Ushuhuda (Mwinjilisti Grace Mbise)
Mungu wa mwinjilisti Filipo ni Mungu
wa mwinjilisti Grace Mbise pia. Katika Matendo ya Mitume 8:38-40 maandiko
yanasema, “Akaamuru lile gari lisimame;
wakatelemka wote wawili majini, Filipo na yule towashi; naye akambatiza. Kisha, walipopanda kutoka majini, Roho wa
Bwana akamnyakua Filipo, yule towashi asimwone tena; basi alikwenda kwake
akifurahi. Lakini Filipo alionekana
katika Azoto…” Kitu ambacho nimejifunza katika maisha na huduma ya mama
Mbise ni kutokumwekea Mungu mipaka ya kutenda jambo. Tabia hii ilimwezesha
kukutana na muujiza au ishara ambayo ilionekana katika maisha ya Filipo.
Yafuatayo ni maneno ya ushuhuda aliyonisimulia mama Mbise:
Wakati fulani mwaka 1984, nilikuwa na huduma Tengeru
nilikuwa ninamwombea mtu mwenye pepo. Tulikuwa pamoja na baadhi ya wanachuo cha
mifugo Tengeru. Mume wangu alinipa
masharti kwamba siku hiyo ni lazima niwahi nyumbani, nifike kabla ya saa kumi
na moja jioni. Aliniambia kama ni zaidi
ya saa kumi na moja nisirudi nyumbani.
Baada ya maombi niliangalia saa
na ilikuwa saa kumi na moja kasorobo.
Tengeru na Makumira, tulipokuwa
tunaishi pana umbali usiopungua kilometa saba au tano. Sehemu tuliyokuwa tunafanyia maombi hapo
Tengeru ilikuwa karibu na barabara.
Nikaenda haraka kituoni na saa hiyo ilikuwa saa kumi na moja kasoro nne!
Nikajiuluza itawezekanaje nifike nyumbani katika hizi dakika nne? Hapo hapo
nikapata wazo kwamba ni kitu gani ambacho hakiwezekani kwa Mungu?
Siku moja kwake ni kama miaka elfu na miaka elfu ni kama
siku moja. Nikaomba na kusema, “Mungu
katika dakika hizi nne naomba muujiza nifike nyumbani, kama
utaleta gari, ndege au malaika.” Baada
ya hapo nikafumba macho. Nilikuwa kama
aliyepitiwa kimawazo, kisha nikafungua macho.
Nilijikuta niko nje ya fensi ya nyumba Makumira, ilikuwa bado dakika
moja! Ile nimeingia ndani tu mzee
akatoka chumbani na kunikuta sebleni akasema, “Bahati yako”. Nikamjibu, “ungejua ni kitu gani kimetokea!”
Baada ya tukio hili la ajabu nilipata imani moyoni mwangu
kwamba hata katika mikutano yangu ya Injili Mungu anaweza kunipeleka ki-muujiza
kama alivyonifanyia muujiza huo. Mwaka 1987 nilikuwa nimealikwa katika
mkutano wa Injili Loitoktok Kenya. Nilikuwa sina nauli. Nikaamua kuchukua begi langu na kuanza kwenda
kwenye mkutano kwa mguu. Nikasema, “Yule
Mungu aliyenisafirisha kwa malaika toka Tengeru mpaka Makumira ataniwezesha
kufika Loitoktok”. Nilitembea mwendo
kama wa kilometa moja hivi, katika njia
ya mikahawani kutoka Makumira shule ya msingi, ni njia ya kuelekea chuo cha
theolojia Makumira. Nikafika chini ya mti mmoja na nikajikuta
nimeangalia ule mti, nikaona jani moja la mti likianguka. Nilishawishika kuendelea kuliangalia lile
jani na lilipofika chini halikuwa jani zilikuwa ni pesa!!
Zilizovingirishwa. Zilikuwa ni shilingi
elfu nane. Pesa hizi zilinitosha kwenda Kenya. Nikaomba Mungu na kusema, “kama
pesa hizi ni zangu Mungu nakuomba nisikutane na mtu njiani anayekuja au
anayeenda” Sikukutana na mtu yoyote,
ingawa barabara hiyo ilikuwa ni njia ya watu wengi wakiwemo wanafunzi wa sekondari,
msingi na chuoni.
Mungu hazungumzi au kutenda kwa njia moja tu. Anazo njia
nyingi. Nilipata safari nyingine tena ya
kwenda Morogoro Kilombero. Katika kanisa
la Anglikana ambalo alikuwepo mchungaji Malekela. Kulikuwa na mkutano wa umoja
wa makanisa. Mpaka naanza kuondoka nyumbani nilikuwa sina nauli. Moyoni nilijua Mungu atafanya muujiza na
kunipa nauli. Nilichukua begi langu na
kuanza kwenda stendi. Ilikuwa ni mwaka
1988. Basi, nilipokuwa nachukua begi mtu
mmoja alisema, “Hivi kweli unaakili? Utakwendaje huna nauli?” nikamjibu “nitaenda”. Wakati nimekaribia geiti la chuo cha
theolojia Makumira, Ndugu mmoja aitwaye
Eliabu Mungure alikuja nyuma yangu akinikimbilia na kuniita. Nikasimama nikamwuliza kuna nini? Akaniambia
ana barua yangu, imemtesa sana mpaka akaja nyumbani na akanikosa, maana
walimwambia ndio tu nimeondoka kwenda safarini.
Nilipofungua ile bahasha nilikuta pesa za kutosha kunifikisha Morogoro,
pamoja na chakula cha njiani.Mungu anapokutuma anajua ni jinsi gani utaweza
kwenda usiogope na kumwekea mipaka. Mara nyingi tunashindwa maana hatumwamini
na tunamwekea mipaka. Muujiza hauji
mpaka uchukue hatua. Tunapoamini kitu
tukitende ili kumruhusu Mungu kufanya Muujiza kwa imani zetu.
Katika shuhuda hizi ambazo amezitoa
mama Mbise tunajifunza kwamba: Mungu anaweza kufanya chochote tukiamini kwamba
anaweza na kuchukua hatua za imani. Ikibidi Mungu anafanya hata muujiza wa
kumnyakua mtu kwa kuwa amemwamini, usimwekee Mungu mpaka katika maombi yako,
mtarajie kwa mambo makubwa zaidi. Kwa upande mwingine tunajifunza kwamba
wainjilisti wanatakiwa wapelekwe kuhubiri injili kwa kutumia pesa na mali
zetu. Mama huyu alimtegemea Mungu
asilimia mia, Mungu alifanya muujiza wa pesa na kumpeleka. Mungu anaposema moyoni mwako umpeleke
muhubiri usiufanye mgumu moyo wako. Uwe
mwepesi kutenda kama alivyotenda Eliabu
Mungure, usisubiri mpaka Mungu ageuze jazi liwe pesa! Ingawa anaweza kutenda
hivyo ili atukuzwe, Maandiko yanasema, “Tena
wahubirije wasipopelekwa?” (Warumi 8:15).
No comments:
Post a Comment