Tuesday, September 2, 2014

Vita Vizuri vya Imani - III

KARAMA YA IMANI NA VITA VIZURI

 Ukiwa na mti wa Krismasi ulio na urembo wa  matunda juu  yake, kitu cha kufahamu ni kwamba matunda yake yamewekwa kwa muda tu. Sio ya asili yake. Wakati wowote yatandolewa. Lakini machungwa katika mchungwa ni asili yake kuwa mchungwani.
           
 Karama za Roho katika maisha yetu, hazipo wakati wote juu yetu huja na kuondoka, kama matunda katika mti wa Krismas. Roho huzileta zinapohitajika, sio za kwetu ni za Roho. Ila tunda la Roho ni sisi tunalolizaa kwa uhusiano wetu na Yesu katika Roho Mtakatifu, ni la kwetu na la asili yetu kama chungwa kaika mchungwa.

 Karama za Roho zilizotajwa 1 Wakorintho 12, zipo tisa. Msitari wa 9 unaonyesha kuwa kuna karama ya imani, hii ni karama ya imani maalum. Imani hii huletwa na Roho Mtakatifu katika mazingira maalum, kwa mambo ambayo ni Mungu tu awezaye kufanya.

 Maandiko yanasema tumpinge Shetani tukiwa thabiti katika imani
(1 Petro 5:8-9). Hii ni imani yetu, lakini mara nyingine, Roho wa Mungu anaweza kutupa imani maalum kukabiliana na Shetani.

Yesu inaonekana alitumia karama hii katika Mathayo 8:24. Hapa tunaona alipokuwa ziwani  na wanafunzi walitokewa na msukosuko majini. Neno hili msukosuko tafsiri yake kwa Kiyunani ni seismos, ambayo maana yake halisi ni tetemeko la nchi lililosababisha mawimbi. Pia inawezekana liliambatana na upepo mkali. Ukisoma mpaka msitari 34, utagundua ng’ambo ya ziwa kulikuwa na mtu mwenye jeshi la pepo. Inawezekana kabisa msukosuko huo alileta Shetani kujaribu kumuua Yesu au kumpinga asiende kufanya huduma ya kutoa pepo hao.

 Kitu gani kilichomfanya Yesu aukemee upepo? (msitari 26). Huwezi kukemea kitu kisichosikia. Bila shaka kwa kukemea upepo alikemea nguvu iliyokuwa nyuma yake na kusababisha dhoruba. Hapa inawezekana kabisa ilikuwa ni karama ya imani, maana wanafunzi walisema,”……Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari za mtii?”(Mathayo 8:27). Karama ya imani inaweza kufanya mambo ambayo ni Mungu peke yake anaweza kufanya. Hapa Roho wa Mungu ndani ya Kristo alimpinga Shetani aliyekuja kwa tetemeko na upepo kwa karama ya imani, kwa kukemea upepo na bahari.  Twaweza kusema kuna mazingira magumu katika vita vya kiroho unaweza kupewa karama ya imani maalum kushindana. Hii inakuja ghafla! Kama apendavyo Roho Mtakatifu. Sio kitu ambacho unapanga. Roho anakupa ujasiri na usemi wa ghafla bila kujali mazingira, yanaonekana vipi.

Katika vita Joshua alisimamamisha jua ili apigane na adui, ilkuwa ni karama hii (Joshua 10:13-27). Mungu Roho Mtakatifu alimletea imani hiyo katika vita. Hata sasa anaweza kukupa karama hii katika vita. Wakati fulani nilisikia ushuhuda wa mwinjilisti mmoja ambaye alitumiwa nyuki na wachawi akiwa kwenye mkutano. Ghafla! Akapata ujasiri na kuamuru nyuki wale waende katika nguzo moja iliyokuwepo mkutanoni. Nyuki wale walitii na kujikusanya kataka nguzo hiyo. Watu wengi waliona tukio hilo likawa muujiza uliokuwa ishara kwao, iliyofanya wampe Yesu maisha yao. Hii ilikuwa ni karama ya imani katika vita ndani ya mwinjilisti huyu.

Miaka ya tisini, walikuja Mbeya watumishi watatu wa kike kutoka Kongo.  Walishuhudia kwamba Mungu aliwaokoa wakati fulani walipokuwa katika huduma. Walienda kuhudumu misituni walipo mbilikimo (watu wafupi). Watu hao walifanya uchawi mbele yao na mti ukaanguka. Kisha wakawambia ikiwa wao kweli wana Mungu wafanye kama walivyofanya wao, walidai mungu wao ndiye alieangusha mti.


 Hofu iliwashika, lakini ghafla ujasiri ukamjia mmoja wao na akasikia anaulizwa na Roho wa Mungu, imani yako iko wapi? Walishikana mikono na kuanza kusema Yesu,Yesu, Yesu, Yesu…. Walipokuwa wakisema hivyo upepo, ukang’oa mti mkubwa zaidi! Mbilikimo wote walipiga magoti na kutubu.  Hii ilikuwa ni karama ya imani, iliyotenda kazi na miujiza, uliokuwa ishara kwa mbilikimo hata wakatubu. Wainjilisi hawa, ambao walikuwa wakifanya kazi ya kitume, Wakapona kuuwawa, karama ya imani iliwashindia vita.

1 comment: