Thursday, February 16, 2017

MANENO YA KIVITA



Aina Tofauti za Kushindania Ushindi wako Alioshinda Yesu
Mara nyingine unaposhindana na kitu kibaya cha kishetani kwako au kwa mtu, hujui utaanzia wapi. Maandiko mara kadhaa yametumia aina ya maneno ambayo kwanza yanaonyesha unayo mamlaka, ni wewe ndio unahusika kufanya kitu katika hiyo vita na si Mungu. Pia maneno hayo yanakuonyesha mbinu au jinsi ya kufanya. Usomapo maneno haya tumia na maandiko yaliyoambatanishwa ili uelewe vizuri.

1.KANYAGA (Luka 10:19, Zaburi 44:5)
Yesu ametupa wanafunzi wake, uhalali au haki ambayo ni mamlaka kwa lugha nyingine, kukanyaga nyoka na nnge na nguvu zote za adui. Kukanyaga huku ni kuponda au kusigina. Tunakanyaga na kuponda kwa kutumia jina lake, katika Zaburi hapo juu inaonyesha kwa jina la Bwana tunakanyaga maadui. Je unataka kutodhurika? Kanyaga kwanza, kitu chochote ambacho unaona ni mashambulizi ya kishetani kishambulie wewe kwanza! Kabla, hakitakudhuru. Usikiruhuru kukushambulia kwanza.

2.TOA (Marko 16:17)
Yesu ametupa wanafunzi wake uwezo wa kumtupa Shetani au pepo nje. Neno hili kutoa pepo, tafsiri yake ni kumtupa nje kwa nguvu! Mahali popote shetani alipoingia, ndani ya mtu, ndani ya ndoa nk, unaweza mtoa au mtupa nje kwa nguvu, kwa jina la Yesu.

3. FUNGA (Mathayo 18:19-20)
Yesu ametupa uwezo wa kukataa kitu kisitokee. Kukataa huku ni kutoruhusu kitu cha kishetani kitokee. Kwa lugha nyingine ni kufunga. Kwa jina la Yesu katika vita unaweza kuzuia jambo lisitendeke la kishetani.

4. FUNGUA (Mathayo 18:19-20)
Hapohapo baada ya kuzuia ukaruhusu lingine lifanyike la kiungu. Maombi haya yanahitaji uwezo wa kuwa karibu na Roho, kujua ni kitu gani anakizuia na anakiruhusu wakati huo. Mfano unaweza kuwa unaombea kanisa na Roho akakupa ufahamu kuwa linagawanyika. Mbinguni  huwa hawaganyi  makanisa, Yesu aliomba tuwe na umoja, Hivyo haijaruhusiwa mbinguni.  Wewe hapa duniani unaweza kutoruhusu pia kama ilivyo mbinguni na kuruhusu umoja kama ilivyo mbinguni.

5. PINGA (Yakobo 4:7, 1Petro 5:8-9)
Tunauwezo wa kuzuia mwendo wa kishetani. Kumpinga Shetani. Huku ni kumwingilia wakati atendapo na kumsimamisha asiendelee. Inaweza kuwa katika mawazo, kwa mtoto nk. Tunampinga kwa Neno. Biblia inasema tumpinge tukiwa thabiti katika imani na imani inakuja kwa Neno.  Ukimzua kwa Neno anazuilika hata kama hujisikii hivyo, Yesu alipomwambia imeandikwa (Luka 4), alikuwa anampinga. Kumpinga ni kama kum-stopisha.

6. ANGUSHA (2Wakorintho  10:3-4)
Uwanja wa mapambano ni katika fikra na mawazo. Mawazo mabaya kama kukata tamaa, kujilaumu, kujihukumu bila sababu nk, unapoyaachia ni kama ukuta wa Shetani autumiao kukuzingira na kukufunga.  Mara nyingi Shetani huongea kwa mawazo, unafikiri unawaza tu kumbe adui anaongea! Maandiko yanasema kwa nguvu za Mungu tunawaangusha watesi wetu (Zaburi 44:5), na neno lina nguvu (Waebrania 4:12). Sema Neno kwenye mawazo yanayoonyea kukufunga. Utaangusha ngome katika fikra. Ukiwaza vibaya, ongea vizuri kwa kutumia Neno. Utaangusha ngome.

7. TEKA (2 Wakorintho  10:3-4)
Kuteka ni kutiisha. Katika vita vya mawazo, tiisha fikra zako zikubaliane na Neno. Tiisha zisiibiwe. Tumia Neno kuzitiisha katika amani ya Yesu. Ziambie zikatae kitu kingine chochote kinyume na Yesu. Pia unaweza kuzitiisha chini ya damu ya Yesu, kinyume na roho ya woga nk. 

8. SHINDANA (Waefeso 6:12)
Kushindana kwetu si juu ya damu na nyama. Tunashindana na viumbe visivyo onekana, ambavyo vimeshindwa. Neno hili kushindana ni sawa na kupigana mieleka. Ni kusimamia ushindi wetu na kutokubali unyang’aywe. Unapoombea mfano mkutano wa injili, unaweza kuushindania ushindi wa Kristo kwa kusema alifanya nini msalabani, mfano imeandikwa alizivua enzi na mamlaka (Wakolosai 2:15), Kisha unanena kwa lugha na kusema neno hilo tena na tena. Hapa utakuwa unarudisha nyuma utendaji wa kishetani kinyume na mkutano. Maombi kama haya yanaweza chukua muda, mpaka usikie hali ya kushangilia, kusifu au kufunguka moyoni. Unashindana kwa kusimamia ushindi ambao Yesu alishaupata. Sio mkutano tu inaweza kuwa ni kitu kipo kazini, kwa mtoto nk.

No comments:

Post a Comment