Thursday, October 22, 2015

Kumpokea Roho IV & V



                                                                                       IV

                                                        ISHARA YA KUNENA KWA LUGHA

Kunena kwa lugha siyo Roho Mtakatifu, ni ishara ya kwanza ya nje inayodhihirisha mtu amempokea Roho Mtakatifu ndani.

Roho anaweza kumjaa mtu bila kunena kwa lugha! Ila ishara ya nje inayoonyesha amejaa ni kunena kwa lugha. Watu wengi hujazwa Roho ila ishara ya kunena huwa haijaonekana hii haina maana hawajajazwa bali ishara haijaonekana. Kuna maandiko kadhaa yanaoonyesha kujazwa Roho au kumpokea Roho kunanendana na ishara ya kunena kwa lugha:

Matendo 2:1-4 “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. (2) Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi (3) Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. (4) Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka. ”

Matendo 19:6 “Na Paulo, alipokwisha kuweka mikono yake juu yao, Roho Mtakatifu akaja juu yao; wakaanza kunena kwa lugha, na kutabiri.”

Matendo 10:44-46, “Petro alipokuwa akisema maneno hayo Roho Mtakatifu akawashuki wote waliolisikia lile neno. (45) Na wale waliotahiriwa, walioamini, wakashangaa, watu wote waliokuja pamoja na Petro, kwa sababu Mataifa nao wamemwagiwa kipawa cha Roho Mtakatifu. (46) Kwa maana waliwasikia wakisema kwa lugha, na kumwadhimisha Mungu. Ndipo Petro akajibu, (47) Ni nani awezaye kuzuia maji, hawa wasibatizwe, watu waliopokea Roho Mtakatifu vile vile kama sisi?

Andiko lililopita linaonyesha Waliotahiriwa walifahamu watu wamejazwa Roho maana waliwasikia wakinena kwa lugha.  Kulikuwa na kiashirio kwamba wamepokea Roho na cho ni kunena kwa lugha.

Kitabu hiki kidogo kimekuja ili kukusaidia kuweza kujazwa Roho Mtakatifu na kunena kwa lugha. Kimekuja ili usikie kuhusu kumpokea Roho upate imani  na baadaye ujazwe Roho na kunena kwa lugha.  Nitataja mambo kadhaa hapa ambayo usiyasahau ikiwa unataka kupokea kipawa cha Roho Mtakatifu na kunena kwa lugha.

        I.            Yesu Ameomba Roho Mtakatifu kwa Baba kwa ajili yako (Yohana 14:16)

     II.            Yesu Amempokea Roho Mtakatifu toka kwa Baba kwa ajili yako (Matendo 2:33)

   III.            Yesu Amekupa Roho Mtakatifu toka kwa Baba (Matendo 2:33)

  IV.            Mpokee Roho Mtakatifu kwa imani, uliyosikia (Wagalatia 3:2)

Ikiwa unataka kujazwa Roho mambo haya manne yasitoke ndani yako yatafakari na kuyasema, tumia maandiko tuliyoyataja hapo nyuma.

V

MPOKEE ROHO MTAKATIFU

Katika kipengele hiki cha mwisho, Mungu anakwenda kukusaidia kumpokea Roho na kuanza kunena kwa lugha. Mara nyingi nimeona watu wakimpokea Roho na kunena kwa lugha wakiwa katika hali ya imani ya kuyafanya haya. Ingawa siyo sheria kwamba, kwa hatua hizi ndiyo utajazwa Roho.

I. Mwamini Yesu.

Mwamini Yesu kwa kuoshwa kwa damu yake. Wakati wa maombezi au maombi binafsi ya ujazo wa Roho, lazima kumwamini Yesu na kuzaliwa mara ya pili, kuwa na kisima. Hata kama umeokoka ni vema kukiri wokovu na imani yako kwa Yesu ili kuweza kumpokea Roho wake. Anasema, Aniaminiye mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake (Yohana 7:37-39). Kumwamini Yesu ni msingi wa kumpata Roho (Mito). Roho anafanya kazi na damu. Kipengele hiki ni cha kuhusisha damu ioshayo kabla ya Roho Mtakatifu.

II. Ona Kiu

Yesu alisema mtu akisikia kiu aende kwake anywe (Yohana 7:37). Roho Mtakatifu unampokea kwa shauku kuu! Yaana kiu. Nakumbuka miaka ya themanini alikuja mhubiri kutoka Kenya aitwaye George Gichana. Alikuwa akihubiri viwanja vya Jangwani Dar es Salaam. Alipohubiri alikuwa akinena kwa lugha sana! Mimi nilitamani sana nijazwe na ninene kwa lugha kama yeye. Siku moja baaada ya mkutano nilijisemesha moyoni “leo ni leo lazima ninene kwa lugha”. Nilitoka katika mkutano nikiwa na hamu kuu ya kujazwa Roho na kunena kwa lugha. Nilipofika nyumbani, moja kwa moja nilienda kibalazani, nikapiga magoti na kwa shauku kuu nilianza kusema, “Haleluya, haleluya, haleluya,…” Ghafla nikaanza kunena kwa lugha!

Yesu alisema anayeona kiu aende kwake anywe maji ya Roho, ni kweli niliona kiu nikaenda kwa Yesu akaninywesha maji ya Roho. Hapa udhihirisho wa karama za Roho pia unaendana na kuzitamani, kuona kiu.

III. Simama Mbele za Yesu

Unapotaka kumpokea Roho usitazame mtu, ikiwa ni mhubiri au mchungaji ! Yesu ndiye anayebatiza kwa Roho. Toa macho yako kwa watu wanaoomba au kukuombea, mtazame Yesu kwa imani kwamba yupo mbele yako anakujaza Roho. Luka 3:16 imeandikwa, “Yohana alijibu akawaambia wote, Kweli mimi nawabatiza kwa maji; lakini yuaja mtu mwenye nguvu kuliko mimi, ambaye mimi sistahili kuilegeza gidamu ya viatu vyake; yeye atawabatiza kwa Roho Mtakatifu na kwa moto”. Simama mbele za Yesu huku umefumba macho kwa imani na kusema, “Yesu unanijaza Roho unanibatiza kwa Roho kama maandiko yasemavyo, katika jina la Yesu lolote nilisemalo katika jina lako unalifanya. Yohana 14:14.  Hatua hii ya imani ni nyeti kabla ya udhihirisho kutokea. Endelea kusema na kung’ang’ana. Sema “Yesu ni wewe unamjaza Roho”.

IV. Hisia za Kiroho

Wakati wa kujazwa unaweza kuanza kujisikia furaha, au kulia au hofu ya Mungu. Mara nyingine unaweza kuanza kujisikia mwepesi. Unajua ujazo wa Roho mara nyingine unaendana na hisia au matukio. Mfano matendo ya mitume 2, kulitokea uvumi wa upepo, ndimi za moto, kabla ya kuanza kunena! Wakati unaongea na Yesu unaweza kuanza kupata hisia na mabadiliko.

V. Tendo la Imani

Chukua hatua ya imani ya kusema na kuacha mdomo wazi. Maandiko yanasema, “Mimi ndimi BWANA, Mungu wako, Niliyekupandisha toka nchi ya Misri; Fumbua kinywa chako nami nitakijaza” (Zaburi 81:10). Unaposema mbele za Yesu mfano “Yesu unanijaza, Yesu ni mwema …..” Sema huku unaachia sekunde chache mdomo wako ukiwa wazi. Ufanyapo hivi na kusikia unataka kulia, kufurahi nk, basi ni dalili tayari Roho yupo na wakati wowote utanena  kwa lugha!

VI. Chemchemi Zatoka Ndani

Maandiko yanaposema amwaminiye Yesu,  Ndani yake zitatoka chemchemi (Roho).   Katika  maandiko maana halisi isemayo ndani yake ni ndani ya `tumbo la kiroho’. Roho anatokea ndani, anajaa tokea ndani na anadhihirika nje kwa kunena kwa lugha.

Zipitie hatua hizi ukiwa peke yako utashangaa, utanena kwa lugha, wengi wamenena kwa kujifunza somo hili na kulifanyia kazi.

Baada ya kujazwa Roho na kunena kwa lugha, endelea kunena kwa lugha na kujijenga kwa kunena kwa lugha.  Soma kitabu kiitwacho Kushirikiana na Roho Mtakatifu, ili kuzidi kumwelewa Roho.

Karibu!

No comments:

Post a Comment