Saturday, December 15, 2018

KUTAMBULISHWA, KUJITAMBUA, KUJITAMBULISHA :: [II] YESU ALITAMBULISHWA

Zipo sababu kadhaa za Mungu kumtambulisha mtu, kwa mfano Mungu aliitambulisha Israeli kwasababu ya kutukuzwa kwake, “akaniambia; Wewe u mtumishi wangu, Israeli, ambaye katika wewe nitatukuzwa.” (Isaya 49:3). Mungu hutambulisha pamoja na sababu nyingine, hutambulisha kuonyesha kusudi lake juu ya huyo anayemtambulisha. Hapa aliitambulisha Israeli kuonyesha ipo  kwaajili ya kumtukuza.
Imeandikwa, “1Tazama mtumishi wangu nimtegemezaye; mteule wangu, ambaye nafsi yangu imependezwa naye; nimetia roho yangu juu yake; naye atawatolea mataifa hukumu. 2Hatalia, wala hatapaza sauti yake, wala kuifanya isikiwe katika njia kuu. 3 Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utoao moshi hatauzima; atatokeza hukumu kwa kweli. 4Hatazimia wala kukata tamaa, hata atakapoweka hukumu duniani; na visiwa vitaingojea sheria yake” (Isaya 42:1-4). 
Mungu alikuwa anamtambulisha Yesu katika maneno haya ya Isaya.  Katika Mathayo 12:9-18, baada ya Yesu kuponya mtu aliyepooza na watu wengine wengi waliomfuata, aliwakataza wasimdhihirishe, ndipo maandiko haya ya Isaya ya kumtambulisha yakatajwa. Imeandikwa msitari wa 18 mpaka 21, “18Tazama, mtumishi wangu niliyemteua; Nitatia roho yangu juu yake, Naye atawatangazia Mataifa hukumu. 19Hatateta wala hatapaza sauti yake; wala mtu hatasikia sauti yake njiani. 20Mwanzi uliopondeka hatauvunja, wala utambi utoao Moshi hatauzima, hata ailetapo hukumu ikashinda. Na jina lake Mataifa watalitumainia.” (Mathayo 12:18-21).
Maandiko mengine yanasema, “12Tazama, mtumishi wangu atatenda kwa busara, atatukuzwa, na kuinuliwa juu, naye atakuwa juu sana.” (Isaya 52:12).  Mungu hapa alikuwa anamtambulisha Yesu atakayekufa na kufufuka kisha kuketishwa juu sana kama ilivyoandikwa, “9Kwa hiyo tena Mungu alimwadhimisha mno, akamkirimia jina lile lipitalo kila jina.” (Wafilipi 2:9).
Sehemu mojawapo katika maandiko ya Isaya, Mlango 42, msitari wa kwanza imeandikwa, “…nafsi yangu imependezwa naye”.  Katika agano jipya Mungu Baba alimtambulisha Yesu kwa usemi huu “ninayependezwa naye” alitambulishwa hivi sehemu mbili.
BAADA YA KUJAZWA ROHO
Yesu alitambulishwa mbele ya Wayahudi na sauti ya Mungu moja kwa moja toka mbinguni wakati anabatizwa.  Alipobatizwa tu, Roho alimshukia na sauti ya Mungu ilisikika, “16Naye Yesu alipokwisha kubatizwa mara akapanda kutoka majini; na tazama, mbingu zikamfunukia, akamwona Roho wa Mungu akishuka kama hua, akija juu yake; 17na tazama, sauti kutoka mbinguni ikasema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye.” (Mathayo 3:16-17). 
Israeli katika torati walipewa sadaka za wanyama hasa kondoo ili kuwa ishara ya kuchukua dhambi zao, au kuwalipia dhambi zao.  Wakati Yesu anabatizwa, Mungu alikuwa anamdhihirisha kwa Israeli kwa sauti yake toka mbinguni. Hii bila shaka ilikuwa ni alama aliyowapa ya kumtambua kama Masihi.  Yohana mbatizaji alipewa ishara ya kuwa atakayemwona akishukiwa na Roho, huyo ndiye abatizaye kwa Roho Mtakatifu, ni mtu wa pekee, ni Masihi.  Yohana bila shaka kwa uwezo wa Roho alimtambulisha kuwa ni Mwanakondoo wa Mungu aichukuaye dhambi ya ulimwengu, akiwa na maana ya Masihi, aliyepakwa mafuta awe sadaka ya dhambi na baadaye Kuhani na Bwana.  Hapa Yohana Mbatizaji kwa msingi alikuwa anaonyesha kama nabii, kuisha kwa sadaka zote za wanyama za agano la kale, kwa sura ya kondoo, na zote kutimia katika Masihi Kristo Yesu.  Imeandikwa, “29Siku ya pili yake amwona Yesu anakuja kwake, akasema, Tazama, Mwana-Kondoo wa Mungu, aichukuaye dhambi ya ulimwengu! 30Huyu ndiye niliyenena habari zake ya kwamba, Yuaja mtu nyuma yangu, ambaye amekuwa mbele yangu; kwa maana alikuwa kabla yangu. 31Wala mimi sikumjua; lakini kusudi adhihirike kwa Israeli ndio maana mimi nalikuja nikibatiza kwa maji. 32Tena Yohana akashuhudia akisema, nimemwona Roho akishuka kama hua kutoka mbinguni; naye akaa juu yake. 33Wala mimi sikumjua; lakini yeye aliyenipeleka  kubatiza kwa maji, huyo aliniambia, Yeye ambaye utamwona Roho akishuka na kukaa juu yake, huyo ndiye abatizaye kwa Roho Mtakatifu. 34Nami nimeona, tena nimeshuhudia ya kuwa huyu ni Mwana wa Mungu” (Yohana 1:29-34).
Ubatizo wa Yohana ulikuja ili Mungu amtambulishe Yesu kuwa ni Mwana wa Mungu. Hizi ni alama zake: 1. Sauti ya Mungu toka mbinguni 2. Roho Mtakatifu kumshukia 3. Mwanakondoo wa Mungu 4. Abatizaye kwa Roho Mtakatifu.  Kazi ya ubatizo wa Yohana ilikuwa kumtambulisha Yesu, kazi ya ubatizo wa kanisa ni kututambulisha sisi katika kufa, kuzikwa na kukufuka na Yesu.
Tukirudi Isaya 42:1 na Mathayo 3:17, Mungu alimtambulisha Yesu wakati wa kubatizwa kuwa amependezwa naye. Mapenzi ya Mungu yote ni katika Kristo Yesu.  Kwa namna nyingine Mungu alikuwa anawatambulisha Wayahudi na Yohana ya kwamba katika Yesu Kristo tu, mapenzi yake yote yatatimizwa.
Wakati wa utambulisho huu wanafunzi wa Yesu au Mitume, ambao ni msingi wa kanisa walikuwa hawapo. Mungu alimtambulisha tena kwa mfano kama huu kwa mitume.
KABLA YA KUSULUBIWA
Mungu alimtambulisha Yesu ukuu wake na utukufu ujao, kabla hajasulubiwa. Kufufuka kwa Yesu katika wafu, ndio ulikuwa utangulizi wa Yeye kupewa utukufu, “21ambao kwa yeye mmekuwa wenye kumwamini Mungu, aliyemfufua katika wafu akampa utukufu; hata imani yenu na tumaini lenu liwe kwa Mungu.” (1Petro 1:21).  Alimtambulisha mbele ya wanafunzi wake, na kuuonyesha utukufu wake ujao, kabla hajasulubiwa na kufufuliwa, kuhusu hili Petro aliandika, “17Maana alipata kwa Mungu Baba heshima na utukufu hapo alipoletewa sauti iliyotoka katika utukufu mkuu, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye. 18Na sauti hiyo sisi tuliisikia ikitoka mbinguni tulipokuwa pamoja naye katika mlima ule mtakatifu. (2 Petro 1:17-18). Kusudi la Mungu kumdhihirisha Yesu kwa sauti akiwa na wanafunzi wake, ilikuwa kuwaonyesha utukufu, heshima na nguvu alizokuwa nazo Kristo na hasa utukufu wake ujao, katika ufalme wa Mungu. Yohana aliandika, “14Naye Neno alifanyika mwili, akakaa kwetu; nasi tukauona utukufu wake, utukufu kama wa Mwana pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli.” (Yohana 1:14).  Inawezekana kabisa utukufu anaosema Yohana hapa ni ule waliomwona nao Yesu pale mlimani wakiwa na Petro,  maana walikuwa wote siku hiyo.  Walionyeshwa utukufu wake ujao!
Hebu tuangalie tukio lenyewe lilivyotokea kama ilivyoandikwa katika Luka.  Imeandikwa, Nami nawaambia kweli, Wapo katika hawa wanaosimama hapa, ambao hawataonja mauti kabisa, hata wauone kwanza ufalme wa Mungu (bila shaka alikuwa anazungumzia ufalme akiwa na maana ya utukufu ambao walikuwa wanaenda kumwona nao pale mlimani baada ya siku nane). Baada ya maneno hayo yapata siku nane, aliwatwaa Petro na Yohana na Yakobo, akapanda mlimani ili kuomba.  Ikawa katika kusali kwake sura ya uso wake ikageuka, mavazi yake yakawa meupe, yakimeta-meta. Na tazama, watu wawili walikuwa wakizungumza naye, nao ni Musa na Eliya; walioonekana katika utukufu, wakinena habari za kufariki kwake atakakotimiza Yerusalemu (9:27-31).
Katika kitabu cha Mathayo imeandikwa hivi, “1Na baada ya siku sita Yesu akawatwaa Petro, na Yakobo, na Yohana nduguye, akawaleta juu ya mlima mrefu faraghani; 2akageuka sura yake mbele yao; uso wake ukang’aa kama jua, mavazi yake yakawa meupe kama nuru. 3Na tazama, wakatokewa na Musa na Eliya, wakizungumza naye…. 5Alipokuwa katika kusema, tazama, wingu jeupe likawatia uvuli; na tazama, sauti ikatoka katika lile wingu, ikisema, Huyu ni Mwanangu, mpendwa wangu, ninayependezwa naye; msikieni Yeye.” (Mathayo 17:1-5).
Kwa ujumla maandiko haya ya Mathayo na Luka yanaonyesha vitu kadhaa katika utambulisho huu wa Mungu. Kwanza ni kionjo au arabuni ya utukufu ambao Kristo angeupata au ameupata baada ya kufufuka katika wafu na kupaa mpaka mkono wa kuume. Ukiangalia anavyotajwa Ufunuo wa Yohana, inafanana sana na alivyoonekana mlimani akiwa na wanafunzi, uso wake ulingaa kama jua, hivi ndivyo ilivyokuwa alipofufuka, katika Ufunuo utukufu wake umeonekana kwa upana. Imeandikwa, “16Naye alikuwa na nyota saba katika mkono wake wa kuume; na uso wake kama jua liking’aa kwa nguvu zake.” (Ufunuo 1:16).  Unaweza anzia msitari wa kumi na nne ili kumwona katika hali yake ya utukufu.
Kitu kingine tunachoona ni uwepo wa Musa na Eliya.  Hawa bila shaka wanawakilisha Torati (Musa) na Manabii (Eliya), kisha Mungu anamtambulisha Yesu kuwa ni Mwana wake tumsikie Yeye, siyo Torati tena wala Manabii.  Torati na Manabii wote walikuja kuandaa njia ya Mungu kusema kwa kupitia Yesu tu.  Musa na Eliya walikuja kuongea naye kuhusu kifo chake kitakachotimizwa Yerusalemu.  Torati na manabii pia vilikuwa vinaonyesha kuhusu sadaka ya Kristo kulipia dhambi za binadamu, kwa mfano wa Musa na Eliya.
Kwa kuwa Yesu alikuwa amekaribia kufa, bila shaka Mungu aliona awaonjeshe wanafunzi, utukufu, ukuu na uweza atakaoupata akifufuka, ili watiwe moyo kipindi cha mateso yake. Hivyo akamtambulisha kwa jinsi hii kama vile tulivyoona.
ALIMTAMBULISHA KWA PETRO
Kumtambua Yesu kikamilifu inahitajika roho ya neema katika ufunuo wa Roho Mtakatifu.  Hatumjui kwa kutumia akili zetu.  Wanafunzi wa Yesu waliishi naye uso kwa uso lakini kumwelewa hawakuweza ni mpaka Roho Mtakatifu/Mungu Baba, alipowafundisha ndipo walipoweza kumwelewa.  Hebu angali maandiko haya, “13Basi Yesu akaenda pande za Kaisaria-Filipi, akawauliza wanafunzi wake akasema, Watu hunena kuwa Mwana wa Adamu ni nani? 14Wakasema, Wengine hunena u Yohana Mbatizaji, wengine Eliya, wengine Yeremia au mmojawapo wa manabii. 15 Akawaambia, Nanyi mwaninena mimi kuwa ni nani?16 Simon Petro akajibu akasema, Wewe ndiwe Kristo, Mwana wa Mungu aliye hai. 17Yesu akajibu, akamwambia, Heri wewe Simon Bar-yona, kwa kuwa mwili na damu havikukufunulia hili; bali Baba yangu aliye mbinguni. 18 Nami nakuambia, Wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu; wala milango ya kuzimu haitalishinda. 19Nami nitakupa wewe funguo za ufalme wa mbinguni; na lolote utakalolifunga duniani , litakuwa limefungwa mbinguni; na lolote utakalolifungua duniani, litakuwa limefunguliwa mbinguni” (Mathayo 16:13-19).

Hapa tunamwona Mungu Baba kwa njia ya Roho Mtakatifu akimtambulisha Yesu kwa Petro, Petro akamtamka vile alivyo kama alivyotambulishwa ndani yake na Baba.  Kisha Baba kwa njia ya Yesu na kwa kinywa cha Yesu akamtambulisha kwa kusema juu ya mwamba huu, yaani Kristo Mwana wa Mungu aliye hai atalijenga kanisa lake ambalo milango au mashauri ya kuzimu hayatalishinda. Utambulisho wa Kristo kupitia Petro na Yesu Mwenyewe, Mungu Baba akiwa nyuma yao ni udhihirisho wa mamlaka na nguvu za Kristo, dhidi ya maadui.  Kazi moja kuu ya utambulisho ni kudhihirisha mamlaka na nguvu ya anayetambulishwa au anayejitambulisha. Hii ni kanuni moja kubwa tunayojifunza katika  kitabu hiki.  Mara nyingine unapokutana na majaribu makubwa usiombe maombi mengi bali mtambulishe Kristo kwa kumsema kama alivyotambulishwa na Baba hapa. Mamlaka yake na nguvu itaanza kufungua njia pasipo wewe kujua inafungukaje fungukaje.  Mara jnyingine haumtambulishi Kristo, bali unajitambulisha wewe ni nani katika Yesu, na njia inafunguka.

No comments:

Post a Comment