Tuesday, August 12, 2014

Maombi ya Utimilifu 4



Utimilfu katika Karama za Roho

Kazi ya Roho Mtakatifu ni kumshuhudia Yesu Kristo kupitia Kanisa.  Roho hutumia vipawa na karama ili kufanya kazi hiyo.  Kanisa pasipo karama za Roho ni sawa na simba anayetisha, lakini hana makucha makali wala meno!  Simba huyu anatisha kwa nje tu lakini kiutendaji hawezi kushika mnyama yoyote.

Kazi ya kupeleka Injili kwa waliopotea haiwezi kufanikiwa katika utimilifu wake wote pasipo Uweza wa Roho na karama zake.  Mara nyingine wafuasi wa Yesu wanaonekana kudharau karama za Roho husema; “Neno la Mungu ndilo linalohitajika zaidi ya karama”.  Hii si kweli maana Neno la Mungu na karama hufanya kazi pamoja.   Hatuwezi kuhubiri Injili kwa watu walio maporini ambao hawajamjua na kumsikia Yesu, pasipo ishara na miujiza ya Roho Mtakatifu.  Wengi wa watu hawa wana miungu yao, ili wageuke na kumwamini Mungu wetu inahitajika “ishara, dalili za Roho Mtakatifu na Nguvu”.

Utimilifu wa Uweza Katika Injili

Hii ndio sababu kuna umuhimu wa kuhubiri katika utimilifu wa Karama za Roho.  Paulo aliandika, “kwa nguvu za ishara na maajabu, katika nguvu za Roho Mtakatifu; hata ikiwa tangu Yerusalemu, na kandokando yake, mpaka Iliriko nimekwisha kuihubiri Injili ya Kristo kwa Utimilifu” (Warumi 15:19).  Utimilifu wa Injili aliohubiri Paulo uliendana na udhiirisho wa karama za Roho yaani Nguvu za Mungu.

Maandiko yanasema, “Ufuateni upendo na kutaka sana karama za rohoni…Vivyo hivyo na ninyi , kwa kuwa mnatamani sana kuwa watu wenye karama za roho, takeni kwamba mzidi sana kuwa nazo ili kulijenga kanisa” (1 Wakorintho 14:1, 12) .  Hapa tunagundua kwamba udhihirisho wa karama za Roho Mtakatifu unaendana na sisi kuwa na shauku ajidhihirishe.  Hatuwezi kuchagua karama bali Yeye hutugawia kama atakavyo. Kitu tunachoweza kufanya ni kutaka Roho Mtakatifu atutumie kwa karama yoyote ambayo anataka ifanye kazi kupitia sisi. 

Kutaka kitu hutuwezesha kukiomba. Yesu alisema, “…Yoyote myaombayo mkisali, aminini ya kwamba mnayapokea, nayo yatakuwa yenu.” (Marko 11:24).  Katika tafsiri mojawapo ya Kiingereza andiko hili linasema, “Yoyote myatakayo, mnapoomba, aminini ya kwamba mnayapokea”.  Andiko lingine linasema, ”...ombeni mtakalo lote nanyi mtatendewa(Yohana 15:7).  Maneno yaliyotumika hapa, yaani; yatakuwa yenu, mnayapokea, na mtatendewa, yanaonyesha ya kuwa kitu atakacho mtu katika mapenzi ya Mungu akiomba atakipata.  Kwa hiyo ikiwa unataka udhihirisho wa karama za Roho katika Kanisa, watumishi wa Mungu, au katika maisha yako, unaweza kuomba.  Omba ili Kanisa lijengwe na Injili ihubiriwe katika utimilifu wa nguvu za Mungu, yaani karama za Roho Mtakatifu.  Ukiomba kwa jinsi hii utakuwa umeomba kama kanisa la kwanza. Kanisa hili lilitaka na kuomba udhihirisho wa Mungu kwa karama zake, walimwomba Mungu kwa kusema, “…ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ishara na maajabu vifanyike kwa jina la Mtumishi wako mtakatifu Yesu.” (Matendo 4:29-30).

Tusiogope karama za Roho, bali tutafute kuzifahamu na kuzielewa.  Karama kama vile unabii, kunena kwa lugha, kutafsiri lugha, neno la hekima, neno la maarifa, kupambanua roho, Imani maalum, karama za uponyaji, na miujiza zipo ndani ya kanisa katika Roho Mtakatifu.  Tusipotaka udhihirisho wa karama hizi na kuomba udhihirisho huo, hatutaweza kufanya kazi ya Mungu kwa utimilifu.  Hivyo ni vema  kuanza kufanya maombi na maombezi ya utimilifu wa nguvu za Mungu katika kazi ya Injili.  

Muombe Mungu aandae watendakazi watakao taka kutenda kazi katika nguvu na karama za Roho, jiombee na wewe, kisha waombe wote walio shambani mwa Bwana waweze kufanya kazi kwa utimilifu katika Nguvu za Roho Mtakatifu.  Ombea maeneo yasiyofikiwa na Injili kwa upana kama vile Lindi, Mtwara, Singida, Zanzibar, Shinyanga, Mbozi, Kyela na mengineyo.  Waombee wamishionari wanaofikia; Wasonjo, Wahadzabe, Wamang’ati na makabila mengine, kufanya kazi hiyo kwa utimilifu wa nguvu za Roho.  Ombea wamishionari waliopo Sudani, Msumbiji, Namibia, Angola, China, Indonesia na nchi nyingine, Bwana awalinde na kuwaokoa, awajalie kuhubiri Injili ya Uweza.  Omba milango ya Injili ya utimilifu ifunguke Irani, Pakistani, Afghanistani, Somalia, Libya, Morocco, Algeria, na kwingineko, Bwana aangushe ngome zote katika fikra zinazopinga Injili, ili Injili ya Uweza ihubiriwe kwa utimilifu wote.

Pia mshukuru Mungu kwa makanisa ya Tanzania yaliyo na Mzigo wa kupeleka Injili kwa wasiofikiwa.  Tuombe Mungu ainue mifuko ya kimisheni makanisani kwaajili ya kuwapelekea Injili  wasiofikiwa.

No comments:

Post a Comment