Wednesday, July 30, 2014

Kazi Mbaya za Ulimi




Kitu chochote ambacho ulimi hutoa moyoni hukileta kupitia maneno. Ikiwa maneno hayo yataleta uharibifu hiyo ni kazi mbaya ya ulimi.

Kuchongea

Neno hili kuchongea au mchongezi linataka kufanana na maneno mzushi, mchonganishi au aletaye faraka.  Biblia inasema “Usiende huko na huko katikati ya watu wako, kama mchongezi; wala usisimame kinyume cha damu ya jirani yako; mimi ndimi BWANA”  (Mambo ya Walawi 19 :16). Katika  kitabu cha kutoka imeandikwa  Usivumishe habari za uongo; usitie mkono wako pamoja na  mwovu kuwa shahidi wa udhalimu” (Kutoka 23:1). 

Maneno ya kuchongea yanaweza kuharibu ushirika na hata huduma.  Msukumo wa kuchongea inaweza ikawa ni: hila,wivu,uchungu,chuki au kitu chochote kibaya kilichopo moyoni.  Kusudi la kuchongea laweza kuwa kuondoa kibali alichonacho mtu kiuchumi au kihuduma, ili  kuona ameshindwa kuendelea katika kitu afanyacho. 
Nabothi aliuwawa na Yezebeli kwa uchongezi ambao ndani yake ulikuwa na hila. Ahabu mume wa Yezebeli aliitaka  ardhi ya Nabothi, lakini ilishindikana kuipata kwa njia za kawaida.  Hivyo mkewe yaani Yezebeli akampa mawazo mabaya ili Nabothi achongewe na kuuwawa. Kusudi lilikuwa Ahabu apate ardhi ya Nabothi, imeandikwa, “Akaandika katika zile nyaraka, akasema, pigeni mbiu ya watu kufunga, mkamweke Nabitho juu mbele ya watu; mkainue watu wawili, watu wasiofaa, ili wa mshitaki, na kumshuhudia kunena, umemtukana Mungu na Mfalme kisha mchukueni nje, mkampige kwa mawe ili afe… Na hao watu wawili, watu wasiofaa wakaingia wakaketi mbele yake; wale watu wasiofaa wakamshuhudia Nabothi mbele ya watu, wakasema, Nabithi amemtukana Mungu na mfalme.  Ndipo wakamchukua nje ya mji wakampiga kwa mawe hata akafa” (1Wafalme 21:9-10,13).  Ukiendelea utaona baada ya Nabothi kufa ardhi yake ilichukuliwa na Ahabu.  Je umewahi kuona kitu kama  hiki  kikitokea  kwa mtu? Kama umeona sababu yake  kuu  ni misukumo mibaya iliyopo moyoni ambayo huleta uchongezi. 
Mara nyingi hili linaweza kuonekana maeneo yafuatayo. Ikiwa mtu anafunikiwa kwa kupata kibali mfano kazini, basi mioyo ya wenzake inaweza kujenga hila, wivu au uchungu. Haya ni matayarisho ya kwanza ya uchongezi, ikitokea mtu huyo amekosea kufanya kazi kidogo, basi mioyo hiyo huachilia maneno ya uchongezi ili kumnyang’anya kibali hicho kama Nabothi alivyonyang’anywa ardhi. Mara nyingine kunaweza kukawa hamna kosa, lakini likaundwa na kusambazwa, kama walivyofanya kwa Nabothi wale watu wasiofaa. Hili linaweza kutokea popote hasa maeneo ya madaraka, heshima au mafanikio ya kibiashara. Kila mtu inampasa ijilinde na moyo wa uchongezi kwa kutoruhusu   wivu, hila, au uchungu pale anapoona mtu mwingine  anafanikiwa.  Ulimi wa uchongezi unaua! Shetani ni mchongezi, anasambaza maneno mabaya. 
Tunaposambaza maneno mabaya kama ni ya kweli au si ya kweli tunashirikiana na Shetani.  Ikiwa kuna jambo baya mtu ametenda, fanya vitu vifuatavyo.
1.      Omba Mungu akupe maarifa na hekima jinsi ya kusema au kutenda.
2.      Omba Mungu akusaidie kutenda kwa kutumia maandiko.
3.      Ikibidi lipeleke katika mikono salama ya kiongozi wa mtu huyo hakikisha katika Roho Mtakatifu kiongozi huyo anaweza kulishika na kutoa ufumbuzi kwa Neno na Roho Mtakatifu , sio kwa kusambaza maneno na kuchongea. Sio sawa kukaa kimya tuonapo uovu, lakini pia sio sawa kusema ovyo, ovyo.

4.      Hakikisha unaposema kitu kibaya cha mtu, mfano kama ametenda dhambi, moyoni mwako hamna hali yoyote ya kufurahia.  Ukiona moyo wako una hali ya kufurahi na kukejeli, ukisema kitu hicho kitaachilia roho ya kusengenya. Mara nyingi kusengenya kunaleta hali ya kufurahia kumsema mtu vibaya, kunaburudani ya uongo yenye mauti ndani yake. Mwisho wake ni kuua, “maneno ya mchongezi ni kama vitoweo, hayo hushika pande za ndani za tumbo (Mithali 18 : 8). Ni kweli dhambi ni mbaya, ila inavyoshughulikiwa inapaswa mwenye dhambi huyo apone, pamoja na sura ya kanisa kulindwa. Kuvifanya vitu hivi viwili kwa pamoja sio rahisi, ila kwa Neno la Mungu, Roho Mtakatifu na maombi inawezekana.

5.      Fahamu kwamba kila jambo na wakati wake kuna wakati kusema na kukaa kimya (Muhubiri 3:1). Ukifika wakati wa kusema, inabidi  pia ujue usemeje na useme kwa nani.  Hapa unahitaji kuomba na kumsikia Mungu, ili kuponya kanisa  kulilinda, na ikiwezakana kumwokoa mwenye dhambi.

Uongo

Moja ya dhambi ya hatari na rahisi kuifanya ni uongo.  Ninaiita ya hatari kutokana na andiko hili:
Ninyi ni wa baba yenu Ibilisi, na tamaa za baba yenu,  Ndizo mpendazo kuzitenda, Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake.  Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na baba wa huo” (Yohana 8 : 44).

Kama umempa Yesu maisha yako, dhambi moja mbaya ya kujiepusha nayo ni uongo.  Sababu ni kwamba “wote waliompokea Yesu aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu”, lakini hapo hapo wasemao uongo ni watoto wa Ibilisi. Uongo unamwingiza mtu katika umiliki wa Ibilisi. Kwa hiyo ikitokea unasema uongo usivumilie kuwa katika hali hiyo tubu kisha angalia ni msukumo gani uliopo moyoni uliokufanya udanganye. 

Msukumo mmoja unaoweza kumfanya mtu aseme uongo ni woga.  Woga wa kukosa heshima, Woga wa kukosa pesa n.k, unweza kumfanya mtu aseme uongo.  Kwa mfano mtu anaweza kumpingia mwenzake simu, halafu akamwambia nitakupigia baadaye, Akisema hivi akasahau ni sawa ingawa si sawa.  Ila akisema hivi na moyoni  amekusudia kutopiga ila anaogopa kukuambia moja kwa moja kitu unachomuuliza, huu ni uongo. 

Anaweza kuwa amelinda heshima yake kwa kutoonyesha kuwa hana kitu hicho, lakini kiroho amekuwa mwongo! Biblia inasema Ibilisi ni baba wa uongo, hivyo  huyu anaingia moja kwa moja katika imaya ya Ibilisi.  Ndugu yangu ninapoandika maneno haya niaandika pia kwa aliji yangu mwenyewe. Tunahitaji neema kubwa eneo hili maana ni rahisi kusema uongo lakini ni hatari, maana uongo unamwingiza mtu kwenye hukumu ya Ibilisi kwa kuwa ni baba wa uongo. Hatari nyingine inaonekana kwenye andiko hili “kuna vitu sita anavyovichukia BWANA ….ulimi wa uongo” (Mithali 6:16,17).  Vimetajwa vitu kadhaa anavyochukia Mungu katika Maandiko haya  kimoja ni ulimi wa uongo.  Mtu anaposema uongo neno hilo litokapo kinywani inawezekana Mungu anakuja uso.  Maana anajua chanzo cha uongo ni Ibilisi adui yake.  Tusemapo uongo tunamwacha Mungu kama Baba na kumpa Ibilisi nafasi, hiyo ni hatari. Hatari nyingine inaonekana katika andiko hili “Bali waoga, na wasioamini na wachukizao na wauaji, na wazinzi, na wachawi na hao waabuduo sanamu, na waongo wote sehemu yao ni katika lile ziwa liwakalo moto na kiberiti.  Hii ndiyo mauti pili” (Ufunuo 21:8). Angalia neno hili “na waongo, wote”.  Andiko hili halijaonyesha tofauti ya waongo, limesema waongo wote!  Itatugharimu kutosema uongo, lakini gharama ya kwenda jehanamu ni kubwa kuliko kitu chochote ambacho tunaweza kukipoteza tukisema kweli.  Kumbuka vitu hivi.

1. Tusemapo uongo tunakuwa chini ya Ibilisi.
2.   Tusimapo uongo Mungu anachukia.
3.   Tusemapo uongo tunafungua mlango wa kwenda Jehanam kwa ndimi zetu.
 
Kuanzia leo jilinde na dhambi zote lakini hasa uongo.  Sababu ni kwamba ni rahisi kuitenda lakini ni hatari. Misukumo ya moyoni ambayo inaweza kuleta uongo kinywani ni woga (hasa wa wanadamu) tamaa ya heshima au vitu, au mashindano.  Hapa tunahitaji toba ya haraka na neema ya kushinda.  Mara nyingine mwombe msamaha yule uliyemdanganya, hii inaweza kukupotezea heshima, kibinadamu, lakini kwa tendo hili utamkana Shetani na kumpa Mungu nafasi.  Huu utakuwa  mlango wa kushinda uongo, kuna faida gani watu wakikuheshimu wakati umedanganya, halafu Mungu akakasirika, Shetani akakupata, na mlango wa jehanamu ukafunguka?  Dhambi moja ya ulimi inaweza kusababisha nyingine.  Kwa mfano umesikia mtu amesema uongo halafu ukamwambia mtu mwingine “jamani he! Sikuhizi mijitu ni miongo kweli umesikia fulani alivyosema….”. Hapa utakuwa umeanza kusengenya.  Ni kweli yule alisema uongo, lakini umeruhusu uongo wake kukufanya usengenye!  Pia kwa kusema uongo huko unaweza kuanza kumtangaza si kwasababu unataka kumsaidia, bali una wivu au hila  au uchungu na kitu fulani alichonacho, unataka kumchongea.  Hapa utakuwa umefanya dhambi ya uchongezi kwa uongo wake.  Njia salama zaidi ni kumwambia na kumwonya kama kweli unataka kumsaidia.  Mara nyingine mtu anaweza kusikia amesengenywa au kachongewa, halafu yeye akatukana.  
Dhambi za ulimi ni kama mnyororo ikitokea moja inafungua mlango kwa nyingine, inabidi mnyororo huo ukatwe haraka. Zikiachiliwa  kanisa zima linaweza kufungwa na mnyororo huo “chachu kidogo huchachua donge zima” tena “moto mdogo huwasha msitu mzima”. Biblia inasema “msidanganyike;  mazugumuzo mabaya huharibu tabia njema” (Wakorintho 15 : 33). Tafsiri  nyingine ya andiko hili ni “kuwa na ushirika wa karibu kwa njia ya maneno na mtu mbaya mwenye maneno mabaya huaribu tabia njema”.  Ikibidi jitenge na mtu mchongezi, au msengenyaji, ili kukata mnyororo wa dhambi za ulimi, lakini ni vizuri kumwonya kwanza.
 

Maneno Yasiyo na Maana

Mara nyingine unaweza kutamka neno bila kumaanisha kwa hakika ulichokisema.  Hilo linaweza kuwa neno lisilo na maana. Kwa upande mwingine mtu anaweza kukufuru au kudhihaki jambo la Mungu hili nalo ni neno lisilo na maana. Yesu alisema  Basi nawaambia kila nenolisilo maana, watakalolinena wanadamu,watatoa hesabu ya neno hilo siku ya hukumu” (Mathayo 12: 36). Yesu alisema maneno haya baada ya Mafarisayo kusema anatoa pepo kwa Belzebuli mkuu wa  pepo.  Hili lilikwa ni neno nilisilo na maana.  Maneno anayotamka mtu mfano kumwita Mungu “Bwana Godi” au “sir Godi” ni maneno yasiyo na maana.  Maneno haya ni ya kutoa hesabu. 
Siku moja nilikuwa sebuleni naangalia televisheni.  Mtoto wangu mmoja alipita na kuanza kupiga kelele.  Ghafla nikatamka maneno yafuatayo bila kujua “Liangalie, linapiga kelele…” hapo hapo moyoni nikapata ushuhuda usemao “UMEKOSEA” Neno nililotamka lilikuwa halina maana, niliudhalilisha uthamani wa mtoto kwa kusema “Liangalie” nilitubu haraka bila hivyo neno hilo ingenipasa nilitolee hesabu.

Maneno ya Haraka
Moyo wenye shida ya uchungu au hasira unaweza kusema haraka kitu ambacho mwisho wake ni mauti. Biblia inasema “Wakamghadhibisha kwenye maji ya Meriba.  Hasara ikampata Musa kwaajili yao, kwasababu  waliiasi roho yake, Akasema yasiyofaa kwa midomo yake” (Zaburi 106:32-33). Kwa kuwa Musa alikuwa na kisirani na wana wa Israeli katika moyo wake alitamka kwa haraka maneno ambayo yalimzuia kuingia nchi ya ahadi.

 Mke wangu Slyvia amenifundisha kukaa kimya kama nimekasirika mpaka niwe katika hali ya kawaida.  Mara nyingi nikisema wakati nimekasirika husema kwa haraka bila kufikiria na ni lazima nitakosea. Kwa neema ya Mungu ananiwezesha kutosema kwa haraka kutokana na misukumo ya moyoni.
Unaweza kuwa na nia nzuri ya kufanya kitu, mfano moyo wako unafurahia kuhubiri kisha ukasema mbele za Mungu, “Mungu niko tayari kuhubiri injili dunia nzima”.  Haya ni maneno ya haraka yatokayo katika moyo wenye shauku nzuri, ila yamenenwa bila kufikiria.  Biblia inasema “Usiseme maneno ya ujinga kwa kinywa chako, wala moyo wako usiwe na haraka kunena mbele za Mungu; kwa maana, Mungu yupo mbinguni na wewe upo chini, kwa hiyo maneno yako na  yawe  machache. Wewe ukimwekea Mungu nadhiri usikawie kuitoa…”(Muhubiri.5:3-14).  Tunapotamka kitu mbele za Mungu, Mungu hukishika.  Tusipokifuatilia kinaweza  kugeuka kuwa dhambi kwa hiyo tuyatazame maneno mioyoni mwetu  kabla hatujasema Mungu huyafuatilia.   Hapa pia imeandikwa maneno yetu yawe machache.  Ila hatujui maneno machache ni mangapi! Ninaamini maneno machache ni kuweza kuongea huku unajisikiliza.  Ni kuongea kitu ambacho moyoni umekiona na kukisikia na hakijatoka bahati mbaya.

Ni kitu ulichokichuja, vinginevyo ni rahisi kukosea.  Bibliainasema “Katika wingi wa maneno hapakosi kuwa na uovu.  Bali yeye azuiaye midomo yake hufanya akili” (Mithali 10 :19). Kuweza kuzuia ulimi au maneno ni busara.  Maneno “yeye azuiaye midomo yake afanya akili”, yanafanana na neno busara. Tumekamilika kwa njia ya kuhesabiwa haki kwa imani ya Yesu.  Tunauishi ukamilifu huo katika ndimi zetu. Mtu awezaye kuushinda ulimi anaweza kushinda kitu chochote. Biblia inasema “Maana twajikwaa sisi sote pia katika mambo mengi.  Mtu asiyejikwaa katika kunena huyo ni mtu mkamilifu awezaye kuzuia mwili wake wote kama kwa lijamu” (Yakobo 3:2).  Kwa njia ya ndimi zetu kumbe tunaaweza kuongoza vitu vingine katika miili au maisha yetu. 
Vipimo
Hatuwezi kuangalia kazi zote za ulimi ambazo ni mbaya.  Kitu cha msingi ni kujua kanuni ambazo kwazo tutaweza kujua neno linalofaa ni lipi na lisilofaa ni lipi.
1.      Jiulize je, neno ninalosema linaleta neema, linamwezesha na kumwinua mtu anayesikiliza? “Neno lolote lililo ovu lisitoke vinywani mwenu, bali lililo jema la kumfaa mwenye kuhitaji ili liwape neema wanaosikia” (Waefeso 4 :29).
2.      Je neno unalosema kuhusu mwenzako, upo tayari kusikia wewe unasemwa hivyo? bila kusaidiwa? Kumsema mtu bila kumsaidia na yeye bila kujua, ni kama kumtafuna mgongoni kidogo kidogo wakati yeye haoni na hawezi kujilinda.  Uko tayari kufanyiwa hivyo? “Basi yoyote myatakayo mtendewe na watu, nanyi watendeeni vivyo hivyo; maana hiyo ndiyo torati na manabii” (Mathayo 7:12).
3.      Ikiwa umesambaza habari mbaya kuhusu mtu au watu.  Baadaye ukagundua si kweli je utaweza kusambaza habari njema ili kufuta ile mbaya uliyosema? Utaweza kuponya moyo wa mtu uliye muumiza kwa kumsema vibaya? Utaweza kuirudisha mioyo ya watu waliopoteza imani kwa mtu huyo wamwamini tena? Kama ni kanisa limegawanyika  unaweza kulirudisha tena?
4.      Je usemapo neno dhamiri yako inakuwa na ujasiri mbele za Mungu? Unasika kutohukumiwa “….mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu” (1Yohana 3 : 2).
5.      Neno unalotaka kulisema utalisema ukiwa katika hali gani? Je utakuwa umekasirika, una uchungu, una wivu, una unafiki, una upendo au imani?  Hali hizi za moyo ndizo zinazojenga aina za maneno. Hali hizi ziujazapo moyo, kinywa kitanena maneno yanye sura ya hali hizo za moyoni.
6.      Unachotaka kusema kinapatana na Neno la Mungu? Kila kisemwacho kinyume na Neno ni dhambi na kila kusemwacho, Bila imani ambayo chanzo chake ni Neno ni dhambi “Na kila tendo lisilotoka katika Imani ni dhambi” (Warumi 14 : 23)  Hivi ni vipimo au gharama zitakazo kusaidia kuwa mwangalifu jinsi unavyoongea.

1 comment: