Utimilifu
Katika Kutenda Mema
Wakati fulani nilipewa maneno yafuatayo moyoni
mwangu, “Iweni na juhudi katika kutenda mema, maana wakati wenu ni
mchache”. Kwa maneno haya nilipata
msisitizo kwamba kutenda mema ni jambo la muhimu sana tunapokuwa hai.
Paulo aliwaombea Wakorintho wasitende mabaya alisema,
“Nasi twamwomba Mungu, msifanye lolote lililo baya…” (2 Wakorintho 13:7). Bila shaka Mungu alijibu maombi haya kwa
kuwapa neema Wakorintho ya kutotenda mabaya kwa msaada wa Roho wake.
Kutenda Mema na Neno la Mungu
Mungu hutuwezesha kutenda mema kwa
njia ya Roho Mtakatifu katika Neno lake.
Roho wa Mungu huyahuisha maandiko ndani yetu na hivyo yakawa ni Maneno
ya Mungu yenye pumzi yake. Neno la Mungu
katika Roho Mtakatifu linaweza kumkamilisha mtu katika kila tendo jema. Jinsi unavyokuwa na bidii ya kulijua Neno na
kupata ufahamu wa Roho kupitia Neno, ndipo unapozidi kukamilika katika kutenda
mema. Unaposikiliza Neno, omba uweze kulielewa na kujua linakuonya kitu gani,
linakuongoza ufanye nini, na linakuandaaje kutenda haki.
Ukijizoeza kufanya hivi matendo mema yatakuwa ni
sehemu ya maisha yako, kwa nguvu ya Neno la Mungu lililo hai. Maandiko yanasema, “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa kwa mafundisho, na kwa
kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki;
ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa
apate kutenda kila tendo jema”
(2 Timitheo 3:16-17). Hivyo fanya maombi kwaajili yako na maombezi kwa wengine wakamilishwe katika kutenda mema kwa njia ya kukutana na Neno lenye pumzi ya Mungu. Uwaombee watu wote unaowafahamu ambao husema Neno; yaani wanaofundisha, wanaohubiri nk. Omba waweze kusema Neno lenye pumzi ya Mungu, liwezalo kuwabadidilisha wanaosikia na kuwafanya wakamilike katika kutenda mema.
(2 Timitheo 3:16-17). Hivyo fanya maombi kwaajili yako na maombezi kwa wengine wakamilishwe katika kutenda mema kwa njia ya kukutana na Neno lenye pumzi ya Mungu. Uwaombee watu wote unaowafahamu ambao husema Neno; yaani wanaofundisha, wanaohubiri nk. Omba waweze kusema Neno lenye pumzi ya Mungu, liwezalo kuwabadidilisha wanaosikia na kuwafanya wakamilike katika kutenda mema.
Matendo Mema ni Nuru
Utimilifu katika kutenda mema unatukamilisha katika
kazi yetu ya kuwa nuru ya ulimwengu.
Sisi kama watu wenye Nuru (Yesu) twaangaza duniani kwa matendo mema ya
Yesu akaaye ndani yetu. Matendo mema ni nuru.
Maandiko yanasema, “Ninyi ni nuru
ya Ulimwengu. Mji hauwezi kusitirika
ukiwa juu ya mlima. Wala watu hawawashi
taa na kuiweka chini ya pishi, bali juu ya kiango; nayo yawaangaza wote waliomo
nyumbani. Vivyo hivyo nuru yenu na
iangaze mbele za watu, wapate kuyaona matendo yenu mema, wamtukuze Baba yenu
aliye mbinguni.” (Mathayo 5:14-16).
Wakati wote nuru ing’aapo giza haliwezi kushinda, ”Nayo
nuru yang’aa gizani, wala giza halikuiweza”(Yohana 1:5). Ubaya (giza)
hauwezi kushinda tutendapo mema(nuru). Hii ndio maana Biblia inatuagiza, kwa kusema,
”usishindwe na ubaya(giza), bali uushinde ubaya kwa wema(nuru).”
(Warumi 12:21). Kuombea utimilifu katika
kutenda mema kutatuwezesha kuangaza kwa matendo hayo, hatimaye watu
watamwinua/watamtukuza Mungu, wayaonapo matendo yetu mema.
Kutenda Mema ni Mbegu
Kama mkulima asivyochoka kupanda mbegu, kwa kuwa
anatarajia mavuno kwa wakati wake ndivyo itupasavyo kufanya. Matendo mema kwa wanaotuudhi, walioamini
na watu wote ni mbegu, maandiko
yanasema, “Tena tusichoke katika kutenda
mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho. Kwahiyo kadiri tupatavyo nafasi na tuwatendee watu wote mema; na hasa jamaa ya waaminio.” (Wagalatia
6:9-10). Utendapo mema kwa wanadamu
Bwana atayahifadhi matendo hayo mbele zake kama mbegu na kukupa mavuno. Kornelio alitenda mema na Mungu akayahifadhi
matendo yake kama mbegu, baadae alimpa mavuno, yaani malaika kumtokea na kusema
naye
(Matendo 10:1-8).
(Matendo 10:1-8).
Upandapo mema
utavuna mema, maombi ya utimilifu katika kutenda mema yatakuwezesha kupanda
mema. Unapomgawia mwenye njaa chakula,
aliye uchi mavazi na kufanya maombezi, Bwana hatasahau matendo hayo mema,
atakulipa kama yasemavyo maandiko, “mkijua
ya kuwa kila neno jema alitendalo
mtu atapewa lilohilo na Bwana…” (Waefeso 6:8).
Kufanywa
Imara Katika Kutenda Mema
Mungu
hutoa neema ya kutotenda mabaya kwa njia ya kumfanya mtu imara
katika kila neno na tendo jema, “…Mungu
Baba…awafariji mioyo yenu, na kuwafanya imara
katika kila neno na tendo jema”
(2
Wathesalonilke 2:16-17). Kutenda mema wakati unafanyiwa mabaya si kitu rahisi,
kumsema mtu vizuri au kumfanyia kitu kizuri wakati yeye anakufanyia kitu kibaya
si jambo rahisi kwa mtu wa kawaida. Maandiko
yanasema, “…Wapendeni adui zenu, watendeeni mema wale ambao wawachukia
ninyi…msimlipe mtu ovu kwa ovu. Angalieni yaliyo
mema machoni pa watu wote…Maana huu ndio wema hasa mtu akivumilia
huzuni kwa kumkumbuka Mungu, pale ateswapo isivyo haki” (Luka 6:27, Warumi 12:17).
Mtu
yoyote aliye na Yesu yampasa kuwatendea mema watu wote wabaya kwa wema. Ili kuweza kutenda mema kwa watu wote wakiwemo
wanaokuchukia inakupasa uwe imara kiroho,
maana si jambo rahisi. Ili kutenda tendo
jema kama vile kumuombea, kumvisha, kumsalimu,
au kumpa zawadi mtu, yakupasa uwe umetiwa nguvu katika Roho Mtakatifu kuyatenda
hayo.
Ili kufanywa imara na kutimilika katika kutenda mema kwa watu
wote, yakupasa uombe Mungu akusaidie na uwaombee wengine pia. Ni vizuri kuwaombea watumishi wa Mungu au
washirika katika kanisa lako, wasifanye
lolote lililo baya. Kisha unaweza
kuendelea kuwaombea wafanywe imara au
watiwe nguvu katika kutenda mema.
Ukifanya hivi utakuwa unawasaidia kufanana kitabia na Yesu ambaye,“… alipotukanwa, hakurudisha matukano;
alipoteswa hakuogofya…” (1 Petro 2:23).
Inawezekana
kuwa umekutana na mtu asemaye kulipiza
kisasi ni sawa au haiwezekani kusamehe.
Mtu wa namna hii yampasa aombewe utimilifu katika kutenda mema kwa njia
ya kufanywa imara katika kutenda mema, yaani afanywe imara ili aweze kusamehe
au kutolipiza kisasi.
Kutenda
Mema na Hekima
Kutenda mema kuna uhusiano wa karibu na hekima ya
Mungu. Mtu mwenye hekima hufanya mambo
mazuri hutenda mema na ana matunda mema. Maandiko yanasema, “N’nani
aliye na hekima na ufahamu kwenu? Na aonyeshe kazi zake kwa mwenendo wake mzuri, katika upole wa hekima…Lakini
hekima itokayo juu kwanza ni safi,
tena ni ya amani, ya upole, tayari kusikiliza maneno ya watu, imejaa rehema na matunda mema, haina fitina, haina
unafiki.” (Yakobo 3:13,17). Mambo
yaliyotajwa hapa ni matendo ya hekima itokayo juu, haya ni matendo mema. Kuwa na amani na watu ni tendo jema la
hekima, kuwa mpole/kutolipiza kisasi ni tendo jema la hekima, kusikiliza watu,
kutokuwa mnafiki, kutofitini haya yote ni matendo mema ya hekima.
Ikiwa
tumepungukiwa matendo haya inawezekana tumepungukiwa na hekima ya Mungu itokayo
juu, maana inayo matendo hayo mema. Kama tumepungukiwa na hekima twaweza kuomba, “Lakini mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima,
na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.”
(Yakobo 1:5).
Namna
nyingine ya kuombea utimilifu katika kutenda mema ni kuomba hekima ya Mungu
iongezeke katika maisha yetu, katika Kanisa na watumishi wa Mungu. Hekima ya Mungu mioyoni mwetu itatuelekeza
jinsi ya kufanya au kusema pale tunapokutana na mazingira yanayoweza
kusababisha tutende mabaya. Hekima hii
itatuokoa kwa kutupa njia au mlango maalum wa kutenda mema, mahali ambapo kwa
hali ya kawaida tungetenda mabaya. Kwa mfano, wakati wa kulaumu au kukasirika
hekima itatufundisha katika mioyo kutokasirika.
Usiache
wala kuchoka kuombea utimilifu katika kutenda mema, kwa njia ya kuombea
ongezeko la hekima ya Mungu ndani ya Mwili wa Kristo/Kanisa.
No comments:
Post a Comment