Saturday, December 29, 2018

KUTAMBULISHWA, KUJITAMBUA, KUJITAMBULISHA :: [IV] TUMETAMBULISHWA

Mungu ameleta maandiko matakatifu kwasababu nyingi, kwanza kabisa ni ili tumjue yeye.  Pili ni ili tupate kujua jinsi ya kuenenda, tatu tujijue sisi ni kina nani.  Hapa ni kabla hatujampa Yesu maisha, tujijue sisi ni wenye dhambi, na baada ya kumpa Yesu maisha tujijue sisi ni nani katika Yesu Kristo. Kwa kusema hivi kazi ya maandiko ni kututambulisha.
Katika agano la kale Mungu amewatambulisha watu wake kwa njia ya maandiko: “6Mimi nimesema, Ndinyi miungu, Na wana wa aliye juu, nyote pia.” (Zaburi 82:6). Katika Isaya Mungu amewatambulisha Israeli katika maandiko, “8Nawe, Israeli, mtumishi wangu; Yakobo, niliyekuchagua; mzao wa Ibrahimu rafiki yangu.” (Isaya 41:8).  Si maandiko haya tu Mungu anayotabia ya kutambulisha watu wake katika Agano alilonalo na wao.
Sehemu kubwa ya Agano jipya au kusudi moja wapo la Agano jipya ni utambulisho wa waamini na Yesu Kristo.  Biblia inaonyesha utambulisho wetu pamoja na Yesu, au katika Yesu.  Utambulisho wetu ni pamoja na Yesu, na tunaujua katika maandiko.  Angalia andiko hili la ajabu, “29Maana wale aliowajua tangu asili, aliwachagua tangu asili wafananishwe na mfano wa Mwana wake, ili yeye awe mzaliwa wa kwanza miongoni mwa ndugu wengi.” (Warumi 8:29). Kusudi la Mungu kumleta Yesu ni wanadamu wote wawe kama Yeye, msalaba ndio msingi wa kutimiza lengo hili.  Chanzo cha kusudi hili ni kumwamini kama Bwana na Mwokozi, kwa njia ya kazi yake msalabani kisha kuwa wanafunzi wake. Kujua utambulisho wetu katika Yesu Kristo ni msingi mkubwa wa kufikia kusudi hili, la kufananishwa na Kristo.  Kuujua utambulisho wetu katika Kristo kwa njia ya maandiko ni mlango wa kutufikisha katika ufanano na Kristo alioukusudia Mungu, pia kuweza kusimama kiimani na mamlaka katika hali yeyote ngumu.
 Utambulisho wa maandiko kwa waamini kwa sehemu kubwa unaonekana katika nyaraka za agano jipya.  Nyaraka za agano jipya ziliandikwa kwaajili ya waamini, kwa hiyo zinao utambulisho mkubwa wa sisi ni nani kwa njia ya Yesu.

Unaposoma Biblia hasa nyaraka tafuta mambo yasiyopungua yafuatyo: Yesu alifanya nini mbele za Baba kwaajili yako, Yesu alifanya nini mbele za Shetani kwaajili yako, unacho kitu gani ndani ya Yesu, Wewe ni nani katika Yesu, Yesu ni nani ndani yako. Vipengele hivi vitano, ndiyo ramani ya maandiko kukutambulisha. Ndiyo misingi ya kujitambua kama tutakavyoona sehemu itakayofuata.

No comments:

Post a Comment