Sunday, August 31, 2014

Vita Vizuri vya Imani - I


Vita Vizuri vya Imani
Katika maandiko, Habakuki 2:4, Inaonyesha mwenye haki ataishi kwa imani. Hii pia imeonekana agano jipya; Warumi 1 :17, Wagalatia 3 : 11 na Waebrania 10:38. Maisha ya wenye haki ni imani yao, kwa upande mwingine kifo chake ni pale imani yake inapokufa.
Hapa tunagundua siri ambayo ni hii “Shetani anawinda imani ya wenye haki kuliko kitu kingine chochote”, kwa nini? Kwa kuwa imani ndiyo inakufanya uishi kama Mungu aishivyo, imani inakuunganisha na Mungu. Mungu anakuja kwako, na wewe unaenda kwa Mungu, kiunganishi ni imani. Kwa mfano, Mathayo 19:26-27, inasema, yote yanawezekana kwa Mungu. Marko 9:23, inasema yote yanawezekana kwake aaminiye. Hivyo ni kusema mtu anakuwa kama Mungu alivyo katika utendaji wake, ikiwepo imani; bila shaka Shetani anachukia imani kwa sababu hii. Hatimaye huja kuipinga au kujaribu kuidhoofisha. Katika sehemu ya kwanza tumeangalia imani kwa ujumla na mambo yapaswayo kufanya ili kuichochea. Sehemu hii ya pili ni ya vita ambayo hufanywa kwa kulinda imani au kuishindania na kwa njia ya kuitumia kumpinga Shetani kwa ahadi za Mungu.
Biblia Inasema
Mpingeni huyo mkiwa thabiti katika imani (1 Petro 5:9). Kwa kuwa andiko hili limesema hivi, Shetani hafurahii imani, maana kuwepo kwa imani zetu ni kupingwa kwake. Imani haimleti Mungu duniani tu! Bali inampinga Shetani, inamzuia kutenda kazi, inamwondoa duniani, si kwamba inamfanya asiwepo duniani, bali inamzuia, inamdhibiti.
Yuda aliandika, “Mwishindanie imani waliokabidhiwa watakatifu mara moja tu”(Yuda 1:3). Neno la Kiyunani lililotumika kuonnyesha kuishindania imani katika andiko hili ni “epagonizomai”, maana yake ni kushindana kinyume na wengine, ni kushindana na mafundisho ya uongo waliyofundisha wengine, yaliyokuwa kinyume na Injili ya Kristo au imani ya Kristo.
Hapa utagundua pia, Shetani anaharibu imani ya wokovu kwa kuleta mafundisho ya uongo.
Silaha Atumiazo
Silaha anazotumia kupinga imani ni 1. Mawazo ya uongo 2. Mazingira hasi 3. Maneno ya watu 4. Hisia za uongo 5. Mafundisho ya uongo 6. Muda, kuchelewesha kutimia kwa ahadi kwa kutumia nguvu za giza 7. Mwenendo usio sahihi, kuchochea matendo ya mwili. Vita vizuri vya imani tunavipiga maeneo hayo yote.
Imani inakaa moyoni na inao uhusiano na Mungu moja kwa moja. Shetani akitaka kuishambulia na kuiua anatumia mashaka. Mashaka ni kutokuwa na msimamo mmoja, kuwa pande mbili wakati mmoja. Njia ya kuleta mashaka ni kuuliza maswali kuhusu udhahiri au bayana ya Mungu na neno lake. Maswali haya kwa sehemu kubwa anayaleta katika mawazo.
Anaweza kutumia mazingira ya muda na kuuliza “mbona siku zinaenda na sioni matokeo? labda Mungu hajasikia” mawazo haya ya kujiuliza kuhusu Mungu au Neno lake huleta mashaka. Hapa Shetani hushambulia uhakika ili kuua uhakika, kwa kuleta wasiwasi katika udhahiri wako wa ndani, yaani Mungu na Neno lake.
Kama wewe ni binti hujaolewa na umemwamini Mungu, kwa kuwa imeandikwa mtu atamwacha baba na mama yake na kuambatana na mke wake. Jaribu la kwanza unaloweza kupata, Shetani atatumia muda kusema nawe katika mawazo. Utapata mawazo yasemayo “muda unaenda sasa nina miaka 33, ikifika miaka 40 kuna hatari nikashindwa kuzaa hata nikiolewa …….” Haya si mawazo yako tu ni mashaka yanayopandwa na Shetani, hupiga matumaini ili kuua imani. Anajaribu kuiua kwa kupiga matumaini na udhahiri wa ndani.
Mara nyingine, wakati mawazo hayo yanakujia anaweza kutokea mtu wa karibu na kusema, “Hee!unazidi kuzeeka tu! Utaolewa lini?” Hapa adui anamtumia mtu kuuwa matumaini. Mara nyingine baada tu ya mtu kumpa Yesu maisha yake, na kuwa na uhakika wa dhahiri ndani yake kuwa ameokoka. Mazingira ya nje hubadilika kabisa. Ataanza kupata mateso na kukataliwa. Baada ya hapo atakosa matumaini na mawazo kama haya yanamjia “afadhali nilivyokuwa sijaokoka”. Hapa Shetani anapiga tumaini lako ili kuua uhalisi wako wa ndani kuwa umeokoka. Mara nyingine wazo kama hili huja “Mungu si mkweli anasema nikimwamini Yesu nitaokoka, mbona sasa matatizo tu!” Hapa Shetani anapinga udhahiri wa Mungu na Neno lake kuua uhakika wa moyoni, kwa kumshitaki Mungu katika nafsi yako.
Akishindwa kukuangusha kwa kutumia dhiki, atatafuta kukuangusha imani yako kwa mafundisho ya uongo, ya kukupotosha. Kanisa la kwanza lilipata dhiki, baadaye ukaja upotefu wa imani.
Mbali na mawazo, njia nyingine atumiayo adui ni hisia. Hisia hapa nina maana ya; kuona, kugusa, kusikia, kunusa na kuonja. Unaweza kuomba jambo na kuliona moyoni kuwa na uhakika umelipokea kwa udhahiri wa Neno la Mungu. Vita itakayototea ni hii “Kiko wapi nilichoomba? mbona sijisikii ninacho?”. Hapa jambo la kufanya ni kuamini kwa njia ya kusema Neno linasemaje, na kutafakari unavyoona uhakika wa ndani. Baadaye hisia zitabadilika.
Jinsi mwenendo wetu ulivyo, au jinsi tunavyoishi haiwezi kutenganishwa na imani zetu. Jinsi Imani ilivyo kwa Yesu ndivyo jinsi tutakavyoenenda kitabia, tabia unayoishi sasa inaonyesha utakuwaje milele. Maandiko yanasemaje, “lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa injili ya Kristo …….” ( Wafilipi 1 : 27). Ndani ya injili kuna imani, “kwa maana haki ya Mungu inadhihirishwa ndani yake toka imani hata imani..…… “(Warumi 1 : 17). Kwa hiyo Paulo angeweza kusema “lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Imani ya Kristo” au “mwenendo wenu uwe kama yanavyopasa maisha ya Kristo”. Kuishi injili ya Kristo ni kuishi imani ya Kristo. Haya ni maisha ya Kristo. Shetani hushambulia eneo hilo la mwenendo wa Kristo katika maisha yetu. Kwa nini anafanya hivyo? Anajua jinsi unavyoenenda sasa,matendo tuendayo yanaambatana na sisi milele (Ufunuo 14:13). Mwenendo wa imani ya wokovu ni matendo ya upendo. Shetani atapinga tusiendende kwa Roho yaani Upendo ili imani zetu zisiwe na matunda.


No comments:

Post a Comment