Saturday, November 7, 2015

Imani na Kuhesabiwa Haki



Muda si mrefu kutoka sasa, nitatoa kitabu hiki cha Imani na Kuhesabiwa haki. Usikose kukisoma. Nimeonyesha utangulizi wake na sura ya kwanza hapa.
 
UTANGULIZI
Leo tarehe 02/07/2015, nilipokuwa naomba kwa kunena kwa lugha asubuhi, niliona maandishi moyoni yaliyokuja ghafla “Imani na kuhesabiwa haki”. Hapo hapo nikajua hilo ni somo ambalo lapaswa liwe kitabu. Wakati naendelea kunena kwa lugha likaja somo lingine liitwalo “Dawa ya Imani”. Haya ni masomo mawili yaliyokuja wakati mmoja! Ingawa kwa sasa tutajifunza somo hili la imani na kuhesabiwa haki.
Maandiko yanonyesha tumehesabiwa haki kwa Imani ya Yesu Kristo. Msingi wa haki yetu mbele za Mungu ni Imani katika Yesu Kristo. Hii ndiyo tofauti kubwa ya Agano la Kale na Agano Jipya. Agano la Kale lilikuja kwa ajili ya Wayahudi na lilikua la SHERIA. Mtu akitenda SHERIA, basi angehesabiwa haki. Agano Jipya ni kwa ajili ya dunia nzima na sio kwa Wayahudi tu, katika Agano hili mtu anahesabiwa haki kwa IMANI.  Maandiko yanasema, “(28)Basi, twaona ya kuwa mwanadamu huhesabiwa haki kwa Imani pasipo matendo ya sheria. (29)Au je! Mungu ni Mungu wa Wayahudi tu? Siye Mungu wa Mataifa pia? Naam, ni Mungu wa Mataifa pia; (30)kama kwa kweli Mungu ni mmoja, atakayewahesabia haki wale waliotahiriwa katika Imani, nao wale wasiotahiriwa atawahesabia haki kwa njia ya Imani iyo hiyo.”(Warumi 3:28-30). Katika  Yesu, baada ya kumpa maisha yetu, msingi wetu wa ushirika na yeye wenye nguvu kwa mtu aliyeokoka ni kufahamu kuhesabiwa haki kwa Imani maana yake nini.
Usiache kusoma na kuelewa somo hili la kuhesabiwa haiki kwa Imani. Ufahamu kuhusu kuhesabiwa haki ni kama nguzo ya katikati ishikayo nyumba yote. Wokovu wako wote unaweza kushikwa na kutotikisika kwa ufahamu wa kuhesabiwa haki kwa Imani.
Katika Sheria iliwapasa binadamu (Wayahudi) kufanya kitu kwa kuitii Sheria ili wahesabiwe haki. Katika Agano Jipya, Yesu amefanywa kwetu jambo fulani ili sisi tuhesabiwe haki tunapomwamini, sasa hatufanyi sisi amefanyika Yesu, “Bali kwa yeye ninyi mmepata kuwa katika Kristo Yesu, aliyefanywa kwetu hekima itokayo kwa Mungu, na haki, na utakatifu, na ukombozi” (1Wakorintho 1:30).



I
MAANA YA KUHESABIWA HAKI
Maandiko yanasema, “kwa sababu wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu; (Warumi 3:23). Binadamu wote wametenda dhambi mbele za Sheria ya Mungu. Wanadamu ni watenda dhambi kwa sababu kuu moja: Ni watenda dhambi kwa sababu wamezaliwa katika dhambi. Dhambi ipi?Ni dhambi ya Adamu. Adamu alipokosea watu wote waliokuwa ndani yake katika mbegu (wewe na mimi), tulikosea. Wote tulitenda dhambi, Adamu alipotenda dhambi. Maandiko yanasema, “Kwa sababu kama kwa kuasi kwake mtu mmoja watu wengi waliingizwa katika hali ya wenye dhambi, kadhalika kwa kutii kwake mmoja watu wengi wameingizwa katika hali ya wenye haki.” (Warumi 5:19). Mtu ni mtenda dhambi siyo kwa sababu anatenda dhambi tu, la! Ni mtenda dhambi kwa sababu amezaliwa na dhambi ametoka kwa Adamu mwenye dhambi.
Dhambi watu wanazotenda kama kuiba, kuua, kuzini, kusema uongo nk, Siyo msingi unaowafanya wawe wenye dhambi, ni wenye dhambi kwa kuwa wameazaliwa katika dhambi, wamezaliwa toka kwa Adamu mwenye dhambi. Hizo dhambi wanazotenda ni matunda tu yanayoonekana, mzizi wake hauonekani, huu ndiyo tatizo, unaitwa dhambi ya Adamu ndani yao. Adamu alipotenda dhambi wote tulikuwa watenda dhambi na kuzaa matunda ya dhambi.
Dhambi ya Adamu
Tunaposema dhambi ya Adamu tunamaanisha nini? Kitabu cha Mwanzo 2:16 – 17 na Mwanzo 3:6 kinaonyesha Adamu aliasi alichosema Mungu hii ilikuwa ni dhambi iliyopandwa ndani yake na kuwafikia watu wote. Watu wote waliasi alichosema Mungu, waliasi kwa kuwa wote walikuwa ndani ya Adamu. .
Adamu na Eva, Waliasi kwa ushawishi wa nyoka (Mwanzo 3:1) au Shetani (Ufunuo 12:9). Wangeweza kupingana na uasi huo au ushawishi huo kwa kutumia Neno la Mungu  alilosema nao, “BWANA Mungu akamwagiza huyo mtu, akisema, matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16-17). Lakini hawakutumia maneno haya kumpinga Shetani, bali walikubali kudanganywa. Hii inatufundisha nini? Dhambi huwezi kuipinga bila Neno la Mungu. Ushawishi wa kishetani huwezi kushindana nao bila Neno. Mungu aliposema nao na kuwaambia matunda ya kila mti waweza kula ila mti wa ujuzi wa mema na mabaya wasile, aliwapa Neno ambalo wangeweza kulitumia kupinga ushawishi wa kishetani na kupinga dhambi. Pengine ndiyo maana Daudi alisema ameliweka Neno moyoni mwake asije kumtenda dhambi (Zaburi 119:11).
Jinsi Adamu na Eva walivyoshindwa kutumia Neno alilowapa Mungu ili kupinga ushawishi wa Shetani, ndivyo Yesu alivyoshinda kwa kutumia Neno na kupinga ushawishi wa nyoka /Shetani (M
athayo 4:1-11). Kwa hiyo twaweza kusema dhambi ya Adamu ni uasi wa Neno la Mungu alioufanya Adamu. Huu ulipelekea kumuua kiroho na kuingiza kifo duniani. Dhambi hii ipo kwa wanadamu wote, imeingia kwao kwa mtu aitwaye Adamu. Inaondoka kwa ‘mtu’ aitwaye Yesu Kristo (Adamu wa pili).
Kuhesabiwa Haki
Kuhesabiwa haki ni neno la kisheria, ambalo linaonyesha hali ya kuonekana mbele ya sheria kwamba mtu hana hatia. Kuhesabiwa haki ni kumwachilia mtu toka katika hatia. Kwa mfano mtu amekosea anatakiwa auawe kwa kuwa ameua. Halafu akatamkwa kwamba hana hatia hatakiwi kufa tena! Kitendo cha namna hii kikitokea, basi amehesabiwa haki. Neno la Kiyunani dakaioo, limebeba maana hizi ambalo tafsiri yake ni: kufutia na kuonyesha hali ya kutokuwa na hatia, kuweka huru mbali na hatia, kufanya mtu asiwe amekosea wala asiwe na hatia.
Katika Sheria ya Mungu mtu hawezi kuachiliwa hivi na kutamkwa hivi bure! Lazima tamshi hilo lilipiwe. Maandiko yanasema mshahara wa dhambi ni mauti (Warumi 6:23). Haiwezekani mtu akatamkwa hana hatia bila dhambi zake kulipiwa na mauti. Ikiwa Mungu angetutamka kuwa hatuna hatia wakati tumefanya dhambi ya Adamu istahiliyo kufa, basi asingekuwa mwenye haki katika sheria yake.
Hivyo ilikuwa ni lazima, ili Mungu aweze kutuhesabia haki na yeye aendelee kuwa Mwenye haki, dhambi zetu zilipiwe kwanza kwa kifo. Kifo hiki alikufa Yesu asiyekuwa na dhambi. Njia ya zamani ya kuingia mbinguni ilikuwa matendo ya Sheria, yaani kuitenda Sheria yote ya Musa, hii ilishindikana. Yesu ndiye njia mpya ya kuingia, njia hii imewezekana, “Yesu akamwambia, Mimi ndimi njia, na kweli na uzima; mtu haji kwa Baba, ila kwa njia ya mimi.” (Yohana 14:6), Pia soma Waebrania 10:19-20.
Kuna tajiri mmoja katika maandiko anaonekana alizishika amri na kuzitegemea ili amwone Mungu hii ilishindikana. Yesu akaonyesha ilimpasa auze vyote, asitegemee chochote kisha amfuate Yesu. Tajiri alishindwa, hapo hapo akaonekana alipenda mali kuliko Mungu. Akavunja amri ya kwanza wakati alisema amezishika zote! (Soma Mathayo 19:26). Hakutakiwa kutegema chochote bali Yesu tu, ili amwone Mungu. Yote aliyoyafanya kwa kushika Sheria hayakumsaidia. Kuhesabiwa haki kwa Imani maana yake  ni Yesu tu anatosha ili Mungu akukubali na usiwe na hatia mbele zake, na siyo kitu kingine chochote. Ni kwa Imani katika Yesu tu!
Haki ni Kipawa
Kuhesabiwa haki ni kuokoka. Fananisha maandiko haya mawili utagundua kwamba kuhesabiwa haki ni kuokoka. Matendo 16:31 na Matendo 13:38. Katika andiko la kwanza (Matendo 16:31), imeandikwa mwamimini Yesu Kristo nawe utaokoka na nyumba yako. Kumwamini Yesu kunaleta kuokolewa. Andiko la pili (Matendo 13:38-39), linasema mtu akimwamini Yesu atahesabiwa haki. Kwa hiyo kumwamini Yesu huleta wokovu au kwa lugha nyingine, wokovu huu unaitwa kuhesabiwa haki. Kwa kuunganisha maandiko haya na kuyatafsiri tunajifunza kwamba kuokoka ni kuhesabiwa haki kwa njia ya kumwamini Yesu.  Kuokoka ni zawadi ni kipawa, kuhesabiwa haki pia ni zawadi ni kipawa, Warumi 5:17, inaita haki ni kipawa. Haki tunayopewa katika Kristo tunapewa kama zawadi iliyotolewa kwa neema ya Kristo kufanyika dhambi, ili sisi tuwe haki ya Mungu katika yeye. Sisi hatujahesabiwa haki tu, tumekuwa haki ya Mungu, baada ya Kristo kuwa dhambi zetu.











No comments:

Post a Comment