Yesu yupo ndani yetu tuaminio, kama ilivyoandikwa katika
Ufunuo 3:20. Ili kumjua Yesu aliye ndani
yako yukoje, angalia alijitambulishaje. Katika maisha yangu huwa namsema Yesu
mara kwa mara kama alivyojitambulisha na namwona, ingawa simwoni kwa macho ya nyama, yupo pamoja
nami kama ninavyomsema. Huwa namtafakari kama alivyojitambulisha, pia namsema,
mara zote nikifanya hivi hutiwa nguvu na kuwa na msimamo mkuu kiimani.
Kuna wakati nilipata msukumo mkubwa moyoni wa kufunga na
kuomba kwa muda, nilikuwa nakula jioni tu.
Mwishoni mwa mfungo huo nilijifunza mbele za Mungu somo liitwalo, “Nafsi
ya Kristo Yesu”, ambayo unailewa katika maandiko kwa maneno aliyotumia Yesu
kujisema kama, “Mimi”, “Kwangu”, “Langu” nk.
Baada ya muda mfupi nilipata jaribu baya! Ambalo bila kukaa katika Nafsi
ya Yesu Kristo lingenipeperusha kama makapi yapeperushwavyo na upepo. Nilijifunza kumtambulisha Kristo kama
alivyojitambulisha, huu ni ufunguo wa kuweza kusimama katika hali yoyote ngumu.
Yesu alijitambulisha kama alivyotambulishwa na Baba
hakujitambulisha yeye tu, “17Tena katika
torati yenu imeandikwa kwamba, Ushuhuda wa watu wawili ni kweli. 18Mimi ndimi
ninayejishuhudia mwenyewe, Naye Baba aliyenipeleka ananishuhudia.” (Yohana
8:17-18). Kwa maneno mengine Yesu
alikuwa anasema, mimi ninajitambulisha mwenyewe na Baba aliyenipeleka ananitambulisha.
Sehemu hii tutaangalia maeneo saba ambayo Yesu
alijitambulisha, ambayo yatupasa tumtambulishe wakati wote katika maisha yetu. Amejitambulisha
si kwa namna hizi saba tu, nyingine zitafute mwenyewe usomapo injili nne, hizi
ni za msingi tunaojiwekea kumjua katika kitabu hiki ila zipo zaidi.
MIMI SABA (UTAMBULISHO MKUU WA YESU)
Njia
“6Yesu akamwambia, Mimi
ndimi njia, na kweli, na uzima, mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.”
(Yohana 14:6). Yesu amejitambulisha kuwa pekee ndiyo njia ya kumfikia Mungu. Wakati unakutana na hali
unaona hata Mungu huwezi mfikia, au hawezi kukusikia, Mtaje Kristo au Nafsi ya Kristo
kama Njia. Hii si wakati wa jaribu tu, wakati wote mtambulishe hivi katika
maisha yako.
Ufufuo
“25Yesu akamwambia,
Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa
anaishi. Naye kila aishiye na kuniamini
hatakufa kabisa hata milele, je unayasadiki hayo” (Yohana 11:25). Kila binadamu atafufuliwa ama katika ufufuo
wa kwanza wa wenye haki au ufufuo wa pili wa wenye dhambi. Mtu asiye na Yesu amekufa kiroho, aliye na
Yesu yu hai kiroho, Yesu anaonyesha huyu atakuwa hai milele katika Kristo Yesu
na ataingia katika ufufuo wa kwanza wa wenye haki yaani uzima wa milele. Mtambulishe Yesu wakati wote katika maisha
yako ya milele kuwa yeye ndiye ufufuo na uzima na katika yeye unaishi milele.
Nuru
“46Mimi nimekuja ili
niwe nuru ya ulimwengu, ili kila mtu aniaminiye mimi asikae gizani.”
(Yohana 12:46), “12Basi Yesu akawaambia
tena, Mimi ndimi nuru ya ulimwengu, yeye anifuataye hatakwenda gizani kamwe,
bali atakuwa na nuru ya uzima.” (Yohana 8:12). “9Muda
nilipo ulimwenguni, mimi ni nuru ya ulimwengu.” (Yohana 9:5). Nuru ni kanuni ya ufalme wa Mungu ambayo
ndani yake inaleta utendaji wa Mungu na utawala wake. Dunia ina kanuni ya giza na utawala wa
Shetani, Yesu amekuja alete kanuni ya nuru na utawala wa Mungu. Wakati wote umsemapo kuwa Nuru na
kumtambulisha hivyo katika ulimwengu wa roho, basi utendaji wa ufalme wa Mungu
huachiliwa wakati wote maishani mwako, na giza la namna yeyote haliwezi
kushinda maishani mwako.
Mzabibu
“5Mimi ni mzabibu;
ninyi ni matawi; akaaye ndani yangu nami ndani yake; huyo huzaa sana; maana
pasipo mimi ninyi hamwezi kufanya neno lolote” (Yohana 15:5). Katika hazi zote chanzo cha uhai na utendaji
wetu ni Yesu. Hatuwezi kuwa na matunda
au matokeo ya kudumu ni katika muunganiko wetu na Yesu tu. Katika vita vya kiroho Yesu ni Mzabibu,
tunazaa kushinda kwake. Katika huduma
Yesu ni Mzabibu tunahudumu na kupata matokeo katika neema ya roho wake. Katika familia zetu Yesu ni Mzabibu, tunayo
amani upendo wake kati yetu. Katika
ushirika wetu kanisani Yesu ni Mzabibu anatupa uhai wake kila siku tudumu
katika wokovu. Wakati wote maishani
mtambulishe kwako kama Mzabibu.
Mchungaji
“11Mimi ndimi mchungaji
mwema. Mchungaji mwema huutoa uhai wake
kwa ajili ya kondoo.” (Yohana 10:11).
Yesu ni mchungaji wetu, neno hili Mchungaji ni kila kitu kwa ajili
yetu. Anahusika na maeneo yote ya maisha
yetu. Maandiko haya yanasema anautoa
uhai wake kwaajili ya kondoo. Hii ni
sawa na kusema yeye ndinye anayeyalipia au kuyafidia mahitaji yetu yote (Marko 10:45). Mtambulishe hivi Yesu maishani mwako wakati
wote kama alivyojitambulisha.
Mlango
“7Basi Yesu aliwaambia
tena, Amin, amin, nawaambieni, Mimi ndimi mlango wa kondoo. 8Wote walionitangulia ni wengi na
wanyang’anyi; lakini kondoo hawakuwasikia.
9Mimi ndimi mlango mtu akiingia kwa mimi ataokoka, ataingia na kutoka,
naye atapata malisho. 10Mwivi haji ila aibe na kuchinja na kuharibu; mimi
nalikuja ili wawe na uzima, kisha wawe nao tele.” (Yohana 10:7-10). Wachungaji wa kondoo zamani za Biblia pia
waliitwa milango ya kondoo. Wao ndio
walikaa sehemu ya kutokea au kuingilia zizini, hivyo wao wenyewe kuwa
milango. Yesu ndiye tuliyeingilia kwaye
katika ufalme. Hakuna aweza kututoa
maana yeye ndiye yupo sehemu ya kuingilia, katika yeye tuko huru zizini tunaingia
na kutoka na kupata malisho. Ndani ya
zizi tunajua mlango wetu alikuja tuwe na uzima kisha tuwe nao tele, harakati
zote za mwizi kuiba kuchinja na kuharibu hazitashinda maishani mwetu.
Chakula
“51Mimi ndimi chakula
chenye uzima kilichoshuka kutoka mbinguni.
Mtu akila chakula hiki ataishi milele.
Na chakula nitakachotoa mimi ni mwili wangu, kwaajili ya uzima wa
ulimwengu.” (Yohana
6:51). Chakula ni chanzo cha nguvu, afya
na maisha. Wana wa Israeli waliutegemea
mkate wa mana kuishi jangwani. Sisi
twamtegemea Yesu kama chakula chetu kuishi duniani. Meza ya Bwana ni alama kubwa na kiimani
kutekeleza hili (Usome kitabu nilichoandika kiitwacho, “Meza ya Bwana, Jinsi ya
kuitumia”).
Hatuwezi kupitia maeneo yote aliyojitambulisha, kwa wewe
binafsi soma injili nne na ukusanye maandiko yote yanayoonyesha nafsi ya
Yesu. Ni muhimu kuyaelewa kwaajili ya
kuishi na nafsi ya Yesu. Hakikisha
unamsema Yesu wakati wote kama alivyojitambulisha. Rudia rudia tena na tena mpaka iwe sehemu ya
maisha yako kabisa. Kuna maisha mapya
utaona yanajidhihirisha, haya ni maisha ya Yesu wenyewe. Hata kama huelewi sana unachokisema sema tu!
Hizo zitakuwa ni mbegu ambazo hujajua zitaotaje na kukuaje lakini zitaota na
kukua, na kumdhihirisha Yesu maishani mwako.
Usikose muendelezo wa somo hili wiki ijayo. Wajulishe na Wengine.
Sambaza Blogu hii kadiri uwezavyo ili kuwasaidia na wengine katika Kumjua Yesu na Kuudhirhirisha Ufalme wa Mungu katika Maisha yetu ya kila siku.
No comments:
Post a Comment