli wa Neno, tunakuwa na ngao na
kigao cha kutukinga. Kujua huku kunatufanya tusiogope! Hata kama tukisikia
dalili bado tunapo pa kukimbilia na pa kujifichia ni katika BWANA. Mwiko ni
kuogopa hatuogopi hatari za gizan tusizozijua tunapolala usingizi.
Maadui wote wanaopanga uharibifu wetu, gizani,
ni mfano wa hofu ya usiku. Mipango ya hila inayopangwa pasipo sisi kujua ni
mfano wa hofu ya usiku. Mambo yote wanayopanga magaidi kinyume chetu ni hofu ya
usiku. Hatuogopi hofu ya usiku tusiyoijua, wala mshale urukao chana, wala yale
tunayoyasikia na kuyajua hatuogopi. Tukisikia mchana wanasema watatuchinja
hatuogopi silaha hiyo ya kutisha, kwa nini? Ukweli wa Bwana! Unasema yeye ni
mahali pa kujifichia na kuwa salama, unasema tunapokaa uvulini pake hatuonwi na
adui! Hawatuoni ingawa wanatuona, tumefichwa, hatuogopi.
V
TUMETOFAUTISHWA
ZABURI 91:7
IJAPO WATU ELFU WAANGUKA UBAVUNI PAKO. NAAM,
KUMI ELFU MKONO WAKO WA KUUME! HATA HIVYO HAUTAKUKARIBIA WEWE.
Maneno ya andiko hili ni maneno yanaoonyeshwa
kutofautishwa. Musa aliona kutofautishwa kwa wana wa Israeli na Wamisri. Damu
iliwekwa juu ya miimo ya milango ya Waisraeli ikawatofautisha na wa Misri
hawakupigwa na malaika (Kutoka 12:13). Damu ndiyo iliyokuwa msingi wa agano wa
kuwatofautisha. Walitofautishwa na agango la damu. Kutoka 8:22 Inzi
walioisumbua Misri kama pigo hawakuwepo Gosheni kwa Waisraeli ingawa ilikuwa ni
hapo hapo. Mvua yam awe iliyopiga Misri haikupiga Gosheni (Kutoka 9:26).Hii
inaonesha kwamba walitofautishwa.Nini kiliwatofautisha? Walikuwa na Agano na
Mungu.
Andiko hili linaonyesha kwamba hata kama kuna
vitu vinaathiri dunia ambavyo vinatisha, tumetofautishwa na dunia havitatupata.
Tuonapo tatizo linawapata watu wote tuwaze na kusema moyoni mfano “Japo watu
elfu na makumi elfu wanakosa kazi, kukosa kazi hakutanipata mimi. Siko duniani nimo ndani ya Yesu
nimetofautishwa”
Safina iliwatofautisha Nuhu na watoto wake na
wake zao. Walipna kwa kuwa ndani ya Safina. Sasa tunapona na kutoautishwa kwa
kuwa ndani ya Yesu.
Kujiona na kujisema kuwa uko tofauti na dunia
na yaliyo duniani ni njia ya kuanza kushi kimiujiza na kuokolewa na hatari.
Taja kitu sema, “Ingawa watu maelfu na makumi elfu wanapata ajali na kufa na
kuvunjika haita nipata mimi katika Yesu Kristo”.
ZABURI 91:8 – 9
8 “ILA KWA MACHO YATO UTATAZAMA, NA KUYAONA
MALIPO YA WASIO HAKI.”
Maandiko yanasema tusimlipe mtu ovu kwa ovu.
1Petro 3:9). Mungu ndiye alipaye kisasi (Warumi 12:19). Tuendeleapo kumwona
Mungu kuwa ni ngome, kimbilio, ngao na kadhalika na kumsema hivyo, maadui zetu,
yeye atashughulika nao sisi haturuhusiwi. Baadaye tutaona kisasi chake mbele za
macho yetu. Sisi tukazane na kujiona salama kwa BWANA, tusijishughulishe na
watu, yeye atashughulika nao. Imba Bwana ni ngome, kimbilio, ngao, furahi na
kuimba wakati wote mengine mwachie yeye.
9 “KWA KUWA BWANA NDIWE KIMBILIO LANGU;
UMEMFANYA ALIYE JUU KUWA MAKAO YAKO.”
Ukweli wa andiko hili pia unaendana na msitari
wa 1,2 na wa tatu.
VI
TUNALINDWA
ZABURI 91:10-12
10 MABAYA HAYATAKUPATA WEWE, WALA TAUNI
HAITAIKARIBIA HEMA YAKO
11 KWA KUWA ATAKUAGIZIA MALAIKA ZAKE WAKULINDE
KATIKA NJIA ZAKO ZOTE
12 MIKONONI MWAO WATAKUCHUKUA USIJE UKAJIKWAA
MGUU WAKO KATIKA JIWE
Maandiko haya yanaonyesha kwa upana ulinzi wa
malaika. Tunapomwona BWANA kuwa ngome, kimbilio, ngao nakadhalika. Tunaposema
hivyo na kutoogopa, Huduma ya malaika inaachiliwa.
Malaika wanaendeshwa na maneno yetu (Zaburi
103:19-20). Tunaposema tupo sirini tumefichwa, yeye ni ngome malaika huagizwa.
Msitari wa kumi anasema mabaya na tauni hayatatupata: mabaya ni nini?Ni
uharibifu.Tauni ni magonjwa. Mara nyingine unapolala sema “Leo sitaota mabaya,”
siyo matendo tu haya ndoto au mawazo mabaya hatatupata”. Kumbuka mabaya
hayakupati kwa kuwa umetofautishwa katika agano la damu. Mabaya hayakuwapata
Israeli kwa damu iliyopakwa katika mti wa mlangoni (Mlangoni) Sasa mabaya
hayakupati kwa agano la damu ya mti wa msalaba.
Msitari wa kumi na moja anaanza kwa kusema
“kwa kuwa ……”, mabaya hayatupati kwa kuwa atatuangizia malaika zake, watulinde
katika njia zetu zote. Magaidi hawatajilipua makanisani mwetu kwa kuwa
atatuagizia malaika watulinde katika njia zetu zote. Wanatulinda hata na
amgonjwa.
Msitari wa kumi na mbili umeandikwa mikononi
mwao watatuchukua mguu wetu usijikwae katika jiwe. Hizi ni ajali zote za
kudhuru mwili kama ni kujichoma na msumari, kuungua, nakadhalika. Malaika wapo
wakati wote watuokoe.Kwa sababu ya Agano la damu ya Yesu lililotutofautisha.
ZABURI 91:13
UTAWAKANYAGA SIMBA NA NYOKA, MWANASIMBA NA
JOKA UTAWASETA KWA MIGUU.
Simba na nyoka ni ishara za Shetani (soma Luka
10:19, na 1Petro 5:6-8). Kukanyaga ni kukiweka kitu miguuni ni ishara ya kuwa
na mamlaka juu ya kitu hicho (Warumi 16:20, Luka 10:19). Kukaa sirini kwake
aliye juu, kumsema kama ngao na ngome hutupa uwezo wa kumdhibiti Shetani pande
zote, huachilia mamlaka ya kiungu ya kumtiisha. Tunaweza kudhihirisha tuko juu
ya kazi zote za kishetani; tukaapo katika Agano na kulisema. Hali hii itatupa
hari au ujasiri wa kumpinga adui na kuzitiisha kazi zote. Sema “Mungu ni ngome,
ngao, kimbilio, kweli.Malaika zake wanilinda. Kwa sababu hii Shetani aliye
nyoka na simba na kazi zake zote, mitego, magonjwa vimetiishwa chini yangu. Kwa
njia ya Yesu Kristo.”
VII
TUNAMPENDA
ZABURI 91:14 – 16
14 “KWA KUWA AMEKAZA KUNIPENDA NITAMWOKOA; NA
KUMEKA PALIPO JUU, KWA KUWA AMENIJUA
JINA LANGU”
15 “ATANIITA NAMI NITAMWITIKA NITAKUWA PAMOJA
NAYE TAABUNI NITAMWOKOA NA KUMTUKUZA”
16 “KWA SIKU NYINGI NITAMSHIBISHA NAMI
NITAMWONYESHA WOKOVU WANGU”
Maandiko haya tuyasomapo kupitia Yesu twaweza
kusema, “kwa njia ya Yesu ndani yangu ninampenda Mungu sana ananiokoa na hatari
zote na kuniweka palipo juu. Nakuwa juu kazini, shambani, katika lolote
nifanyalo kwa njia ya upendo wangu kwa Mungu kupitia Yesu ndani yangu.” Kwa
nini namtaja Yesu hapa, au kwa nini umtaje Yesu? Kwa kuwa huwezi kumpenda Mungu
na upendo wako ukakubalika bila Yesu Kristo. Upendo wetu kwa Mungu kwa njia ya
Yesu huleta ulinzi na wokovu maeneo yote. Kwa upendo wa Yesu ndani yetu ambao kwa
huo tunampenda Baba, tunaomba na kupokea. Mungu anakuwa nasi taabuni anatuokoa
na kututukuza.
Si hivyo tu katika agano hili la kulindwa na
Mungu anatuongezea siku nyingi, ajali, magonjwa, magaidi, wachawi na kitu
chochote hakitakatisha maisha yetu, kwa nini? Tunampenda, tumemjua jina lake,
tunamsema kama ngome, kimbilio, kweli na mwaminifu. Tunatiisha nguvu zote za
uharibifu kwa ufahamu huu. Kwa kufanya haya kwa neema uhai wetu na umri wetu
unaongezeka, adui mwindaji hatakatisha maisha yetu kwa mipango ya gizani
tusiyoijua, au ya mchana. Tunahifadhiwa sirini, tunakingwa nay eye.
Katika sura inayofuata tutaangalia mifano ya
jinsi tunavyoweza kujiombea ulinzi na usalama katika maisha yetu.
VIII
MAENEO
NYETI
Katika sura hii nimeainisha maendo kadhaa
ambayo unapaswa uyaombee ulinzi au uyakirie ulinzi ikiwekzekana kila siku.
Nitatumia baadhi ya vipengele vya Zaburi hii na vinginevyo. Haya ni maeneo
nyeti! Ambayo adui anayatafuta.
1.
MUSTAKBALI:
Shetani
anatafuta kuharibu mwisho wako, au kusudi lako la kuwepo. Anataka akutege
uanguke dhambini na kuacha mwisho wako au akuue kimwili. Tumia Zaburi 91:3 na
91:16. Yatamke maandiko haya na kujisema upo sirini katika Yesu na unakingwa na
kulindwa kama mume au mke wako ni mtumishi, mwombee maeneo haya.
2.
JINA
Jina
lako Shetani analiwinda alichafue. Jina likichafuka ni vigumu watu kukukubali.
Watu wasipokukubali huduma inakwama.Ila wasipokukubali kwa sababu ya Injii ni
sawa Mungu atakutetea, ila ikiwa umejaribiwa na kushindwa ni hatari jina lako
laweza kuharibika. Hapa unaweza kutumia Zaburi 91:15. Unatumia kuombea mtu au
kujiombea. Unasema kwa kuwa nakupenda Mungu kwa njia ya Yesu, unakuwa na mimi
katika taabu na majaribu, jina langu unaliokoa kuharibika, unalitukuza na
kulipa heshima kwa sababu ya Yesu.
3.
NDOA
Shetani
anawinda ndoa na familia kwa magonjwa, faraka nakadhalika. Anapanda mbegu
polepole mpaka uharibifu udhihirike. Anafanya hivyo ili kuharibu ushuhuda wa
huduma na wokovu. Unaweza kutumia Zaburi 91:3. Pamoja na Mathayo 15:13. Eneo
hili ni la kuombea mitego zaidi, vitu vilivyojificha (pia unaweza kusoma kitabu
nilichoandika kiitwacho Mitego ya Shetani).
4.
VIUNGO
Ombea
viungo vya mwili macho, masikio, ubongo, figo, maini, mapafu, nakadhalika.
Unaweza tumia Zaburi 19:10. Tamka mabaya kutokukupata wala tauni kukaribia
mwili (hema) lako. Tamka upofu hautakupata, kisukari hakitakupata, presha,
ugonjwa wa moyo na kadhalika. Endelea kwa kusema kwa kuwa atakuagizia malaika
wakulinde katika njia zako zote (Zaburi 91:11).
5.
MAJARIBUNI
Mtu
anapojaribiwa ni wakati wa hatari, inapaswa ahuishwe, na kulindwa Imani yake
pia kuokolewa. Ikiwa ni wewe au mtu mwingine mwombee kwa kutumia zaburi 138:7.
“Nijapokwenda katika shida utanihuisha, utanyosha mkono juu ya hasira ya adui
zangu na mkono wako wa kuume utaniokoa”, maombi haya I vema iwe desturi
kuyatamka kabla wakati una Amani. Ikitokea la kutokea utahuishwa na Mungu
atanyosha mkono na kukuokoa.
6.
MAMBO YA ASILI
Tunazungukwa
na hatari za mambo ya asili kama, upepo, mvua kubwa, radi, mafuriko, nyuki,
sumu, nk. Tunaweza kuikiri zaburi ya 91 ili kupata kinga ya mambo ya asili
yaliyo ya hatari. Unaweza kutengeneza ratiba ya kuyataja haya katika kalenda ya
mwezi.
7.
MAKUSANYIKO
Kwa
wakati wa sasa hali ya ugaidi ilivyo yatupasa kujua jinsi ya kuombea makundi ya
watu yawe salama, hasa makanisa. Hapa zaburi yote ya tisini na moja yaweza
kuombwa.
Ugaidi
ni roho ya woga. Shetani anatumia woga kuingia mahali. Magaidi nyuma yao yupo
Shetani ambaye anawatumia watumie kifo kuogopesha watu ili wakubali itikadi
yao. Maandiko yanasema, “hatutaogopa hofu ya usiku…..” Pamoja na ugaidi ni hofu
ya usiku, kwa ini kwa kuwa tupo sirini, tupo ngomeni, malaika wanatulinda,
tumetofautishwa. Zaburi 91:7,10-11 nk. Ni ya kutamka katika makusanyiko pamoja
na msitari wa 5 na 6.
Moja
ya njia ya kushindana na roho ya ugaidi, KWANZA ni kutoogopa! Unaposikia watu
wamechinjwa, au mahali pamelipuliwa au kuna tishio la kuuawa, kitu cha kwanza
USIOGOPE. Shetani mwenyewe yupo nyuma ya sauti hiyo inayotishia, ukiogopa tu ni
mlango.
Unapoona
hali ya woga, sema kitu. Upinge woga huo, utakuwa unampinga Shetani, (Yakobo
4:7) sema, “Sitaogopa hofu ya usiku wala mshale urukao mchana, ijapo watu elfu
wanaanguka ubavuni pangu na makumi elfu mkono wangu wa kuume, uharibifu wa
kigaidi hautanipata mimi/sisi. Ninakanyaga roho ya simba na nyoka, roho ya
kigaidi kwa jina la Yesu. Mungu ananiagizia malaika zake wananilinda katika
njia zangu zote haya yote yapo(Zaburi 91:5,7,11,13).
IX
DAMU YA YESU NA ZABURI 91
Katika
Agano la Kale kila kitu katika ibada kilikuwa na mahusiano na damu. Hata kitabu
cha torati kilinyunyiziwa damu (Waebrania 9:19-22)
Katika
Agano Jipya maandiko tunayoyakiri tunaweza yakiri kwa kuyachanganya na damu ya
Yesu. Kwa nini damu?
1.
Katika damu kuna nguvu ya ufufuo
ambayo inashinda mauti au nguvu ya Shetani “Basi, Mungu wa Amani aliyemleta tena kutoka kwa
wafu Mchungaji Mkuu wa kondoo, kwa damu ya agano la milele, yeye Bwana wetu
Yesu”(Waebrania 13:20)
2.
Katika damu tunakaa na Mungu,
tunakaribia na kukutana naye. Alipo Mungu, Shetani hayupo. “Lakini sasa, katika
Kristo Yesu, ninyi mliokuwa mbali hapo kwanza mmekuwa karibu kwa damu yake
Kristo.” (Waefeso 2:13)
3.
Katika damu hatuna hatia inayoweza mpa
Shetani haki ya kutushitaki, tunamshinda mashitaka yake kwa damu ya Mwana
Kondoo. Tumehesabiwa haki “Basi Zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu
yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye.” (Warumi 5:9) (Ufunuo 12:10-11)
4.
Uhai wa Yesu aliyesema Shetani hana
kitu kwake (Yohana 14:30), upo ndani ya damu yake. Tunapo itunia mbele za
Shetani, Shetani anamwona Yesu aliye ndani ya damu! Maana uhai wa mtu ndiyo
huyo mtu, uhai wa mnyama au inadamu unabebewa na damu, damu ilipo yuop mwenye
damu (Mambo ya Walawi 17:11)
5.
Damu imetununua au imetuhamisha.
Shetani hawezi kutugusa. Tumeingizwa katika ufalme wa Mungu kwa damu na kuwa
juu ya Shetani (Ufunuo 5:9, Wakolosai 1:13-14)
6.
Tunayo Amani na Mungu kwa damu. Mungu
ni rafiki yetu anatupa siri za adui, marafiki wanaamani na kupeana siri.
Tunamwakilisha duniani (Wakolosai 1:20)
Kwa hiyo tunaweza itumia Zaburi 91 yote kwa
kuichanganya na damu ya Yesu. Tufanyapo hivi tutamhusisha Yesu mwenyewe ndani
ya Zaburi nzima. Haya yatakuwa ni maombi ya Agano Jipya katika Zaburi 91.
Omba maombi haya na kuyarudia huku ukisoma
andiko katika Biblia yako
1.
Nimeketi mahali pa siri ndan ya Yesu Kristo
kwa damu yake. Nipo katika uvuli wa Mungu nimezungukwa na Mungu.
2.
Kwa damu ya Agano ya Yesu Kristo,
Bwana ndiye, mahali pa kuponea (kimbilio) langu na kinga (ngome) yangu Mungu
wangu nitakayemtumaini.
3.
Kwa damu ya Yesu ananiokoa na mtego,
hila yoyote ya kishetani na kila aina ya ugonjwa kwa damu yake. Napata mlango
wa kutoroka katika kila jaribu ambalo ni mtego (1Wakorintho 10:13).
4.
Kwa uwepo wa Roho wake Mtakatifu aliye
mfano wa hua mwenye mabawa na manyoya ananifunika kwa damu ya Yesu. Chini ya
mbawa za Roho Mtakatifu ninapata kimbilio. Uaminifu wake ni ngao, nakingwa na
uaminifu wake. Uaminifu wake ni kigao, nakingwa kwa kuwa ni mwaminifu.
5.
Kwa damu ya Yesu aliyesema usiogope
mimi ni wa kwanza na wa mwisho, sauti hii inasikika ndani ya damu yake sasa!
Siogopi hofu ya usiku, vitu vyote vinavyopangwa kinyume nami gizani. Wala vitu
vilivyo kinyume nami vya wazi.
6.
Kwa damu ya Yesu aliye Yesu kati yangu,
siogopi magonjwa: kisukari, presha, ugonjwa wa moyo na mengineyo. Wala
uharibifu (nele) wowote unaoweza kutokea mchana. Ikiwa ni ugaidi, ujambazi,
wizi na mengineyo.
7.
Ijapo kila mtu anaonekana kuathiriwa
na hatari zilizopo sasa, hatari za kiuchumi, kimwili, na kiroho. Mimi
nimetofautishwa kwa damu ya Yesu. Kama vile wana wa Israeli walivyotofautishwa
na Misri hawakupigwa. (Kutoka 2:13) Kwa damu ya Yesu nimetofautishwa na dunia,
yanayoipata dunia hayanipati. Biblia inasema “ole wao wakaao katika nchi maana
Shetani ametupwa huko akijua wakati wake ni mchache” (Ufunuo 12:12). Mimi
nimeketishwa na Yesu mbinguni (Waefeso 2:5-6) Shetani yupo chini yangu.
Nimefichwa katika Yesu (Wakolosai 3:1-3) sionekani na Shetani. Nimezingirwa na
Mungu sipo duniani ingawa nipo.
8.
Ndani ya Agano la damu ya Yesu kazi
yangu ni kutazama malipo ya maadui zangu. Kazi yangu si kulipa kisasi ni
kutazama. Kwa damu ya Yesu naona nguvu za giza zikidhibitiwa, hakuna Shetani
ashindaye kisasi cha Bwana kinaonekana.
9.
Wewe Bwana kwa njia ya damu ya Yesu
ndiyo kimbilio langu, mahali pa kuponea kwa jia ya damu ya Yesu nakaa na wewe
nimekukaribia.
10.
Mabaya hayatanipata nilipo ndani yako
kwa damu ya Yesu. Ninapolala, ndoto mbaya haizinipati katika fikra, hakuna
mwizi wla jambazi wala mchawi. Tauni na ugonjwa wowote haukaribii mwili wangu,
nyumba yangu, familia yangu (hema). Kwa kuwa nipo mahali pa kuponea katika
Bwana kwa damu ya Yesu.
11.
Kama mrithi wa wokovu katika agano la
damu ya Yesu malaika wananihudumia (Waebrania 1:14). Wananilinda katika njia
zangu zote. Ninapotembea, ninaposoma, ninapokula, ninapohubiri, ninapoongea na
watu nk. Hatari itakapokutokea ghafla utaniagizia malaika hata Zaidi ya waliopo
kuniokoa. Malaika kwa agano la damu wananilinda na magonjwa ambukizi.
12.
Kwa damu ya Yesu malaika wananishika
na kuniokoa na ajali yoyote ya kuniumiza mwili. Kuanzia kujikwaa mpaka
kupinduka au kugongwa na gari. Hakuna kiungo change kitakachovunjika.
Ikikaribia kutokea hivyo malaika wataninyanyua ghafla! Kama mwana wa Agano la
damu.
13.
Nimenunuliwa kwa damu, siko chini ya
sheria, dhambi na Shetani. Kwa damu ya Yesu nimetolewa ndani ya nguvu za giza.
Nimeingizwa ndani ya Mungu kwa damu. Sasa niko juu ya simba na nyoka. Ninayo
amri/mamlaka ya kukanyaga nyoka, nnge, na simba. Nguvu zote za kishetani katika
Kristo Yesu ndani ya damu yake nazizuia kufanya kazi mwilini, katika mawazo kwa
watoto nk.
14.
Kwa njia ya agano la damu ya Yesu
nimezaliwa mara ya pili. Upendo wa kumpenda Mungu umo ndani yangu kwa Roho
Mtakatifu (Warumi 5:5). Kwa upendo huu kwa Mungu ananiokoa na kuniweka palipo
juu. Nafasi yangu inabadilika! Kila nilipo nakuwa kichwa kwa kuwa nimemjua jina
lake Mungu.
15.
Katika Kristo Yesu ndani ya damu yake
ninasikiwa na Mungu ninapoomba. Nipo sirini ndani yake nipo karibu naye.
Anakuwa pamoja nami ninapoomba uwepo wake unakuwa na mimi! Ananiokoa na
kuniinua.
16.
Katika Kristo Yesu kwa damu yake,
ninashibishwa siku nyingi kwa kuwa nina haki yake. Nashibishwa siku nyingi kwa
kuwa nimefichwa ndani yake. Nimeketi, nimekaa, nimezingirwa, nimekingwa! Maadui
wa kukatisha maisha magaidi, mapepo, magonjwa, hofu na vyote viharibuvyo
havitanipata.
Asante Yesu kwa Agano la damu.
Amen
Maombi haya unaweza kuyasoma huku unaomba.
Huku pembeni ukisoma na Andiko. Rudia, rudia
mpaka upate ufahamu wako binafsi. Usifungwe na mambo haya niliyoandika
huo ni mfano tu. Mungu anaweza kukupa upana zaidi.
UMEBARIKIWA!
THANKS SERVANT OF GOD
ReplyDelete