Monday, October 12, 2015

Kumpokea Roho II & III

SOMO LA NYUMA KABLA YA USHUHUDA WA DADA NYISAKI, TULIANZA SOMO LA KUMPOKEA ROHO MTAKATIFU. LEO TUNAENDELEA SEHEMU YA PILI NA YA TATU.



II
KABLA YA KUJA ROHO MTAKATIFU
Labda, turudi nyuma kidogo tuangalie kwa kifupi kabla ya kuja Roho Mtakatifu duniani mambo gani ilikuwa lazima yatangulie.
1. Kuja kwa Yesu
Kabla ya Roho Mtakatifu kuja, ilikuwa ni lazima Yesu aje kwanza, ni kama ilivyokuwa kwa Yohana Mbatizaji, kabla ya kuja Yesu ilikuwa lazima aje Yohana mbatizaji, Maandiko yanasema, “Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. (38) Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake (39)  neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana roho alikuwa hajaja, kwa sababu  Yesu alikuwa hajatukuzwa.” (Yohana 7:38-39). Andiko hili linaonyesha ni mpaka Yesu aje, Afe, Afufuke, na atukuzwe ndipo Roho anatokea.
2. Kuondoka kwa Yesu
Yesu alisema, “Lakini mimi nawaambia iliyo kweli; yawafaa ninyi mimi niondoke, kwa maana mimi nisipoondoka, huyo Msaidizi hatakuja kwenu; bali mimi nikienda zangu, nitampeleka kwenu.“ (Yohana 16:7) Kuondoka kwa Yesu duniani ni kuja kwa Roho Mtakatifu duniani. Huu ni uhakika wa kumpokea. Unaweza kumpokea Roho kwa kuwa Yesu ameshaondoka!
3. Kuomba kwa Yesu
Yesu anasikiwa na Mungu siku zote! Alisema “…… Baba, nakushukuru kwa kuwa umenisikia. (42) Nami nalijua ya kuwa wewe wanisikia siku zote; lakini kwa ajili ya mkutano huu wanaohudhuria nalisema haya, ili wapate kusadiki  kwamba ndiwe uliyenituma” (Yohana 11:41-42). Kati ya maombi ya Yesu ambayo yameshajibiwa kwetu na Baba aliyoomba Yesu yanaonekana katika maandiko haya “Nami nitamwomba Baba, naye atawapa Msaidizi mwingine, ili akae nanyi hata milele” (Yohana 14:16). Yesu anasema, naye atamwomba Baba na Baba atatupa Msaidizi mwingine yaani Roho Mtakatifu. Inaonekana katika maandiko haya ni kitu kirahisi! Alitupa lini? Au maombi hayo yalijibiwa lini? Yalijibiwa Roho aliposhuka wakati wa Pentekoste, Matendo 2:1-3. Sasa imebaki wewe kupokea tu, Yesu ameshajibiwa maombi yake, aliomba Roho akapewa sasa unampokea! Kirahisi bila kuhangaika.
4. Kuketi kwa Yesu
Yesu alipoomba kwa Baba tupewe Roho Mtakatifu Baba alijibu. Alimpa Yesu Roho Mtakatifu na Yesu akatupa sisi. Inaonekana Baba alimpa Yesu Roho kwa ajili yetu baada ya Yesu kufufuka na kuketi mkono wa kuume wa Mungu.
Yesu aliposema atamwomba Baba Msaidizi mwingine inawezekana kabisa alikuwa na maana ya kumwomba akiwa mkono wa kuume wa Mungu maana maandiko yanaonyesha hapo ndipo alipompokelea na kutupa sisi, “Basi yeye, akiisha kupandishwa hata mkono wa kuume wa Mungu, na kupokea kwa Baba ile ahadi ya Roho Mtakatifu amekimwaga kitu hiki mnachokiona sasa na kukisikia“ (Matendo 2:33).
Mpaka hapa fahamu ya kuwa Yesu amemwomba Baba Roho Mtakatifu. Baba akampa mkono wa kuume na yeye Yesu akatupa sisi. Wajibu wetu sasa ni kumpokea! Siyo kumbembeleza Mungu atupe! .


III
SURA ZA ROHO NDANI YA MWAMINI
Roho Mtakatifu kwa mwamini anaonekana kwa sura mbili. Sura ya kwana ni `Chemichemi’ na sura ya pili ni ‘Mito’.
JUMAPILI YA KUFUFUKA (Chemchemi)
Biblia inasema “Yesu akajibu, akawaambia, Kila anywaye maji haya ataona kiu tena; (14) Walakini ye yote atakayekunywa maji yale nitakayompa mimi hataona kiu milele; bali yale maji nitakayompa yatakuwa ndani yake chemchemi ya maji, yakibubujika uzima wa milele.” (Yohana 4:13-14). Chemchemi inayotajwa hapa tafsiri yake rahisi ni kisima. Kisima ni cha mtu au watu fulani. Kisima kinaweza kuwa na ubinafsi. Unaweza kukifunga au kuruhusu watoto wako tu watumie nk. Roho Mtakatifu anaweza kuonekana kama kisima ndani yetu, yeye ni mmoja atuwezeshaye kuwa na mahusianao ya moja kwa moja na Mungu sisi kama watu binafsi mmoja mmoja. Yeye Roho Mtakatifu ndani yetu ni chemchemi za maji zibubujikiazo uzima wa milele.
Ukisoma maandiko Yohana 20:19-22, imeandikwa, “Ikawa jioni, siku ile ya kwanza ya juma, pale walipokuwapo wanafunzi, milango imefungwa kwa hofu ya Wayahudi; akaja Yesu, akasimama katikati, akawaambia, Amani iwe kwenu. (20) Naye akiisha kusema hayo, akawaonyesha mikono yake na ubavu wake. Basi wale wanafunzi wakafurahi walipomwona Bwana (21) Basi Yesu akawaambia tena, Amani iwe kwenu; kama Baba alivyonituma mimi, mimi nami nawapeleka ninyi. (22) Naye akiisha kusema hayo, akawavuvia, akawaambia, Pokeeni Roho Mtakatifu.
Baada ya Yesu kufufuka na kukutana na wanafunzi, Biblia inasema hapa, akawavuvia akawaambia wapokee Roho Mtakatifu. Hii ilikuwa ni siku ya kwanza ya juma, Jumapili ya ufufuo. Kwa kuvuviwa Roho Mtakatifu wanafunzi walikuwa wakizaliwa kwa Roho Mtakatifu. Kufufuka kwa Yesu ndiyo mlango wa watu kuzaliwa  mara ya pili kwa Roho Mtakatifu. Yesu alipowavuvuia Roho alikuwa anawazaa mara ya pili. Tayari walikuwa wanamwamini na kumkiri Yesu kama Bwana kabla hajafa, Lakini walibadilishwa na kuzaliwa mara ya pili baada ya Yesu kufufuka.  Ili mtu azaliwe mara ya pili ni lazima amkiri Yesu kama Bwana na aamini Mungu alimfufua katika wafu, Wanafunzi tayari walikuwa wanamkiri Yesu kuwa ni Bwana ila bado alikuwa hajafufuka, hivyo wasingeweza kuokoka/kuzaliwa mara ya pili kabla hajafufuka, Hivyo baada ya kufufuka waliweza kuamini kuwa Mungu alimfufua katika wafu, Wakavuviwa Roho Mtakatifu, hapa walikuwa wanaokoka wanazaliwa kwa Roho, “Kwasababu ukimkiri Yesu kwa kinywa chako ya kuwa ni Bwana, na kuamini moyoni mwako ya kuwa Mungu alimfufua katika wafu, utaokoka” (Warumi 10:9).
Sehemu hii ya kuvuviwa Roho, Roho Mtakatifu alikuwa ni kama KISIMA au CHEMCHEMI. Hatua hii ni hatua ya mahusiano ya mtu binafsi na Mungu, kuzaliwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, “Yesu akajibu, akamwambia,Amin, amin nakuambia, Mtu asipozaliwa mara ya pili, hawezi kuuona ufalme wa Mungu. (6) Kilichozaliwa kwa mwili ni mwili; na kilichozaliwa kwa Roho ni roho ” (Yohana 3:3,6).
Tunaposema kila mtu aliyeokoka ana Roho Mtakatifu tunamaana hii, “Kila mtu aliyeokoka ana Roho kama Kisima amenyweshwa Roho Mtakatifu anaye Roho wa Kristo.” Kuna watu husema kila mtu aliyeokoka ana Roho wa Kristo, ni kweli kwa maana ya kila aliyeokoka amezaliwa na Roho wa Kristo na ni mali ya Kristo,”Lakini ikiwa Roho wa Mungu anakaa ndani yenu, ninyi hamwufuati mwili; bali mwaifuata roho. Lakini mtu awaye yote asipokuwa na Roho wa Kristo, huyo si wake.” (Warumi 8:9).
Mtu huyu aliyezaliwa mara ya pili ni kweli ana Roho Mtakatifu, lakini ni kwa ngazi ya kisima anachotumia yeye na watu wachache. Anatakiwa asasifi toka Jumapili ya kufufuka Yesu yenye kisima/kuzaliwa na Roho, mpaka afike Jumapili ya Pentekoste, yaani siku ya kwanza ya juma aliyoshuka Roho Mtakatifu na kuwajaa mitume.
JUMAPILI YA PENTEKOSTE (Mito)
Jumapili hii ni Jumapili ya MITO na sio KISIMA. Hata hivyo huwezi kuingia Jumapili hii ya Pentekoste kabla ya Jumapili ya kufufuka. Ni lazima kuzaliwa kwa Roho kwanza na kupata kisima kabla ya kujazwa Roho na kupata mito. Biblia inasema, “(37) Hata siku ya mwisho, siku ile kubwa ya sikukuu, Yesu akasimama, akapaza sauti yake akisema, Mtu akiona kiu, na aje kwangu anywe. (38) Aniaminiye mimi, kama vile maandiko yalivyonena, mito ya maji yaliyo hai itatoka ndani yake. (39) Na neno hilo alilisema katika habari ya Roho, ambaye wale wamwaminio watampokea baadaye; kwa maana Roho alikuwa hajaja, kwa sababu Yesu alikuwa hajatukuzwa.” (Yohana 7:37-39). Maandiko haya yalidhihirika wakati wa Pentekoste, “Hata ilipotimia siku ya Pentekoste walikuwako wote mahali pamoja. (2) Kukaja ghafula toka mbinguni uvumi kama uvumi wa upepo wa nguvu ukienda kasi, ukaijaza nyumba yote waliyokuwa wameketi (3) Kukawatokea ndimi zilizogawanyikana, kama ndimi za moto uliowakalia kila mmoja wao. (4) Wote wakajazwa Roho Mtakatifu, wakaanza kusema kwa lugha nyingine, kama Roho alivyowajalia kutamka.   ” (Matendo 2:1-4).
Mto una nguvu kuliko kisima. Mto hauna ubinafsi, hamna mtu anayeweza kuufungia mto kama tufanyavyo kwa visima. Mto Nile ni wa Uganda, Sudani, Misri nk. Wote hawa wana haki nao. Ndivyo ulivyo ujazo wa Roho Mtakatifu, unaathiri eneo kubwa zaidi ya kuokoka na kuzaliwa mara ya pili. Unakuathiri wewe, jinari zako na dunia kwa ujumla. Aliyejazwa Roho anaweza kufika Marekani akiombea mtu kwa lugha akiwa Tanzania! Hamna mipaka.
Tunajazwa Roho Mtakatifu ili tufikie mbali katika Yesu Kristo. Tuwe na karama, tumdhihirishe Yesu kuwa yu hai amefufuka, Tuidhihirishe kazi yote ya msalaba kwa Roho Mtakatifu.
Kumpokea Roho Mtakatifu ni kujazwa Roho Mtakatifu. Tunaposema kumpokea Roho katika kitabu hiki hatuna maana ya kuvuviwa Roho, yaani kuzaliwa kwa Roho na kuwa ‘kisima’. Tunamaana ya kuzamishwa ndani ya Roho na kuwa na `Mito’.
Katika Kanisa la kwanza ilikuwa ni kawaida kumpokea Roho Mtakatifu, baada ya kumwamini Yesu. Ilikuwa ni kawaida kupokea mito baada ya kisima, “… akawauliza, Je! Mlimpokea Roho Mtakatifu mlipoamini? Wakamjibu, La, hata kusikia kwamba kuna Roho Mtakatifu “ (Matendo 19:2).
Andiko hili linatuonyesha vitu kadhaa. Kwanza baada ya kuamini iliwapasa wampokee Roho. Pili iliwapasa wasikie kuhusu Roho ili wampokee. Kwa nini wasikie? Ni ili wawe na imani ya kumpokea, Maana imani huja kwa kusikia, “Basi imani, chanzo chake ni kusikia; na kusikia huja kwa neno la Kristo” (Warumi 10:17). Sababu moja kuu ya watu kutompokea Roho Mtakatifu ni kutosikia kuhusu Roho, hatimaye kutokuwa na imani ya kumpokea Roho. Roho anapokelewa kwa imani, “Nataka kujifunza neno hili moja kwenu. Je! Mlipokea Roho kwa matendo ya sheria, au kwa kusikia kunakotokana na imani?  ” (Wagalatia 3:2)












No comments:

Post a Comment