Tuesday, August 26, 2014

Fahamu Unao Ufalme

Fahamu Unao Ufalme
Mungu anatawala kwa mamlaka yake na nguvu. Ufalme wake ulipo, nguvu zake, utukufu wake, upendo wake, neema yake, haki yake, furaha yake pamoja na amani huwepo. Ufalme wa Mungu ukiwepo yote yanawezekana! maana uko juu ya yote.

Ufalme wa Mungu Unatawala Vitu Vyote

Maandiko yanasema, “BWANA ameweka kiti chake cha enzi mbinguni, Na ufalme wake unavitawala vitu vyote” (Zaburi 103:19). Kuanzia leo fahamu ya kuwa ufalme wa Mungu uko juu na unatawala kila kitu.
Hakuna ugonjwa uliopo juu ya ufalme wa Mungu, hakuna uchawi au mkosi uliyo juu ya ufalme, kila kitu kiko chini ya ufalme; yaani mamlaka na nguvu za Mungu.

Ufalme Upo Ndani Yako

Kwa sababu umemwamini Yesu kuwa Bwana na Mwokozi wako ufalme wake ulio juu ya kila kitu upo ndani yako. Ndani yako unazo nguvu na mamlaka ya kutawala kila kitu. Yesu aliwaambia mafarisayo, “…tazama, ufalme wa Mungu umo ndani yenu” (Luka 17:21). Kwa kusema hivi alimaanisha ufalme wa Mungu unaweza kutawala ndani ya mtu na kupitia mtu.
Kuna mambo kadhaa yanayoweza kukuhakikishia kwamba ufalme wa Mungu uliopo ndani yako unaweza kutawala vyote kupitia wewe.
Mungu Mwenye Ufalme Yupo Ndani yako
Biblia inasema, “Hamjui ya kuwa ninyi mmekuwa hekalu la Mungu, na ya kuwa Roho wa Mungu(Mungu)anakaa ndani yenu?
(1 Wakorintho 3:16). Mungu ni Mfalme, anao ufalme. Kwa kuwa anakaa ndani yako, utawala wake juu ya dhambi, magonjwa, mashetani na kifo umo ndani yako pia. Unao ufalme unaoshinda ndani yako.

Roho Mtakatifu Anakuwezesha Kutawala kwa Ufalme Ndani yako
Maandiko yanasema, “Maana ufalme wa Mungu si kula wala kunywa, bali ni haki na amani na furaha katika Roho Mtakatifu.” (Warumi 14:17). Kwa haki furaha na amani katika Roho Mtakatifu wewe ni mtawala juu ya vyote. Dhambi haikutawali kwa kuwa umehesabiwa haki, pia ni mtenda haki kwa uwezo wa Roho. Huzuni ya namna yoyote yakiwemo magonjwa, haikutawali maana u mwenye furaha kwa msaada wa Roho Mtakatifu. Unayo amani mbele za Mungu kwa damu ya Yesu iliyokuosha katika Roho wa Kristo. Shetani hawezi kukushitaki tena hata ukakosa amani, Damu imefanya amani kati yako na Mungu, wewe si adui wa Mungu damu ya Yesu imekupatanisha na Mungu.
Ufalme wa Mungu upo Ndani yako kwa Neno lake
Daudi alisema, “Moyoni mwangu (ndani yangu) nimeliweka neno lako, nisije nikakutenda dhambi.” (Zaburi 119:11). Neno la Mungu linaweza kukaa ndani yetu kama ufalme wa Mungu. Ninaamini kuwa ufalme wa Mungu na Neno lake haviwezi kutenganishwa, kwa kuwa Neno lina mamlaka, nguvu, furaha, amani, haki, na uwepo wa Mungu. Mtu mwenye Neno la Mungu ndani yake anao ufalme wa Mungu. Inakupasa kulitafakari Neno mpaka ulione bayana, ili uhakika uzaliwe utakaobeba yatarajiwayo na kuyazalisha kwa kuamini.

Tawala kwa Kutumia Neno lililo Ndani yako

Neno la Mungu linao ufalme ulio juu ya yote. Ulitamkapo kwa imani, unapoliamini ni lazima limiliki na kushinda! Utamkapo Neno kwa imani unakuwa juu ya kila kitu kinachojaribu kukumiliki, kwa kuwa unatamka kwa kutumia mamlaka iliyo juu ya mamlaka zote. Utumiapo Neno juu ya ugonjwa lazima ugonjwa utii na kuondoka kwa kuwa ni mamlaka iliyo kuu. Ingawa unaweza kuonekana kwamba bado upo, imani hupokea uponyaji sasa, baada ya hapo huamini kwa kusema kama Mungu aliye dhahiri asemavyo. Ulitumiapo dhidi ya mapepo lazima yatii kwa kuwa ni Neno la ufalme ulio juu yao ni Neno la ufalme wa Mungu. Hili ni Neno lisiloweza kuzuiliwa na mazingira yoyote, ni Neno lisilozuilika kutenda, maandiko yanasema, “…neno la Mungu halifungwi.” (2 Timotheo 2:9).

Malaika na Ufalme
Malaika wa Mungu ni watumishi wa ufalme wa Mungu, wanamtumikia Mungu na wale wanaourithi wokovu (wana wa Mungu), (Waebrania 1:12-13). Malaika wanasikiliza na kulitenda Neno lake Mungu, wanafanya mapenzi ya Mungu, maandiko yanasema, “Mhimidini BWANA, enyi malaika zake, Ninyi mlio hodari, mtendao neno lake, Mkiisikiliza sauti ya neno lake.” (Zaburi 103:20). Kwasababu malaika wanafanya Neno au mapenzi ya Mungu, inamaana kwamba wanakutumikia kwa njia ya Neno hilo. Unapotamka Neno la Mungu lililofunuliwa na Roho Mtakatifu ndani yako, malaika hulitenda/hulitimiza Neno hilo. Kwa mfano ukisema, “Bwana Yesu ndiye mlinzi wangu”, kwa neno hilo malaika watakuhudumia na kukulinda. Uliitapo jina la Yesu likuokoe, kwa mfano toka katika ajali malaika watakupigania na kukuokoa.
Utamkapo Neno la Mungu unamiliki kwa nguvu za ufalme wake kwa utendaji wa malaika zake, haikupasi kuwatukuza na kuwaabudu malaika kwa matendo yao, bali kumpa Mungu utukufu wote maana wanamwakilisha yeye kwa yale wayatendayo.


Sasa umekwisha kufahamu kuwa wewe uko juu ya kila kitu kwa njia ya ufalme ulioko ndani yako. Achilia nguvu ya ufalme huo kwa njia ya kulitamka Neno lake kwa imani. Hakuna ugonjwa, kifo, uchawi au laana, inayoweza kukushinda, unao ufalme ushindao/ utawalao kila kitu; UFALME HUO, UMO NDANI YAKO, UNATAWALA KUPITIA KINYWA CHAKO.

No comments:

Post a Comment