Monday, September 1, 2014

Vita Vizuri vya Imani - II


Jinsi ya Kupigana Vita viziri vya Imani
Paulo alimwandikia Timotheo maandiko haya “Mwanangu Timotheo nakukabidhi agizo hilo liwe akiba, kwa ajili ya maneno ya unabii yaliyotangulia juu yako, ili katika hayo uvipige vile vita vizuri” (1 Timotheo 1:18). Vita hivi vizuri vinavyotajwa na andiko hili ni vipi? Andiko lifuatalo linatoa jibu, “Piga vita vile vizuri vya imani, …….. “( 1Timotheo 6:12). Kwa nini vita hivi vinapigwa? Vinapigwa ili kuilinda imani mpaka matarajio yatokee, anasema tena Paulo “nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, imani nimeilinda.” (2Timoteo 4:7). Baada ya kuilinda imani matarajio yake au matumaini yanaenda kudhihirika “ baada ya hayo nimewekewa taji ya haki ………….. “ (2Timoteo 4:8). Maandiko hayo yote yanatufundisha mambo yafuatayo:-
1. Vita vizuri vinapigwa kwa kutumia maneno ya unabii ( Neno la Mungu)
2. Vita hivi vizuri ni vita vya imani
3.Vita hivi vinapigwa kuilinda imani mpaka itakapo dhihirishwa madhihirisho yote, yanayotarajiwa.
Kipele Kilichokuwa Usoni
Wakati fulani nilikuwa na kiupele cha kuzaliwa nacho usoni na kilinikosesha raha. Ilifikia wakati nikakiamuru kiondoke kwa jina la Yesu. Niliona moyoni, Yohana 14:13 ni dhahiri na nikawa na uhakika (pistis), kwamba nikisema tu kitaondoka. Nilisema kwa jina la Yesu kiondoke na moyoni nikaona kimeondoka. Ingawa kilikuwepo nje moyoni hakikuwepo tena! Baada ya hapo nikaendelea kuamini (pisteuo) kwa njia ya shukrani, kutafakari Yohana 14:13, sifa, pia kuamuru udhihirisho utoke nje ambao tayari ninao moyoni. Matarajio yangu ya kuona udhihirisho ya kawa hai wakati wote. Nikijiona katika kioo nilikuwa naona kipele, Shetani alisema mawazoni “bado kipo” na mimi nikapiga vita vya imani kwa kuamini na kusema toka moyoni “Kimeondoka……” vita vya imani vinapiganiwa katika moyo na mawazo au mazingira kwa kutumia Neno la unabii, maandiko na jina la Yesu.
Mungu hujenga udhahiri wa Neno moyoni, Shetani hujenge maswali na mashaka akilini. Baadaye kipele kile kilipotea usoni, ingawa kilipotea siku nyingi moyoni. Niliyapata niliyotarajia kwa kuvumilia na kupiga vita kwa kuamini, Kwa kutenda mambo kinyume na mazingira.
Goita Ilipotea
Mtumishi wa Mungu Smith Wigglesworth alitoa ushuhuda wa mwanamke mmoja aliyeombewa katika mkutano wake, akiwa na ugonjwa wa goita. Baada ya kuombewa moyoni alipata uhakika goita imetoka. Aliona ni halisi imetoka kama Mungu alivyosema katika Neno. Alikuwa akijiangalia kwenye kioo na kusema goita haipo (haikuwepo moyoni katika Imani) ingawa ilikuwa inaonekana. Ilipita miaka takribani mitatu akiendelea kusema hivyo. Siku moja alishuhudia katika mkutano kwamba goita imetoka, watu walimcheka! Mmoja akamwita pembeni na kumwambia aache kusema hivyo anakuwa kama kichaa, wamesikia vya kutosha. Muda si mrefu ikapotea! Watu walipomuuliza akawajibu ilishapotea miaka mitatu iliyopita! Vita vya imani alivyopigana mwanamke huyu, vilihusiana na maneno ya watu, muda na mazingira ya ugonjwa kuwepo, alitarajia yasiyoweza kutarajiwa si kwa imani tu, bali pia kwa kuamini.


 Mitume Wakati wa Kanisa la Kwanza

Wakati mitume wanahuburi injili, mara kwa mara walikutana na upinzani. Hasa kutoka kwa viongozi wa dini. Waliwakataza wasihubiri kwa jina la Yesu (Matendo 4: 16-19). Hii ilikuwa ni imani ya Yesu inapingwa. Vita vizuri vya Imani vilipigwa kwa kusema yafuatayo kwa wapinzani, “….. maana hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia” (Matendo 4:20).
Mitume walishindania imani kwa kufanya atakavyo Mungu aliyekuwa dhahiri ndani yao, na kutii agizo ambalo Yesu aliwaagiza kuhubiri injili kwa kila kiumbe bila shaka lilikuwa dhahiri kwao. Hatimaye wakawa na uhakika mkuu wa walichofanya. Hii ilikuwa ni imani iliyoweza mpinga Shetani na matakwa yake ya kuzuia kuhubiriwa injili, alitaka kuzuia kupitia watu viongozi wa dini.
Kwa kanisa la Pergamo (Ufunuo 2:12-13), Yesu alisema, likaapo kanisa hilo ndipo penye sinagogi la Shetani. Lakini akalisifu kwamba halikuikana imani ya Yesu kwasababu ya dhiki za kishetani! Hili ni kanisa ambalo lilikuwa tayari kuifia imani. Mtu aliyeokoka kweli, lazima awe mwanafunzi wa Yesu. Mtu aliye tayari kufa kwa ajili ya imani ya Yesu ni mwanafunzi wa Yesu.


No comments:

Post a Comment