Tuesday, August 19, 2014

Mwili wa Yesu na Agano


Yesu Alikuja Katika Mwili na Damu
Yesu alikuja kufidia maisha ya wanadamu. Mwanadamu alikuwa na madeni ambayo hayakuweza kulipwa na Agano la kwanza. Hakuweza kuachiliwa toka katika utumwa wa dhambi, utumwa wa shetani na mauti. Ili aachiliwe ilipasa maisha yake yafidiwe na sadaka ya maisha ya mtu mwingine.

Kuwepo kwa Yesu duniani ni fidia ya mwanadamu. Sio kwa njia ya kufa na kufufuka tu, bali kwa maisha yake yote ambayo yalihitimishwa kwa kifo na ufufuo wake. Ikiwa alijaribiwa na kushinda ni kwaajili yetu ili tushinde, ikiwa alikuwa maskini ni kwaajili yetu tutoshelezwe, ikiwa alidhihakiwa ni kwaajili yetu tuheshimiwe. Ikiwa alikufa ni kwaajili yetu tusamehewe dhambi, ikiwa alifufuka ni kwaajili yetu tuhesabiwe haki yenye uzima wa milele kwa njia ya kumwamini. Kwa njia ya kuwa fidia ya wanadamu alianzisha Agano jipya. “Kwa maana Mwana wa Adamu naye hakuja kutumikiwa, bali kutumika na kutoa nafsi yake iwe fidia ya wengi.” (Marko 10:45). Mwili na damu yake vinaonyesha fidia hiyo na ukombozi.
Wokovu Katika Mwili na Damu Yake
Kwa njia ya mwili na damu yake Yesu alianzisha Agano na wanadamu. Kupitia mwili huo pia alimharibu adui wa mwanadamu yaani Shetani.
Mwili
Kwa Mwili wake Alimshinda Shetani
Wanadamu wana mwili wa damu na nyama na kwa huo Shetani aliwashinda. Yesu naye alishiriki mwili wa damu na nyama ili kwa njia ya huo na kupitia huo aweze kumharibu Shetani. Asingeweza kumharibu bila mwili kwa kuwa Shetani alipata nafasi kutawala dunia na mwanadamu kupitia mwili alipowadanganya Eva na Adamu waliokuwa katika mwili. Yesu alimshinda katika mwili na kumnyang’anya mamlaka na nguvu zake juu ya wanadamu. Majaribu yote aliyowajaribu Adamu na Eva na kuwashinda Yesu aliyashinda. Kisha kwa njia ya mwili alikufa msalabani na kumnyang’anya Shetani silaha zote kupitia mwili wake (Wakolosai 2:14). Alipofufuka alirejesha kwa njia ya mwili wake mamlaka yote Adamu aliyopoteza (Waebrania 2:14). Wakati tunaposhiriki mkate katika meza ya Bwana tukiri mambo haya ambayo Yesu aliyafanya kwa Shetani kwa njia ya mwili wake, kwaajili ya maisha yetu.
Alimharibu Shetani
Kazi zote za Shetani yaani dhambi, magonjwa na mauti viliharibiwa kwa njia ya mwili wa Yesu (1Yohana 3:7-8). Tunaposhiriki mwili wa Yesu katika meza ya Bwana tukiri na kusema katika agano jipya Yesu alidhihirishwa azivunje kazi zote za Ibilisi katika maisha Yetu kupitia mwili wake.
Alijaribiwa katika Mwili
Yesu katika mwili wake alijaribiwa katika hali na mambo yote bila kufanya dhambi (Waebrania 4:15). Katika mwili wa damu na nyama alishinda majaribu yote. Tunapoushiriki mwili wake katika mweza ya Bwana tukiri na kusema katika hali zote tunazojaribiwa tunayo neema ya kushinda dhambi toka mwili wa Yesu, uliotolewa katika Agano jipya. 
Alikuwa Maskini katika Mwili
Katika mwili Yesu alifanyika maskini kwa neema yake ingawa alikuwa tajiri. Alifanyika maskini ili sisi tuwe matajiri kwa umaskini wake (2Wakorintho 8:8-9). Tunapoushiriki mwili wa Yesu katika meza ya Bwana, tukiri kwamba tunatajirishwa katika neema yake ili tuweze kuipeleka injili. Yeye ni mchungaji wetu hatutapungukiwa na kitu. Umaskini haumtukuzi Mungu. Utajiri na kupata mahitaji yetu ya kila siku humtukuza Mungu, ikiwa tumepata ndani ya Yesu. 
Alifanyika laana Katika Mwili
Yesu alifanyika laana ya torati ili baraka ya Ibrahimuiwe juu yetu. Laana ni uharibifu utendao kazi kwa siri kwasababu ya kanuni fulani ya kiroho kuvunjwa. Laana ya torati ilitokana na kuvunjwa kwa torati, hivyo matokeo ya kuivunja na kutokuitenda yalileta uharibifu kwa aliyevunja (Soma Kumbukumbu 28). Yesu alikuja kuifia torati na mashitaka yake yote kwa mwanadamu iliyoleta pamoja na laana. Baada ya hapo akafungulia mlango wa kubarikiwa kama Ibrahimu alivyobarikiwa (Wagalatia 3:12-4). Ibrahimu alihesabiwa haki baada ya kuamini (Mwanzo 15:6), sasa katika Yesu tunahesabiwa haki kwa kumwamini Yesu sio kwa kuitii Torati. Ibrahimu aliweza kuongezeka, kuwa na kibali na kushinda maadui. Kwa mfano wa Ibrahimu sasa tunaishi katika Yesu Kristo. Tunaposhiriki meza ya Bwana tukiri kwamba uharibifu wa namna yoyote katika maisha yetu uliondolewa katika mwili wa Yesu. Ikiwa kuna dhambi tunaijua tutubu na kusema Yesu alifanyika laana katika mwili ili turithi baraka za Ibrahimu.
Kufanyika dhambi Katika mwili
Yesu hakuwa na dhambi. Sheria ya kiroho inahitaji mtu akitenda dhambi anastahili kufa. Kwa kuwa yeye hakutenda dhambi na akahukumiwa kifo, ilipasa afanyike dhambi zetu ili afe kwa halali. Yesu alifanyika dhambi zetu  katika mwili na kuzifia. Kwasababu hiyo sisi ni haki ya Mungu katika yeye. Tunapomwamini tunakuwa hatuna hatia ya dhambi tena katika yeye. Ikitokea tunatenda dhambi tunatubu na kuitegemea neema yake kutusaidia kutotenda dhambi. Mungu alitoa sadaka ya Yesu msalabani ili afanyike dhambi na kwa yeye tushinde dhambi kwa neema. Unapompa Yesu maisha yako inakupasa kutegemea kutenda haki zaidi kuliko kutegemea kwamba utatenda dhambi. Ni kweli huwa inatokea mtu anatenda dhambi lakini sio lazom atende baada ya kumpa Yesu maisha.
Baada ya kuzaliwa mara ya pili Biblia inatuagiza tujihesabu kuwa wafu katika dhambi, “Maana kwa kule kufa kwake, aliifia dhambi mara moja tu; lakini kwa kule kuishi kwake, amwishia Mungu. Vivyo hivyo ninyi nanyi jihesabuni kuwa wafu kwa dhambi, na walio hai kwa Mungu katika Kristo Yesu.”(Warumi 6:10-11) Kujihesabu kama wafu wa dhambi ni kujiona katika Yesu hatuna dhambi na kujisema hivyo. Hii itatupa neema ya kuzidi kubadilika na kutotenda dhambi. Tunatubu dhambi na kujihesabu tumekufa katika dhambi. Sio kutubu peke yake. Vitu hivi vinapaswa viende pamoja ili tuishinde dhambi tuliyoitubu. Katika meza ya Bwana inatupasa tutamke kwamba kwa njia ya mwili wa Yesu tumeshinda dhambi na hatuna dhambi kwa neema tumehesabiwa haki.





No comments:

Post a Comment