Tuesday, April 7, 2015

Ushuhuda wa Mwinjilisti Grace Mbise



Malaika na Vita vya Kiroho

Maandiko matakatifu yanaonyesha kwamba malaika wa Mungu wapo na wanatenda kazi pamoja na watu wa Mungu; katika kuwahudumia na vita vya kiroho.  Kwa mfano hebu soma maandiko haya, “Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazunguka wamchao na kuwaokoa” (Zaburi 34:7), “Waaibishwe wafedheheshwe, Wanaoitafuta nafsi yangu.  Warudishwe nyuma, wafadhaishwe…Wawe kama makapi mbele ya upepo, Malaika wa BWANA akiwaangusha chini.” (Zaburi 35:4-5), “Kwa kuwa atakuagizia malaika zake Wakulinde katika njia zako zote.” (Zaburi 91:11). Katika makabiliano ya vita vya kiroho, malaika wa Mungu wanatenda kazi hata sasa, ikiwa tunawaona au ikiwa hatuwaoni.  Mama Mbise amepewa neema ya kuona utendaji wa malaika wakati akiwa katika mapambano ya kiroho katika huduma.  Karibu usome shuhuda hizi tena:

Wakati fulani mgonjwa aliletwa nyumbani kwangu ili aombewe.  Alikuwa ni ndugu wa rafiki zetu huko Njani.  Alitokea hospitali ya KCMC.  Alikaa siku tatu wakati huo huo tukiendelea na maombi.  Vita vilikuwa vikali sana alikuwa hawezi kuongea mdomo umepinda nk.  Baada ya siku nne alianza kupata ufahamu.  Baada ya wiki moja alianza kukaa na kufanya mazoezi ya kutembea.  Tulikuwa na dada aliyekuwa akitusaidia kazi aitwaye Esta aliokea Nkwanekoli.  Siku moja saa tano mchana  wakati Esta anamwogesha mgonjwa, mimi nilikuwa chumbani naomba.  Baada ya kumaliza maombi nikakaa kitandani, ghafla upepo ukaanza kuingia chumbani kwa mfano wa moshi, ulikuwa wa rangi kama ya kijivu au bluu.  Ulikuwa ni mfano wa ukungu mzito.  Nikaanza kushindwa kupumua.  Nikaanza kuomba na kukemea.  Ghafla ndani ya ule moshi nikaona viumbe vingii!, kama viwatu vidogo vidogo.  Mwonekano wake ulikuwa kama askari wengi wenye mavazi ya kivita, walikuwa wameshika vitu mfano wa virungu (Maandiko yanasema vita vyetu vinahusika na jeshi la pepo wabaya katika ulimwengu wa roho, inawezekana hawa walikuwa ni moja ya kikosi cha pepo hao- Waefeso 6:12).  Walianza kunipiga na mimi niliendelea kukemea, nikaona kama vile ninazidiwa nguvu nikalegea wakachukua miguu yangu na kuiweka kitandani.  Yakatokea majitu mengine makubwa mawili, walikuwa na maumbo kama watu lakini hawakuwa watu! (Inawezekana hawa ni wakuu wa giza ambao walikuwa ni majemedari wa jeshi la pepo hawa). 

Wakachukua kamba kubwa wakaiviringisha na kunifunga mpaka kwenye mabega yangu.  Wakaanza kunibeba na kusema “Dawa yake huyu ni kumbeba na kumpeleka, ni kumtowesha asionekane tena”  Nikajiona natoka kitandani mpaka pua yangu ikagusa dari.  Ghafla nilisikia sauti ya kishindo kama radi “PAAA” Wakatokea malaika wawili wakubwa!! Mmoja akasimama kushoto kwangu na mwingine kulia.  Kila mmoja ameshika upanga, ambao ulikuwa ni kama moto uwakao!! Sikujua wameshikaje mapanga yale maana mpini ulikuwa hauonekani ilikuwa kana kwamba wameshika kwenye moto.  Malaika hawa walikuwa wana utisho mkuu.  Walikuwa wazuri wenye sura za huruma zenye kung’aa, pia walikuwa na mabawa makubwa yaliyovuka mabegani mwao.  Urefu wao haukupungua futi  saba au nane hivi.  Mmoja wao akasema, “hapo hapo asitoke hata mmoja”  Akafunua chini kwa mfano wa mtu afunuaye  mfuniko wa shimo la maji machafu.  Wale malaika wakawaambia, “Hamna mamlaka huyu ni mtumishi wa Mungu, amekombolewa na damu ya Yesu”.  Wakachomoa kitu mfano wa kadi za benki au kadi ya ATM, kilikuwa cha rangi nyekundu wakawaonyesha na kusema, “Huu ndio ushahidi”, Halafu wakasema, “Mko wangapi?” wakajibu, “Elfu moja mia sita” , Malaika akasema, “Kuanzia sasa hamtafanya kazi tena duniani” Halafu wakawatumbukiza ndani ya lile shimo kwa kuwaamrisha. 

Wakati huo nilikuwa kitandani nimefungwa kamba, Dada Esta akafungua mlango alikuja kuchukua mafuta ya kumpaka mgonjwa, akaanguka chini na kuanza kunena kwa lugha muda mrefu.  Alipokuwa akinena kamba niliyokuwa nimefungwa ikaanza kulegea.  Alipomaliza kunena tu, kamba zote zilikuwa zimeniachia (Kunena kwa lugha za Roho Mtakatifu kunaweza kumfungua mtu na kamba za kishetani zinazoonekana na zisizo onekana, usiache kunena kwa lugha.  Mfano huo tumeuona kwa dada Esta).  Wakati huo malaika walikuwa wameshaondoka.  Baadaye Esta aliniambia alipofungua mlango aliona watu wanaongaa sana na akashindwa kustahimili na kuanguka.

Baada ya tukio hilo Shetani alijaribu kulipiza kisasi.  Wakati huu nilikuwa na safari ya kwenda Mulala kuombea mtu mwenye pepo.  Nilipofika lile pepo likasema, “wewe mama umetunyanyasa lakini tutalipiza kisasi, umewatesa wenzetu lakini utaona”.  Sikujua hicho kisasi kitalipwa kwa vipi.

Siku moja jumapili asubuhi saa nne hivi nilikuwa nyumbani na wote walikuwa wame enda kanisani.  Nilikuwa najisikia mdhaifu  kidogo.  Nilikuwa chumbani mlango ukiwa umefunguliwa kidogo. Nikaona mtu ameingia sebuleni. Tangu alipokanyaga sebuleni nikasikia hali mbaya ya nguvu za giza, akaanza kuja chumbani alipokaribia nilianza kuona giza.  Baada ya hapo nikapoteza fahamu.  Nikajikuta nipo kwenye sehemu yenye giza kuu, lakini kuna watu wengi wenye hofu.  Eneo hilo lilikuwa limetengwa sehemu, sehemu (sections).  Miezi kama mitatu iliyopita niliwahi kwenda kumwombea mama mmoja eneo la Poli, alikuwa na kansa.  Nikamwona mama huyo katika sehemu mojawapo akaniambia, “Mama Mbise umekuja huku! Afadhali jamani niombee”  Nikamwambia “ahh umekujaje huku?” hapohapo nikaona lebo imetokea usoni pake imeandikwa, “MCHAWI”. Nikamwambia kumbe ulikuwa mchawi! Nitakuombeaje?  Machozi  yakamdondoka.  Baadaye niliporudi duniani nilienda kumwulizia yule mama nikaambiwa alishafariki na miezi mitatu imepita  (Mama huyu alitaka kuponywa ugonjwa wa kansa kwa kuombewa lakini hakutubu na kumpokea Yesu.  Wewe kama ni mgonjwa usitake Yesu akuponye tu, mpe maisha yako, maana ukifa bila Yesu utapotea, hata kama uliombewa ugonjwa).

Nikapita sehemu nyingine nikamkuta shangazi yangu alikufa miaka ya sabini kwa kifua kikuu.  Mwili wake ulikuwa kama mwili wa aliyeoza ukitoa usaha, alikuwa kwenye hali ya mateso.   Kuna mtu alikuwa mbele yangu akiniongoza.  Mahali hapa palikuwa na giza kuu lakini mwili wangu ulikuwa ukitoa mwanga.

Akaja kiumbe mmoja  mfano wa mtu, akanichukua na kunifungia sehemu ambayo ilikuwa ni kama mahabusu.  Ilikuwa ni ndani ya mwamba mkubwa.  Akatokea mmoja mfano wa jemedari, alionekana kuwa na mamlaka kuliko wengine akasema, “wewe si unajifanya mbabe utafia humohumo”.  Akachukua kitu mfano wa kufuli kubwa na kunifungia.  Nilianza kulia na kulia.  Kulikuwa hamna namna ya kutoka nikasikia kukata tamaa.  Nikomba na kusema, “Mungu  naomba unitetee maana sitaweza” Mara! Nikasikia sauti kama ya mwanadamu, tofauti yake ilikuwa nzito, iliyotulia na ilikuja na hali ya tetemeko, alisema, “Mbona umekuwa mwoga, iko wapi imani? Je mfukoni mwako kuna nini?”.  Nika angalia ndani ya jaketi langu nikakuta wembe nikamjibu, “Kuna wembe” Sauti ikaniambia “Je unaamini ninaweza kukutoa sehemu uliyopo kwa huo wembe?” nikajibu, “Ndiyo Bwana naamini” Sauti ikaniambia, “Anza kukata huo mwamba kwa imani na kutoka kama nilivyokufundisha”.  Nikajiuliza kwani alinifundishaje?, kisha wazo likanijia, “Kila kitu kwa jina la Yesu”.  Nikaanza kusema kwa jina la Yesu, huku ninakwaruza mwamba kwa wembe, nilipokuwa nafanya hivyo nikaangalia juu, nikaona kiganja kikubwa kimeshika wembe mkubwa mfano wa ule nilioshika.  Ule wembe mkubwa ukakata ule mwamba.  Wembe wangu ulipofikia ndipo ule mkubwa uliposimama kukata.  Sauti ikaniambia “Inua mikono yako juu”.  Kumbe kwa juu walikuwapo malaika wawili wakubwa wamesimama.  Walikuwa hawana mabawa.  Wakanivuta na kunitoa mahali pale, kisha pakajifunga.

Malaika wale wakanichukua tukaanza kupaa.  Tulipokwenda kwa kitambo kidogo nikawaambia tupumzike maana nimechoka.  Wakaniambia “Hapa bado ni himaya yao (Mashetani) wataendelea kutufuatilia.  Tukafika eneo ambalo lilikuwa na kitu kama sahani ya shaba kubwa, wakaniambia nikae upande wa pili wa ile sehemu.  Akaniambia mmoja “huu ni mpaka wa dunia na kuzimu”.  Wakati huu malaika hawa walibadilika na walikuwa na mabawa!  Tulipokwisha kupumzika walisema, “sasa tumeshatoka huko tuendelee”.  Fumba fumbua nikajikuta niko juu sana, tukafika mahali ambapo nikaangalia chini na kuona kitu kama korongo lenye  giza.  Nikawauliza kule ni wapi wakaniambia ni duniani.  Nikawauliza nitarudi tena kule.  Wakasema utarudi bado unayo kazi ya kufanya.  Nikawaambia nitaendaje, ninyi mnayo mabawa, mimi nitaendaje?.  Wakasema tutakupa mabawa.  Mmoja akanigusa mabega yakatokea mabawa, lakini si makubwa kama yao.  Nikaanza kushuka na kurudi duniani, niliyapenda sana yale mabawa.  Nilipokaribia chini nilianza kuyatambua maeneo kama Maji ya chai, Usa riva nk.  Nilipogusa ardhi tu mabawa yakatoweka, nilianza  kulia; mabawa yangu, mabawa yangu.  Nikajikuta nipo nyumbani kwangu Makumira.

Mwaka 1989 nilipata mwaliko wa kwenda Same kufanya huduma kwa mchungaji  Emanuel Mande.  Kabla sijaenda nilipata vita sana.  Nilitokewa na viumbe vitatu vilivyokuwa ni kama wanawake.  Walikuwa wanafanana sana, huwezi kuwatofautisha kirahisi.  Tofauti yao ndogo ilikuwa ni urefu.  Mmoja alikuwa mrefu zaidi na mwingine mfupi kidogo.  Nilipowatiisha na kuwakemea kwa jina la Yesu wakaniambia, “Usituangamize tumetoka Same sisi ndio viongozi wa anga la Same, tumesikia unakuja, tumekuja kukuonya usije, ile himaya ni yetu”  Nikawaambia Same nitakuja katika jina la Yesu.  Nikawauliza kwani nyie ni nani? Nikamuuliza mmoja aliyekuwa mrefu zaidi, “wewe ni nani?” akaniambia, “Uzinzi” nikamwuliza mwingine akasema, “Naitwa Tamaa” wa mwisho akasema anaitwa “Uasherati”.  Baada ya kuwakemea wakaondoka.

Siku mbili baadaye mimi na mama Baraka (mama Kachee) wa Poli tukaanza safari ya kwenda Same.  Safari ilikuwa ngumu magari tuliyokuwa tunapanda yaliharibika.  Tulitoka Arusha asubuhi tukafika Same usiku.  Tulipofika tu umeme ukakatika mji mzima, ilikuwa twende kanisani usiku huo.  Kesho yake tulianza semina.  Usiku wa kwanza wale wale wakuu wa giza walionifuata Arusha wakatokea tena   na kuanza kupiga makelele.  Walikuwa wamekuja na majitu mengine makubwa.  Jitu moja likanikaribia na kutaka kunikaba.  Wale wengine walikuwa wakilishangilia na kuliambia kwa Kipare, “tumia kile kitu chako” mimi sijui Kipare lakini nilielewa katika roho.  Ukanijia ufahamu kwamba kitu hicho ni ukucha   mrefu uliopo katika mkono wake wa kushoto ukucha huo ulikuwa na sumu, nikaushika na kuung’oa.  Jitu lile likaishiwa nguvu menzake yakalibeba.  Baada ya hapo kulitokea uamsho na mabadiliko makubwa Same.

Asubuhi moja nilimwambia mchungaji Mande, “Kuna wachawi, mapepo yanakuja kunisumbua usiku ninavita sana”  Akasema, “mchawi hawezi kunigusa mimi nimeokoka”  nikamwuliza, “kwani mimi sijaokoka?”akasema “mimi sijui lakini Shetani hathubutu kunigusa”  Nikamwambia “Leo usiku watakuja kwako na wewe uwaone” akajibu “hawaweziii” halafu akacheka sana.

Usiku huo tukaomba na kuagana kwenda kulala.  Nilipoweka kichwa kwenye mto tu, nikasikia bati linatikisika.  Yakaingia ndani nikayaambia kwa jina la Yesu hamna mamlaka mmekuja kufanya nini? Yakasema “tumekuja kukuangamiza maana unatusumbua katika huu mji”  Nikayaambia kwa jina la Yesu msinisumbue hapa nendeni kwa Mchungaji Mande.  Saa ileile yakaenda.  Nikasikia chumbani kwa Mande anapiga ukuta mateke, anaongea nayo akasema, “Nyie washenzi hamna adabu mmekuja kufanya nini huku”.  Mke wake akamwuliza, “Baba Debora kuna nini?”.  Akajibu, “Si hawa washenzi walikuwat wananishika miguu na kunitoa kitandani”

Asubuhi nilipoamka na kupiga mswaki.  Mchungaji naye akaamka akaniangalia na akacheka sana.  Akasema “wewe Mbise wewe! wewe ni mtu hatari sana” nikamwuliza kuna nini? Akasema, “Walikuja usiku wakanishika miguu na wakati  nimeokoka?”  akaendelea kusema, “Mama Mbise nimetambua vita ulivyo navyo endelea na huduma mimi nitakuombea huduma yako ina vita sana”.

No comments:

Post a Comment