Thursday, July 31, 2014

Malaika Walinzi

Shuhuda za Mwinjilisti Grace Mbise (Mama Mbise)



Maandiko matakatifu yanaonyesha kwamba malaika wa Mungu wapo na wanatenda kazi pamoja na watu wa Mungu; katika kuwahudumia na vita vya kiroho.  Kwa mfano hebu soma maandiko haya, “Malaika wa BWANA hufanya kituo, akiwazunguka wamchao na kuwaokoa” (Zaburi 34:7), “Waaibishwe wafedheheshwe, Wanaoitafuta nafsi yangu.  Warudishwe nyuma, wafadhaishwe…Wawe kama makapi mbele ya upepo, Malaika wa BWANA akiwaangusha chini.” (Zaburi 35:4-5), “Kwa kuwa atakuagizia malaika zake Wakulinde katika njia zako zote.” (Zaburi 91:11). Katika makabiliano ya vita vya kiroho, malaika wa Mungu wanatenda kazi hata sasa, ikiwa tunawaona au ikiwa hatuwaoni.  Mama Mbise amepewa neema ya kuona utendaji wa malaika wakati akiwa katika mapambano ya kiroho katika huduma.  Karibu usome shuhuda hizi tena:

Wakati fulani mgonjwa aliletwa nyumbani kwangu ili aombewe.  Alikuwa ni ndugu wa rafiki zetu huko Njani.  Alitokea hospitali ya KCMC.  Alikaa siku tatu wakati huo huo tukiendelea na maombi.  Vita vilikuwa vikali sana alikuwa hawezi kuongea mdomo umepinda nk.  Baada ya siku nne alianza kupata ufahamu.  Baada ya wiki moja alianza kukaa na kufanya mazoezi ya kutembea.  Tulikuwa na dada aliyekuwa akitusaidia kazi aitwaye Esta aliokea Nkwanekoli.  Siku moja saa tano mchana  wakati Esta anamwogesha mgonjwa, mimi nilikuwa chumbani naomba.  Baada ya kumaliza maombi nikakaa kitandani, ghafla upepo ukaanza kuingia chumbani kwa mfano wa moshi, ulikuwa wa rangi kama ya kijivu au bluu.  Ulikuwa ni mfano wa ukungu mzito.  Nikaanza kushindwa kupumua.  Nikaanza kuomba na kukemea.  Ghafla ndani ya ule moshi nikaona viumbe vingii!, kama viwatu vidogo vidogo.  Mwonekano wake ulikuwa kama askari wengi wenye mavazi ya kivita, walikuwa wameshika vitu mfano wa virungu (Maandiko yanasema vita vyetu vinahusika na jeshi la pepo wabaya katika ulimwengu wa roho, inawezekana hawa walikuwa ni moja ya kikosi cha pepo hao- Waefeso 6:12).  Walianza kunipiga na mimi niliendelea kukemea, nikaona kama vile ninazidiwa nguvu nikalegea wakachukua miguu yangu na kuiweka kitandani.  Yakatokea majitu mengine makubwa mawili, walikuwa na maumbo kama watu lakini hawakuwa watu! (Inawezekana hawa ni wakuu wa giza ambao walikuwa ni majemedari wa jeshi la pepo hawa). 

Wakachukua kamba kubwa wakaiviringisha na kunifunga mpaka kwenye mabega yangu.  Wakaanza kunibeba na kusema “Dawa yake huyu ni kumbeba na kumpeleka, ni kumtowesha asionekane tena”  Nikajiona natoka kitandani mpaka pua yangu ikagusa dari.  Ghafla nilisikia sauti ya kishindo kama radi “PAAA” Wakatokea malaika wawili wakubwa!! Mmoja akasimama kushoto kwangu na mwingine kulia.  Kila mmoja ameshika upanga, ambao ulikuwa ni kama moto uwakao!! Sikujua wameshikaje mapanga yale maana mpini ulikuwa hauonekani ilikuwa kana kwamba wameshika kwenye moto.  Malaika hawa walikuwa wana utisho mkuu.  Walikuwa wazuri wenye sura za huruma zenye kung’aa, pia walikuwa na mabawa makubwa yaliyovuka mabegani mwao.  Urefu wao haukupungua futi  saba au nane hivi.  Mmoja wao akasema, “hapo hapo asitoke hata mmoja”  Akafunua chini kwa mfano wa mtu afunuaye  mfuniko wa shimo la maji machafu.  Wale malaika wakawaambia, “Hamna mamlaka huyu ni mtumishi wa Mungu, amekombolewa na damu ya Yesu”.  Wakachomoa kitu mfano wa kadi za benki au kadi ya ATM, kilikuwa cha rangi nyekundu wakawaonyesha na kusema, “Huu ndio ushahidi”, Halafu wakasema, “Mko wangapi?” wakajibu, “Elfu moja mia sita” , Malaika akasema, “Kuanzia sasa hamtafanya kazi tena duniani” Halafu wakawatumbukiza ndani ya lile shimo kwa kuwaamrisha. 

Wakati huo nilikuwa kitandani nimefungwa kamba, Dada Esta akafungua mlango alikuja kuchukua mafuta ya kumpaka mgonjwa, akaanguka chini na kuanza kunena kwa lugha muda mrefu.  Alipokuwa akinena kamba niliyokuwa nimefungwa ikaanza kulegea.  Alipomaliza kunena tu, kamba zote zilikuwa zimeniachia (Kunena kwa lugha za Roho Mtakatifu kunaweza kumfungua mtu na kamba za kishetani zinazoonekana na zisizo onekana, usiache kunena kwa lugha.  Mfano huo tumeuona kwa dada Esta).  Wakati huo malaika walikuwa wameshaondoka.  Baadaye Esta aliniambia alipofungua mlango aliona watu wanaongaa sana na akashindwa kustahimili na kuanguka.

No comments:

Post a Comment