Monday, July 28, 2014

Kazi za Ulimi 1


MIFANO YA ULIMI 
Katika maandiko ulimi na maneno vimefananishwa na vitu kadhaa kwa kazi zake.  Mifano hii  inaweza kutufungua na kuzidi kutupa ufahamu kuhusu nafasi ya ulimi na maneno katika maisha yetu.
Maneno ni Matunda
Ulimi ni kama tawi lililo katika mti.  Tawi hili hutoa matunda yanaitwayo maneno.  Unafahamu shina la tawi hili ni nini?  ni moyo.  Ili tawi lizae matunda ni lazima liwe katika shina.  Ili ulimi useme maneno au matunda yapasa uunganishwe na moyo. Ukitaka kubadilisha aina ya matunda usiangaike na tawi shughulikia shina, yaani moyo.  Tukitaka kubadilisha maneno hatuangaiki na ulimi tunahangaika na moyo.
Usisahau mfano huu moyo ni mti, tawi ni ulimi matunda ni maneno. Yesu alisema, “ufanyeni mti kuwa mzuri na matunda yake kuwa mazuri…” (Mathayo 12:33). Kwa mfano wetu tunaweza kusema “ufanyeni moyo kuwa mzuri na maneno yake kuwa mazuri”.  Yesu aliendelea kusema katika mstari huo,…au ufanyeni mti kuwa mbaya na matunda yake mabaya, kwamaana kwa matunda yake mti hutambulikana”  kwa mfano wetu tunaweza kusema “au ufanyenni moyo kuwa mbaya na maneno yake kuwa mabaya”. Baada ya kusema hivi Yesu alisema maneno mengine katika msitari wa thelathini na nne alisema “Enyi wazao wa nyoka, mwawezaje kunena mema, mkiwa wabaya?  Maana kinywa cha mtu huyanena yaujazayo moyo wake.”  Kwa hiyo hapa tunahitimisha kuwa ubaya wa mti unapelekea matunda kuwa mabaya.  Ubaya wa moyo unapelekea maneno ya ulimi kuwa mabaya.  Pia tunagundua kuwa kutozaliwa na Mungu ni kuwa mzao wa nyoka au Shetani. Kutozaliwa na Mungu hupelekea mtu kuwa mbaya na maneno kuwa mabaya.  Maana Yesu alisema enyi wazao wa nyoka mwawezaje kunena mema mkiwa wabaya. Kwa hiyo mtu akiwa mzuri, asipokuwa mzao wa nyoka ni hatua ya kwanza ya kuanza kusema maneno mazuri maana asili yake imebadilika. Lazima mtu azaliwe mara ya pili ili awe mtoto wa Mungu na sio wa Shetani. Hii itamwezesha maneno yake yabadilike.  Huu ni msingi wa kwanza wa maneno mazuri, yaani kuzaliwa na Mungu, kubadilishwa asili ya ndani inayopelekea kubadilika kwa aina ya maneno.

Maneno ni Maji
Maneno yatokayo katika ulimi ni kama maji.  Yanaweza kuwa matamu au machungu. Utamu wake au uchungu unategemeana na yanapotoka.  Kama chanzo chake ni utamu basi yatakuwa matamu, kama ni uchungu yatakuwa ni machungu. Chanzo cha maji twaweza kukiita ni moyo na maji yenyewe ni maneno.  Moyo ukiwa na matatizo na maji yake au maneno yatakuwa na matatizo, ukiwa mzuri na maneno yake pia yatakuwa mazuri. Kama vile maji yanavyobubujika toka katika chemchemi, ndivyo maneno yanavyobubujika toka moyoni. Kama vile maji mazuri yanavyo wafaa watu  kwa mfano kupooza kiu, ndivyo maneno mazuri yalivyo hupooza na kuponya.
Kama vile maji mabaya yenye uchungu au sumu yalivyo ndivyo maneno mabaya hukosesha raha na yanaweza hata kuua.  Ukiwa na kiu ukapewa chupa ya maji yenye chumvi na maji yasiyo na chumvi utachangua chupa ipi?  Maandiko yanasema “Bali ulimi hakuna awezaye kuufuga; ni uovu usiotulia, umejaa sumu iletayo mauti. Kwa huo twamhimidi Mungu Baba yetu, na kwa huo twawalaani wanadamu waliofanywa kwa mfano wa Mungu. Katika kinywa kilekile hutoka baraka na laana.  Ndugu zangu, haifai mambo hayo  kuwa hivyo.  Je chemchemi katika jicho moja hutoa maji matamu na maji machungu? Ndugu zangu, Je! mtini waweza kuzaa zeituni, au mzabibu kuzaa tini? Kadhalika chemchemi haiwezi kutoa maji ya chumvi na maji matamu” (Yakobo 3 :8-12).
Moyo mzuri au wenye hali nzuri hauwezi kutoa maneno mabaya. Moyo mbaya au wenye hali mbaya hauwezi kutoa maji au maneno matamu.  Maneno  mazuri ni uzima maneno mabaya ni mauti.  Moyo mbaya hufunguliwa mauti kwa maneno. Moyo mzuri hufunguliwa uzima kwa maneno.  

No comments:

Post a Comment