Monday, August 18, 2014

Agano la Uzima


ZOE

Agano jipya ni agano la uzima wa milele. Yesu alikuja kuanzisha Agano jipya lenye uzima wa milele, tofauti na lile la kale ambalo mauti ilikuwa na nguvu kwa waabuduo. Katika hili la pili mauti haina nguvu mauti imeshindwa kwa uzima wa milele ulio ndani ya Kristo aliye ndani ya waaminio.

Neno la Kiyunani ambalo linamaanisha uzima wa milele ni “Zoe”. Maana yake ya msingi ni asili ya Mungu. Ni uungu utokao kwa Mungu unaoweza kumbadilisha mtu aishi kama Mungu.

Mungu ni chanzo cha uzima wa milele, “Kama vile Baba alivyo na uzima ndani yake vivyo hivyo amempa Mwana kuwa na uzima ndani yake.” (Yohana 5:26). Katika uzima wa milele kunatoka chemichemi ya Mungu yenye Upendo, imani, mamlaka, hekima, amani, furaha, utuwema, karama, uponyaji, afya, baraka na mambo mengine ya Mungu. Uzima wa milele ndani ya mtu unamwezesha kutawala kama Mungu, kwa chemichemi yenye uzima iliyo na mambo ya kimugu. Kwa njia ya uzima wa milele tumeketishwa mkono wa kuume wa Mungu pamoja na Kristo, sisi sio wa chini sisi ni wa juu. Yesu alisema, “…Ninyi ni wa chini, mimi ni wa juu…mimi si wa ulimwengu huu.” (Yohana 6:23). Kwa kuwa Yesu sio wa duniani ni wa mbinguni sisi tuliomwamini pia ni wa juu maana alipofufuka tuliketishwa naye juu (Waefeso 2:1-6).

Shetani yupo duniani sisi katika Kristo tupo juu yake, maana tupo mbinguni alipo Mungu. Tunamtawala kutoka mkono wa kuume, sio kutoka duniani. Tunamtawala kutoka hapo kwa jina la Yesu na Neno la Mungu. Tumewekwa mkono wa kuume kwa njia ya uzima wa milele ndani yetu katika Kristo Yesu.

Adamu alipokosea mauti, yaani asili ya Shetani iliwatawala watu wote maana wote walitenda dhambi ndani ya Adamu. Kupitia Adamu wote tulitawaliwa na mauti. Sasa kwa njia ya Yesu aliyefanyika dhambi za Adamu na kuzifia msalabani, tunapata neema na kipawa cha kuhesabiwa haki bila matendo. Kwa njia ya Yesu sisi sio wa mauti tena! Tunatawala katika uzima ndani ya Yesu. Mauti, Shetani, dhambi na kila kitu kiovu kipo chini yetu kwa uzima wa Yesu uliopo ndani yetu. “Kwa maana ikiwa kutokana na kosa la mtu mmoja, mauti ilitawala kupitia huyo mtu mmoja, zaidi sana wale wanaopokea wingi wa neema ya Mungu na karama yake ya kuhesabiwa haki, watatawala katika uzima kwa njia ya huyo mtu mmoja, Yesu Kristo.” (Warumi 5:17).

Yesu Chanzo cha Uzima Ndani ya Watu
Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msipoula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa damu yake, hamna uzima ndani yenu. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu anao uzima wa milele; nami nitamfufua siku ya mwisho. Kwamaana mwili wangu ni chakula cha kweli na damu yangu ni kinywaji cha kweli. Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu, nami hukaa ndani yake. Hiki ndicho chakula kishukacho kutoka mbinguni; si kama mababa walivyokula, wakafa; bali akilaye chakula hicho ataishi milele.” (Yohana 6:53-58). Chanzo cha uzima wa milele wa Mungu kwa wanadamu ni kupitia mwili na damu ya Yesu. Mwili wake ulizibeba dhambi juu ya msalaba, damu yake iliziondoa. Yesu alifanyika dhambi katika mwili wake na kuisulubisha katika mwili ili isiwe na nguvu ya kututawala.

Alitoa damu katika mwili wake ili kuiondoa na kuyasafisha maisha yetu toka katika dhambi. Kwa njia ya kuamini kazi ya damu na mwili wake tunapata uzima, “Amin, amin, nawaambia, Yeye aaminiye yuna uzima wa milele.” (Yohana 6:47).

No comments:

Post a Comment