Sunday, August 24, 2014

Vichocheo vya Imani na Tumaini



Mtu awashapo moto,  mfano awashapo jiko la mkaa ili uweke kwa haraka inampasa  auchochee kwa kuupuliza.
Vichocheo vya Imani
Kama vile moto huchechewa kwa upepo, Imani huchochewa kwa kufahamu moyoni.
Kufahamu  moyoni ya kwamba Mungu ni bayana na neno lake alilosema ni bayana. Hii huleta uhakika wa sasa kwamba kile alichosema anatenda hata kama sio dhahiri, yaani  hata kama hatuoni akitenda. Lakini ni dhahiri anatenda na yupo ingawa hatumuoni, kama mawimbi ya redio yalivyo  dhahiri na sauti za watu na nyimbo ingawa hatuyaoni!
Uhakika wa mambo tutarajiayo ambayo sasa tunayo kwa Mungu  na Neno lake unachochewa na ufahamu  atupao Roho Mtakatifu. Kuhusu Mungu na Neno lake. Imani hushika mambo yajayo sasa, katika Mungu na Neno lake moyoni.
Vichocheo vya Tumaini
Tumaini ni matarajio ya akilini kwamba mambo tuliopokea moyoni kwa imani yanaenda kudhihilika au kuonekana. Tumaini limefungwa na muda wa udhihirisho, imani haina muda, yote yameshatimia sasa kwa imani, Kama alivyo Mungu ni wa milele yote yametimia kwake. Tumaini huyangojea kwa wakati na majira yadhihirike. Tumaini limefungwa na muda. Kichocheo cha tumaini ni kuamini( pisteuo), ni kuitenda imani ya moyoni.  Ili tumaini lisife lazima kuifanyia kazi imani au kuitenda imani.
Imani inabeba tumaini au matarajio matumaini huzalishwa kwa kuamini, kusema neno, kutenda,  kushukuru huku ni kuitendea kazi imani.
Angalia Mifano Hii
Maandiko yanasema “Nanyi pia katika huyo mmekwisha kulisikia neno la kweli, habari njema za wokovu wenu:tena mmekwisha kumwamini yeye na kutiwa muhuri na Roho Yule wa ahadi aliye Mtakatifu  ndiye aliye arabuni ya urithi wetu  ili kuleta ukombozi wa milki yake,” (Waefeso 1: 13-14).
Katika andiko hili Roho wa Mungu anaonekana katika maisha yetu kama Muhuri na Arabuni. Mambo haya mawili yanachochea imani natumaini letu katika Kristo Yesu.
Muhuri
Katika Ufunuo 20:3, inaonyesha malaika alipomtia Shetani katika shimo la kuzimu, aliweka muhuri baada ya kulifunga, ili asipate kuwadanganya Mataifa tena. Kwa maneno mengine muhuri ulileta usalama, Mataifa wasidanganywe.
Katika Yohana 6:27, Maandiko yanasema, Yesu ametiwa muhuri na Baba. Tafsiri rahisi ni kwamba Yesu amethibitishwa na Baba. Muhuri huthibitisha.
Katika Waefeso 4:30, Roho Mtakatifu anaonekana kama Muhuri wa kuhifadhi. Maandiko haya yanasema kwa yeye tumetiwa muhuri hata siku ya ukombozi. Tumetengwa na muhuri huo hata ukombozi wa miili yetu utakapotokea. Pia muhuri ni ishara ya umiliki.  Watakaotiwa muhuri katika ufunuo 7:3-8, itakuwa ni ishara ya kwamba watamilikiwa na Mungu.
Kwa hiyo Roho Mtakatifu kama Muhuri katika maisha yetu ni ishara kwamba tupo salama milele, tumethibitishwa, tumehifadhiwa, tunamilikuwa na Mungu. Amefanyika Muhuri tulipozaliwa na yeye au tulipofanywa wana wa Mungu (Warumi 8: 15,  Yohana 3:6).
Kwa kufahamu Roho ni Muhuri, inachochea uhalisi wa wokovu ndani yetu sasa, hii  ni imani ya wokovu.  Pia inachochea matarajio ya kuingia Mbinguni, wakati ujao hili ni tumaini letu. Ikiwa utasema, utamshukuru Mungu na kuwaza haya, yaani Roho ni Muhuri wako, imani yako na umaini la wokovu litakuwa imara.
Arabuni
Arabuni maana yake ni malipo ya kwanza “deposit” (2 Wakorintho 1:22, 5:5). Tulipofanywa wana baadaya kumwamini Yesu, Roho Mtakatifu alifanyika malipo ya kwanza na ukombozi wetu wa milele. Bado hatujamwona Baba, bado hujaona mbinguni, bado hatujaona urithi wetu wote ulio mkubwa mbinguni. Pamoja na hayo Mungu ametuonyesha kwa kutupa Arabuni ya Roho. Huyu ni kama kishika uchumba anaethibitisha siku moja, ndoa itafanyika na Yesu mbinguni.  Yeye ni uthibisho kwamba sisi ni mali ya Mungu ameshatulupia sehemu ya kwanza.  Sehemu ya pili tutaipata katika umilele mbinguni, ya kwanza ni Arabuni ya Roho duniani.
Ni sawa na mtu alieenda dukani kununua kiatu cha elfu hamsini. Anaweza kutoa elfu ishirini kama arabuni na baadaye akalipa elfu thelathini. Elfu ishirini aliyotoa itathibitisha kiatu kile ni mali yake na majira timilifu yakija atakichukua. Ndivyo alivyofanya Baba. Ametupa Roho kuonyesha sisi ni milki yake ni mali yake, siku moja atatumiliki milele mbinguni.
Kufahamu ukweli huu inachochea uhalisi au uhakika wa wokovu wetu sasa. Pia inajenga matumaini makuu ya kuishi na Mungu, wakati ujao. Tunaposema, tunaposhukuru, tunapotafakari au tunapotendea kazi Imani yetu matunaini ya udhihilisho wa kuingia Mbinguni  yanakuwa hai na tunampendeza Mungu tunajitakasa kwa kuwa sisi  si wa dunia hii (1Yohana3:1-3).  Tumaini la wokovu wa milele likiwepo, utakatifu huja. Pasipokuwa na matumaini watu hutenda dhambi, maana hakuna wanachotarajia mbele. Kwa hiyo katika vita vya kiroho Shetani hupiga matumaini vita, ili watu wasiwe watakatifu. Maandiko yanasema “Wapenzi, sasa tu wana  wa Mungu, wala haijadhihilika bado tutakavyokuwa; lakini twajua ya kuwa atakapodhihilishwa, tutafanana naye; kwa maana tutamwona kama alivyo. Na kila mwenye matumaini haya katika yeye hujitakasa kama yeye alivyo mtakatifu. “(1 Yohana 3 : 2-3).  Huwezi kujitakasa usipojua tumaini lako. Tumaini haliwi hai usipoamini. Pia huwezi kuamini bila imani au uhalisi wa ndani. Hamna uhalisi wa moyoni bila udhahiri  bayana wa Mungu na Neno lake. Kumfahamu Roho kama Arabuni kwa Neno la Mungu, inachochea Imani, kuamini, matumaini na utakatifu.

No comments:

Post a Comment