Sunday, August 10, 2014

Maombi ya Utimilifu 2



Utimilifu Katika Mapenzi ya Mungu

Mapenzi ya Mungu ni utashi wake, ni namna anavyotaka tuishi.  Bila kutimilika katika kuyafanya mapenzi yake hakuna mtu awezaye kumwona,  si kila mtu aniambiaye Bwana, Bwana, atakayeingia katika ufalme wa mbinguni; bali ni yeye afanyaye mapenzi ya Baba yangu aliye mbinguni” (Mathayo 7:21).   Hivyo kufanya mapenzi ya Mungu ni kitu cha muhimu sana kwa watu wake, wanaotarajia kumuona.
Maombezi Wasipungue katika Kumpendeza
Mapenzi ya Mungu twaweza kuyafanya kwa njia ya kuwezeshwa na neema yake.  Neema hii ipo ndani ya Neno lake ambalo ni mapenzi yake (Mathayo 12:50, Luka 8:21). Kitu kingine kinachoweza kutusaidia kufanya mapenzi yake ni maombi na maombezi ya utimilifu katika kuyafanya.  Katika baadhi ya maandiko yaliyopita tulimwona Epafra akiwaombea Wakolosai kwa bidii ili wasimame wakamilifu na kuthibitika sana katika mapenzi yote ya Mungu.  Hapa aliwaombea wasipungue katika kumpendeza Mungu.
Kupingana Nguvu za Giza
Tarehe 12.6.2006, wakati ninaomba asubuhi, ndani yangu nilipata ufahamu ya kwamba kuna aina ya pepo na wakuu wa giza ambao wanapinga na kujaribu kuzuia maandeleo ya mtu kukua kiroho na kufanya mapenzi ya Mungu.  Pepo hawa humfuatilia kila mtu aliyempa Yesu maisha yake, hata kujaribu kumzuia asisonge mbele kwa njia ya kuleta hali mbalimbali za kumpinga.  Hali hizi ni kama vile, kumpa mawazo ya kutosoma Biblia, kutoenda katika ibada au kuchochea utendaji wa utu wa kale kwa njia ya kuleta mawazo machafu.

Inawezekana kabisa Paulo alipoandika, “Lakini nachelea; kama yule nyoka alivyomdanganya Hawa kwa hila yake, asije akawaharibu fikra zenu, mkauacha unyofu na usafi kwa Kristo” (2Wakorintho 11:3), moyoni mwake alijua ya kuwa Shetani, wakuu wa giza na mapepo wanafuatilia watu walio okoka.  Sababu ya Shetani kufanya hivyo ni ili waache unyofu na usafi, yaani wasimpendeze Mungu.

Bila shaka Epafra alipowaombea Wakolosai kwa bidii na kwa kushindana alikuwa anapambana na pepo waliojaribu kuwazuia wasikue kiroho na kufanya mapenzi ya Mungu.  Paulo alipoandika, “Kwa maana kushindana kwetu sisi si juu ya damu na nyama bali ni juu ya falme na mamlaka, juu ya wakuu wa giza hili, juu ya jeshi la pepo wabaya katika ulimwengu wa roho.”(Waefeso 6:12).   Alitumia  neno “kushindana” lililofanana na jinsi alivyoomba Epafra, yaani kuomba kwa bidii. Hivyo twaweza kusema, Epafra alipoomba kwa bidii ili wathibitike katika mapenzi yote ya Mungu kwa sehemu alikuwa anashindana na nguvu za giza zilizojaribu kuwazuia kufanya ayatakayo Mungu.  Nguvu hizi ni zilezile ambazo Yesu alizishinda kwaajili yetu na kuzifanya si kitu (Wakolosai 2:15).  Wakuu hawa wa giza na mapepo hawawezi kutenda lolote wakikutana na mamlaka ya Yesu kupitia mtu afanyaye maombezi kwa jina la Yesu.  Kwa hiyo Epafra aliposhindana nazo alikuwa upande wa ushindi kwa kuwa alikuwa na Jina hilo akiwa ndani ya Kristo Yesu aliyeshinda.

Maombi ya Kujua Mapenzi ya Mungu

Paulo aliwaandikia Warumi maneno yafuatayo, “Wala msiifuatishe namna ya dunia hii; bali mgeuzwe kwa kufanywa upya nia zenu, mpate kujua hakika mapenzi ya Mungu yaliyo mema, ya kumpendeza, na ukamilifu.” (Warumi 12:2).  Mapenzi ya Mungu ni mema na ukamilifu.  Kuyajua kunaweza kukuwezesha kuyatenda na kuwa mkamilifu.  Baada ya nia (fikra/mawazo) kufanywa upya kwa Neno la Mungu, utaweza kuyajua mapenzi ya Mungu kwa upana na kuzidi kukamilishwa.  Paulo aliwaombea Waefeso macho ya mioyo (roho,fikra, mawazo, nia) yatiwe nuru ili wajue (Waefeso 1:18).  Wewe pia endelea, kujiombea, kuombea watumishi, na kuliombea Kanisa liendelee kuyajua mapenzi ya Mungu kwa kutiwa nuru katika nia. Matokeo yatakuwa kulijua Neno la Mungu, kufanywa upya, na hatimaye kuweza kulitenda. Hali hii italiwezesha Kanisa kufikia utimilifu wa kufanana na Yesu katika kutenda mapenzi ya Mungu.  Usichoke kufanya maombi haya, muombe Mungu akuwezeshe kutenda mapenzi yake yote. Mueleze ya kuwa  kwa nguvu zako huwezi lakini kwa neema yake inawezekana.  Baada ya hapo ombea Kanisa taja mtu unayeweza kumkumbuka, ili aweze kuthibitika katika mapenzi ya Mungu.  Kisha ombea watumishi wa Mungu wale unaowajua na usiowajua waweze kuthibitika katika mapenzi yote ya Mungu.

Ikiwa wewe ni Mchungaji wa kweli, Mwinjilisti wa kweli, Mwalimu wa kweli, Nabii wa kweli, Mtume wa kweli, Mwombezi au kiongozi yoyote ambaye watu wanakutegemea. Usiache kuwaombea watimilike katika kuyafanya mapenzi ya Mungu.  Matunda ya kazi yako kwao yanategemeana sana na mwisho wao, ambao pia unategemea ni jinsi gani walimpendeza Mungu.












No comments:

Post a Comment