Wednesday, February 11, 2015

Hukumu ya Kifo cha Milele



 Hukumu ya Milele (Ujumbe huu upo katika 'traks' ya uinjilisti tuliyoiandika katika huduma ya LICO)
Sheria mara nyingi hutoa hukumu ya kifo kwa mtu aliyeuwa kwa kukusudia. Mtu auaye huuwawa.  Mwanadamu alipotenda dhambi aliingia katika hukumu ya kifo. Kifo ninachokitaja hapa, sio kutokuwepo duniani, bali ni kutokuwa na Mungu milele, mwanadamu alijiuwa mwenyewe kwa mauti kupitia dhambi. Mwanadamu alitengana na Mungu; Katika busani ya Edeni Adamu na Eva walipotenda dhambi walitengana na Mungu. Hata hivyo kifo si kutengana na Mungu tu, bali pia ni kutupwa katika ziwa la moto na kiberiti milele na milele.

Kwa kuwa wanadamu wote wametoka kwa Adamu, wote wametenda dhambi na wameshahukumiwa kifo cha milele na Mungu (Warumi 6:23). Haijalishi unaenda kanisani, msikitini au hauendi popote, ikiwa wewe ni mwanadamu hukumu ya kifo cha milele ipo juu yako. Ikiwa umesoma au hujasoma, tajiri au maskini, mlemavu au mzima, ikiwa wewe ni mtu, Jehanam ipo mbele yako. Ukifa sasa hivi utapotea milele na milele! Kwenda kanisani hakukufanyi umwone Mungu. Kutoa sadaka hakukufanyi usihukumiwe. Usijidanganye kwa kuwa unashiriki sakramenti tu, ndio sababu ya kumwona Mungu. Sio ubatizo, meza ya Bwana, kipa imara, wala kuombewa ukifa itakayokuwezesha kutoka katika hukumu ya kifo cha milele, Jehanam. Mambo hayo ni mazuri, lakini hayakufanyi ukubalike na Mungu. Siku ya hukumu Mungu atakukataa, pamoja na kupitia yote haya. Usijidanganye wala usiruhusu mtu akudanganye, utakufa peke yako.
Mungu Anataka Kitu Kimoja Tu
Yesu aliwaambia Wayahudi, “Kwa hiyo naliwaambieni ya kwamba mtakufa katika dhambi zenu; kwasababu msiposadiki ya kuwa mimi ndiye, mtakufa katika dhambi zenu.” (Yohana 8:24). Wanadamu wote wanadhambi, hawatakiwi kufa katika dhambi zao. Wakifa katika hali hiyo watakutana na hukumu ya kifo cha milele, Jehanam ya moto. Ili mtu asife katika dhambi zake na kuhukumiwa lazima aamini Yesu NDIYE. 1.Ndiye aliyekuja kufanyika dhambi ili tuhesabiwe haki, 2.Ndiye aliyemwaga damu dhambi zetu ziondolewe, 3.Ndiye aliyekufa badala yetu tusife milele, 4.Ndiye njia ya kupitia ili Mungu amkubali mtu na sio vinginevyo. 5.Ndiye anayeondoa asili yetu ya dhambi, atupe asili ya Mungu mwenye uzima wa milele. Maandiko yanasema, “Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyemwamini amekwisha hukumiwa; kwasababu hakuliamini jina la Mwana pekee wa Mungu.” (Yohana 3:18). Kama hujawahi kwa kinywa chako kumwambia Mungu akusamehe dhambi zako, na ukatamka mbele zake kwamba, unaamini Yesu alitolewa kwaajili ya dhambi zako, hivyo aingie ndani yako kama Mwokozi; Usijidanganye kwamba utaingia mbinguni kwa kitu kingine chochote unachotegemea. Hasira ya Mungu inawaka juu yako! Hivi ninavyoandika UKIFA SASA HIVI NI OLE WAKO! Ni sawa na mtu aliyelala katika treni na daraja limevunjika kilometa moja tu! Ajabu! yeye amelala au amesitarehe na kusoma gazeti. Angekuwa na busara angetafuta namna ya kujiokoa.

Usistarehe sasa na kuona hamna kitu, unayohukumu ya kupotea milele, itatimia ukifa tu, ghafla utajikuta kwenye mateso. Unatoroka hukumu na hasira hiyo kwa kupitia Yesu tu, “Basi zaidi sana tukiisha kuhesabiwa haki katika damu yake, tutaokolewa na ghadhabu kwa yeye.” (Warumi 5:9). Usikubali mtu akuzuie kumpa Yesu maisha yako. Kwa nini usubiri watu wakuombee uwekwe pema peponi ukifa? Si ni heri ujiombee mwenyewe kwa kutubu dhambi na kumpa Yesu maisha kabla hujafa. Hakuna andiko linaloonyesha watu wakiombewa baada ya kufa Mungu atawapokea, huo ni uongo wa mchana wa Shetani. Ila yapo maandiko yanayowataka watu watubu na kumpa Yesu maisha kabla ya kufa. Kwa kuwa huna uhakika ukifa itakuwaje, jihakikishe sasa hivi ukiwa hai. Usije ukahukumiwa kifo cha milele. Mtu yeyote asiyejua anaenda wapi akifa na anajitia moyo Mungu ndiye anayejua anakokwenda, mtu wa namna hii anaenda Jehanam. Kiongozi wa dini, baba, mama au mtu mwingine yeyote hatawajibika na kupotea kwa roho yako. Siku ya hukumu; baadhi ya maaskofu, wachungaji, wazazi na viongozi wengine wa dini, watoa hesabu kwa watu waliowazuia kumpa Yesu maisha yao na kuokolewa.
Utaenda Wapi?
Sasa jiulize, “mimi nitaenda wapi baada ya kifo?” Usipomkubali Yesu kama Mwokozi wako utakutana na mateso ya milele, hii ni hukumu ya kifo cha milele, yaani Jehanam. Biblia inasema, “Baada ya kifo ni hukumu” (Waebrania 9:27).  Hivyo kabla ya kifo chako ni lazima ujiandaye kwa njia ya kumpokea Yesu na kuokolewa.  Amua sasa! si kesho, kesho inaweza isifike.  Sema sala hii:Mungu wangu, ninakuja kwako, nisamehe dhambi zangu.  Yesu Kristo ingia moyoni ulikufa na kufufuka, ili mimi niende mbinguni, nioshe kwa damu yako. Amina.

Ikiwa umempa Yesu maisha yako baada ya kusoma karatasi hili au kama unaswali lolote, au unahitaji msaada wa kiroho wasiliana nasi:
LICO
P.O.Box 15634
Arusha, Tanzania.
Simu :+255 717 354501

No comments:

Post a Comment