Neno ni Mbegu
Haki Zote Zimehifadhiwa
©B
Mwakatundu 20Tabia za Mbegu
Mbegu inazo sifa na tabia kadhaa:
A. Mbegu Inabeba Sura na Sifa ya Mahali Ilipotoka
Katika biblia maandiko yanaonyesha kwamba mbegu
inabeba sura au inafanana na mahali inapotoka, “Nchi ikatoa majani, mche utoao mbegu kwa jinsi yake, na mti uzaao matunda ambao mbegu zake zimo ndani
yake kwa jinsi yake” (Mwanzo 1:12).
Andiko hili linatuonyesha kwamba mti hutoa mbegu ambazo zinafanana
nao. Ndani ya mbegu kuna sura ya mti au
mmea ilipotoka.
Andiko lingine linasema, “Adamu akaishi miaka mia na thelathini akamzaa mwana kwa sura yake kwa mfano wake akamwita jina lake Sethi.”
(Mwanzo 5:3). Binadamu anayo mbegu ndani
yake. Mbegu hiyo inabeba sifa na sura
yake. Ndio maana Adamu alimzaa mtoto
aitwaye Sethi mwenye sura na mfano wake.
Sethi alibeba sura ya mahali alipotoka, alitoka kwa Adamu.
B. Mbegu Inatoa Ongezeko Linalofanana Nayo
Yesu alitoa mfano wa mpanzi unaoonyesha tabia ya
pili ya mbegu. Alisema, “Tanzama mpanzi alitoka kwenda kupanda…Hata
alipokuwa akipanda…nyingine zikaanguka penye udongo mzuri, zikazaa, moja mia,
moja sitini, moja thelathini.” ( Mathayo 13:3,4,8). Katika andiko hili tunaona kwamba mbegu
zilipopandwa ziliongezeka, kipimo cha mia, sitini na thelathini. Mbegu huongezeka kwa jinsi yake.
C. Ili Mbegu Iote Inapaswa Ipandwe
Kuhusu mbegu kupandwa maandiko yanasema, “Isaka akapanda mbegu katika nchi (au
ardhi) ile, akapata mwaka ule vipimo mia
kwa kimoja…” (Mwanzo 26:12). Kama
Isaka asingepanda, asingeifukia mbegu katika ardhi, basi asingepata vipimo mia
kwa kimoja.
D. Mbegu Ipandwapo Haionekani Ingawa Inatenda Kazi
Mtu apandapo mbegu haoni matokeo haraka, kwa juu
inaonekana hamna kitu. Ndani ya udongo
mbegu hiyo huanza kufanya kazi ingawa mtu hawezi kuiona kwa kuwa
imefukiwa. Maandiko yanasema, “Akasema ufalme wa Mungu , mfano wake ni kama mtu aliyemwaga mbegu juu ya nchi; akawa akilala na
kuondoka usiku na mchana nayo mbegu ikamea na kukua asivyojua yeye”(Marko
4:26-27). Mpanzi hapa hakujua mbegu
zimeotaje otaje, lakini ziliota.
E. Ili Mbegu Iote Inapaswa Imwagiliwe
Maandiko yanaonyesha kwamba kabla ya Mungu
kunyeshea nchi kwa maji Mbegu haikuota, “Siku
ile BWANA Mungu alipoziumba mbingu na nchi hapakuwa na mche wa kondeni bado,
wala mboga ya kondeni haijachipuka bado kwa maana BWANA Mungu hajainyeshea nchi
mvua…ukungu ukapanda katika nchi, ukatia maji juu ya uso wote wa ardhi.”
(Mwanzo 2:4-6) Kabla ya Mungu kumwagia
nchi maji mbegu haikuchipuka. Bila shaka
nchi ilipotoa mbegu na mche kwa jinsi yake (Mwanzo 1:12), ilitokea baada ya
Mungu kuinyeshea maji.
II
Yesu Alisema Neno ni Mbegu
Yesu alipokuwa akiwaelezea wanafunzi wake maana ya
mfano wa mpanzi alisema, “Na huo mfano,
maana yake ni hii; Mbegu ni neno la Mungu.” (Luka 8:11). Kwa kuwa mbegu ni Neno la Mungu linafana na
tabia za mbegu nyingine.
A.Neno Lina Sifa na Sura ya Mahali Lilipotoka
Yesu alilifananisha Neno la Mungu na mbegu, hii
inamaana kwamba Neno lina sifa na sura ya mahali lilipotoka. Je, limetoka wapi? Limetoka kwa Mungu. Lina sifa na sura ya Mungu kama
vile mbegu ilivyo na sifa na sura ya mahali ilipotoka.
Tukitaka kujua mbegu ya Mungu, yaani Neno lake lina
sura gani ni lazima tujue mahali ilipotoka pakoje, yaani Mungu yukoje. Tabia au sura ya Mungu ipo ndani ya
Neno. Hebu tuangalie katika jeduali
lifuatalo.
Mungu Alivyo
|
Neno Lilivyo
|
Yote Yawezekana kwa Mungu (Yeremia 32:27)
|
Yote yawezekana kwa Neno
(Luka 1:37) |
Mungu ni Nuru (1Yohana 1:5)
|
Neno ni Nuru (Zaburi 119:105)
|
Mungu Ana Uzima (Yohana 1:4)
|
Neno Lina Uzima (Yohana 6:63)
|
Mungu Anajua Yote(Waebrania 4:12-13)
|
Neno Linajua Yote (Waebrania 4:12-13)
|
Mungu ni wa Milele (Ufunuo 1:8)
|
Neno ni la Milele (1Petro 1:23)
|
Mungu ni Mponyaji ni afya yetu(Kutoka 15:26)
|
Neno linaponya, neno ni Afya yetu (Mithali 4:20-22)
|
Tabia yoyote ya Mungu unayoifahamu imo ndani ya
Neno lake, yeye na Neno ni umoja.
B. Neno kama Mbegu Linatoa Ongezeko Linalofanana Nayo
Neno linazalisha tabia za ki-Mungu mahali
linapopandwa. Linaleta ongezezeko la
tabia na sifa za Mungu alivyo. Maandiko
yanasema, “kwa kuwa mmezaliwa mara ya
pili; si kwa mbegu iharibikayo, bali kwa ile isiyoharibika; kwa neno la Mungu
lenye uzima, lidumulo hata milele.” (1Petro 1:23). Kama
tulivyokwisha kuona Neno la Mungu ni mbegu limefanana na pale lilipotoka,
limefanana na Mungu.
Mtu anapozaliwa mara ya pili kwa mbegu ya Neno la
Mungu, sura,tabia na sifa za Mungu
zinapandikizwa ndani yake kwa mbegu hiyo.
Roho iliyozaliwa mara ya pili inabeba sura ya Neno, hii ni sura ya
Mungu! Inabeba Uzima, Utakatifu, Hekima,
ufahamu na mengineyo yaliyo ndani ya Mungu.
Kwa njia ya Neno la Mungu au mbegu yake kuwa ndani
ya watu wengi, na watu hao kuzaliwa mara ya pili, sura ya Mungu na tabia zake
inaweza kuzalishwa katika mioyo ya wengi.
Hatimaye Mungu atazamapo duniani anaweza kuona sura yake ambayo imeumbwa
kwa Neno lake ndani ya wale waliomwamini Yesu.
Dunia inaweza kujawa na utukufu na sura ya Bwana
kwa njia ya wanadamu kujazwa Neno la Mungu, na kuishi kwa tabia za Neno hilo, hii ni sura ya Mungu
duniani.
D. Neno Lipandwapo Moyoni Halionekani Ingawa Linatenda Kazi
Ili
mbegu iote lazima ipandwe kwenye ardhi. Ili Neno la Mungu lifanye kazi inabidi
lipandwe moyoni. Moyo wa mtu ni shamba la Mungu, ni shamba la
Neno lake.
Mbegu yenye matokeo au mavuno ni ile ipandwayo
ardhini, Neno lenye matokeo au mavuno ni lile lipandwalo moyoni.
Daudi aliliweka Neno la Mungu moyoni, Neno lilipandwa
moyoni mwake. Matokeo yake au mavuno
yalikuwa ni kutotenda dhambi, roho
yake haikutenda dhambi“Moyoni mwangu
nimeliweka neno lako, nisije nikakutenda dhambi” (Zaburi 119:11).
Yakobo aliandika kwamba, Neno lililopandwa ndani lina
matokeo au mavuno; nayo ni kuokoa roho au nafsi. Neno linafanya upya nafsi zetu, linatupa
fikra na mfumo wa ki-ungu katika mawazo yetu, hutuokoa na mfumo wa dunia na
dhambi katika mawazo yetu, “Kwa hiyo
wekeeni mbali uchafu wote na ubaya uzidio, na kupokea kwa upole neno lile
lililopandwa ndani liwezalo kuziokoa roho zenu.” (Yakobo 1:21).
Mwandishi wa Mithali alionyesha kwamba maneno ya Mungu yaliyohifadhiwa moyoni,
yaliyopandwa ndani yetu ni afya ya mwili
wetu, imeandikwa, “Mwanangu, sikiliza
maneno yangu; Tega sikio lako, uzisikie kauli zangu. Zisiondoke machoni pako uzihifadhi ndani ya
moyo wako. Maana ni uhai kwa wale
wazipatao, Na afya ya mwili wao wote.” (Mithali 4:20-22).
Neno kama mbegu ya Mungu lipandwapo mioyoni mwetu
lina mavuno katika roho, nafsi na miili yetu.
Linaleta sura ya Mungu rohoni (utakatifu), katika nafsi (kubadilishwa
mfumo wa kufikiri) na miili (uponyaji na afya).
E.Neno
Litendalo Bila Kuonekana
Kama
ilivyo mbegu ya kawaida, ipandwapo haionekani jinsi inavyofanya kazi. Kutoonekana kwa mbegu hiyo hakuzuii isifanye
kazi. Mbegu ya Neno inafanya kazi ndani
ya waaminiyo hata kama haionekani. Paulo aliandika, “kwasababu hiyo sisi nasi twamshukuru Mungu bila kukoma kwa kuwa
mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama
neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu na
ndivyo lilivyo kweli kweli; litendalo kazi pia ndani yenu ninyi mnaoamini.”(1
Wathesalonike 2:13). Neno kama mbegu
linatenda kazi ndani yako uaminiye hata kama
huoni linatendaje tendaje.
Huwezi kuona au kujua jinsi mifupa ya mtoto
inavyoongezeka na kukua ndani ya tumbo la mama mjamzito. Unacho ona ni matokeo, yaani mtoto kuzaliwa! Pia huwezi kujua njia ya upepo, tunajua upepo upo
baada ya kuona matokeo yake. Kadhalika Neno la Mungu tunaona matokeo yake
ingawa hatuoni njia yake, jinsi linavyotenda kazi, “Kama vile wewe usipojua njia ya upepo ni ipi, wala jinsi mifupa ikuavyo
tumboni mwake mja mzito; kadhalika hujui kazi ya Mungu, afanyaye mambo yote”
(Mhubiri 11:5). Baada ya kusikia, kusoma
au kutamka Neno katika mazingira yako, linatenda kazi kama
mbegu pasipo wewe kujua. Neno hilo huleta sura ya Mungu
maishani mwako na katika mazingira.
F. Mkulima Humwagilia Mbegu na Kuitunza hufanya kitu ili Mbegu Itendayo
kazi ndani ya udongo itokee nje au ilete mavuno.
Kama
vile mkulima afanyavyo, sisi pia ili Neno ambalo ni mbegu lifanye kazi au
lidhihirike, tuone matokeo na kupata mavuno, inabidi tufanye kitu. Ingawa limeshaanza kufanya kazi moyoni
inatupasa tulitengenezee mazingira ya kukamilisha kazi yake,
‘tulimwagilie’. Inatupasa tufanye mambo
yafuatayo:
- Tulitafakari-Lizunguke Katika Fikra zetu
- Tulitende
- Tuliseme
- Nalo litatoa Mavuno
Joshua aliambiwa afanye mambo haya juu ya mbegu ya Neno,
akapata mavuno. Wewe pia katika maisha
yako yote, yafanye haya ili Mbegu ambayo ni Neno la Mungu likupe sura ya Mungu;
Uponyaji, Utakatifu, hekima, maarifa, Nguvu, nk.
Hebu soma maandiko haya:
Kitabu hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako (liseme
Neno)bali yatafakari maneno yake mchana
na usiku(lifikiri lizungushe Neno katika mawazo na fikra mchana na usiku). Upate kuangalia na kutenda sawa sawa na
maneno yote yaliyoandikwa humo(ulitende Neno). Ndipo
utakapoifanikisha njia yako (Neno litaleta matokeo/ mavuno katika maisha
yako).
Yoshua 1:18
No comments:
Post a Comment