Sunday, July 27, 2014

Yesu Bado Anatokea 2

 SHUHUDA NA MCHUNGAJI PAULO BUSUNGU



Yesu Anitokea na Kufukuza Mashetani

Nilipofika nyumbani niliona ni vema niombe tena Mungu, kabla sijalala.  Nilipofika usawa wa kitanda nikapiga magoti niombe, nikafanya ishara ya msalaba. Hapo hapo nikakatisha maombi, niliona niombe kwa namna ambayo najisikia kujieleza mimi mwenyewe kwa Mungu na si kufungwa na sala ile ya kanisani.  Niliona nimweleze Mungu hali yangu, ilivyo nisije nikarudi tena shimoni.  Niliomba sala nyingine niliyojitungia.  Niliomba maombi mawili, nikainua mkono na kunyoosha kidole huku naangalia macho juu nikisema, “Ee Mungu nisamehe maovu yangu yote, Nikifa Mungu nisiende kwenye shimo nililoenda, bali niende na Yesu”

Niliposema niende na Yesu, ilitokea ngumi ambayo sikumwona mwenye ngumi, ilikuwa hewani tu, ikanipiga kichwani.  Nikaanguka chini nikijua sasa nimekufa, moyoni nikajisemea, hata kama nimekufa nitaenda na Yesu.  Sikufa ila nilitetemeka hata asubuhi, kulipokucha nilijua mchana wakati wowote naweza kufa.

Asubuhi nikamwambia mke wangu twende shambani.  Nilikuwa na maana ya kwenda shambani kuliangalia mara ya mwisho.  Tuliporudi mke wangu alitengeneza chakula, tulikula huku nikiwa na huzuni nikijua ninamwacha na motto mmoja tuliyekuwa naye.  Baada ya hapo mama akatoka nje, ilikuwa ni kwenye saa tisa ya mchana.  Niliingia chumbani nikakaa kitandani. Nikawaza mbona nimeteseka miaka yote! Acha nife tu, acha nife tu.  Mbona hata Karume amekufa, kipindi hicho Karume raisi wa Zanzibari, alikuwa amekufa muda si mrefu. Maneno haya aliyokuwa akisema mtumishi afe tu afe tu, hakuwa yeye, mashetani yalikuwa yakisema katika nafsi yake kwa sura yake yeye.  Shetani hutumia akili zetu kusema nasi kama nafsi zetu wenyewe.  Ukiweza usome kitabu cha Mitego ya Shetani nilichokiandika upate ufafanuzi zaiji jinsi atendavyo.

Wakati naendelea kuwaza hivyo upepo ulivuma na nikaona kipeperushi cha injili (traks) kimeletwa na upepo kikatua chumbani, nikasikia sauti moyoni ikisema chukua hiyo, chukua hiyo uisome.  Sauti hii ni kama ile iliyoniambia, “Tazama juu” nilipokuwa shimoni.  Nyumba yetu ilikuwa ya kienyeji ina dirisha dogo, nikatoka nje kuisoma nikasimama mlangoni niisome. 

Roho ya Mauti
Nikaianza kuisoma msitari wa kwanza uliandikwa, “Yesu Kristo ni Mwokozi”.  Niliposoma tu, nikapigwa ngumi tena kama usiku!  Nikaingia chumbani huku ninatetemeka. Nilipofika usawa wa kitanda nikaanguka kitandani.  Nilipopandisha miguu kitandani nikaona kitu.  Niliona lidude kama binadamu, lakini si binadamu. Lilikuwa kubwa na lenye nguvu mtu asiweze kushindana nalo.  Kwa kulitazama liliweza hata kushinda watu elfu kwa mara moja. Likanishika kinywa na pua nishindwe kupumua. Nikasema wakati linaziba pua na mdomo, “Ikiwa Shetani anauwa nitakufa, lakini shimoni siendi naenda na Yesu”  Nilipotamka naenda na Yesu likaniachia na kukimbia kwa hofu!

Likarudi tena mara ya pili na kuniziba pua na mdomo, nikasema tena kwa ujasiri na nguvu zaidi kama nilivyosema kwanza, likakimbia tena kwa hofu.  Nikagundua kwamba nikisema naenda na Yesu linaogopa sana na kukimbia.  Nikajipanga kama likija mara ya tatu nitasema kwa ujasiri na nguvu zaidi.  Lilipokuja mara ya tatu nikasema kwa nguvu na ujasiri zaidi, “Naenda na Yesu” Lilikimbia na kupotea kama ndege arukaye kwa kasi.

Yesu Atokea
Niliamka kitandani nione lile jitu limekimbilia wapi, nilipoamka nilikuta kumbe kuna mtu amesimama pembeni ya kitanda.  Alikuwa na vazi jeupe linalong’aa na kutingishika tingishika.  Katikati ya vazi hilo kulikuwa na mkanda uliong’aa na miguuni alikuwa na viatu vizuri ambavyo havifanani na viatu vya duniani, vilikuwa ni kama viatu vya kamba za ngozi.  Nywele zake zilikuwa nyeupe, lakini weupe wa aina yake tofauti na weupe wa vazi alilovaa;  Zilianguka mgongoni mwake.  Weupe wake haukufanana na weupe walionao binadamu wa kawaida. Huwezi kusema ni mzungu, muhindi mwafrika au mchina, alikuwa “neutral” Macho yake yalikuwa makali yanayong’aa.

Tukatazamana macho kwa macho nikamwangalia kwa makini.  Mara! akanyosha mkono wake wa kulia na kusema, “Ninyi mashetani mnataka mumfanye nini mtu huyu.” Nikashangaa likatoka lijitu lenye umbo la mwanaume lilikuwa refu na jeusi tii!  Wakati naendelea kushangaa likatoka lingine lilikuwa jeusi fupi na nene!  Nikajiambia mwenyewe kwa mshangao nilikuwa na watu ndani yangu! Walikaaje kaaje? Huyu mfupi mnene alikuwa akitembea na kuangalia nyumba huku anaondoka yule wa kwanza alikimbia haraka zaidi.  Baadaye nikaaacha kuyaangalia yale mashetani na kugeuka nitoe shukrani kwa Yesu, nikakuta ameshatoweka! Nilijisikia mwepesi sana, kichomi kikaisha na ugonjwa wa muda mrefu uliokuwa ukinisumbua ukaisha, Hofu ya kufa tokea hapo ikaisha.

Katika ushuhuda uliopita tunajifunza yafuatayo kwa neno la Mungu. Kwanza ni Yesu anaona kila kitu ndani yetu (Waebrania 4:12-13).  Alimkazia macho mtumishi wake kumbe ameona mashetani ndani yake. Kitu cha pili tunajifunza Yesu anayo mamlaka juu ya mashetani, alisema tu mnataka kumfanya nini huyu mtu na yakatoka. Leo tunapotumia jina lake anatenda kama yupo hapo hapo, jina lake mbele za mashetani ni yeye mwenyewe kwa kuwa lilipo jina lake na yeye yupo(Marko 9:37, Mathayo 18:20). Kama aliyauliza tu yakatoka na sisi tukiyaamuru kwa jina lake yatatoka (Marko 16:17). Kitu kingine tunachoweza kukiona katika ushuhuda huu ni kwamba pepo wanazo ngazi na vyeo. Hukaribishana ndani ya mtu.  Inawezekana kabisa yule aliyemtoka wa mwisho aliyekuwa mfupi ndiye aliyekuwa mkubwa, maana aliondoka huku akiangalia angalia alipotoka. Jambo lingine tunalojifunza ni kwamba si kila ugonjwa ni ugonjwa tu, mwingine ni mashetani yanakuwa yapo ndani ya mtu na yanasababisha kuumwa.

Nikaitafuta ile traks, niisome nione kama nitapigwa tena ngumi.  Nilisoma na kuimaliza  hakuna kilichotokea tokea wakati huo, ugonjwa ulionitesa miaka sita uliisha nikafunguliwa kabisa.  Siku hiyo aliponitokea Bwana nilisema, kuanzia sasa niwe mpole na mzuri kama aliyeniponya. Nikajiambia nitakuwa naenda kanisani na kuwa mtakatifu kama yeye alivyo.

Muda ulipita siku moja haya mashetani yalirudi tena. Yalianza kunishawishi niyakubali tukae nayo na yatanifanya niwe tajiri nisipate shida tena. Walinishawishi niachane na mambo ya kuokoka, Yalisema nimewahuzunisha mno ndugu zangu.  Wakati huu majitu haya yalikuwa yamevaa nguo kama za kijeshi.   Nikawajibu kwa ujasiri “hakuna kurudi nyuma” Waliondoka hawakurudi tena.

Katika ushuhuda uliopita tunajifunza kwamba Shetani hutumia heshima, Mali na watu wanavyotuona ili atupate.  Hata Yesu alimwambia akimsujudia atampa yote yaliyopo duniani (Mathayo 4:9).  Lakini Yesu ametufundisha akisema, uzima wa mtu haupo katika wingi wa vitu alivyo navyo (Luka 12:15).  Kuwa na mali na fedha hakutuokoi, Yesu ndiye utajiri, tukae kwake yeye aliye ufalme wa Mungu atatuzidishia yote (Mathayo 6:33).  Utajiri ulio nao mkubwa ni nafsi yako kutopotea kwa njia ya Yesu Kristo. Nafsi yako ina thamani kuliko vyote unavyoviona duniani! Kwa hiyo Shetani asikudanganye ukaiuza nafsi yako kwa kumwasi Mungu kwa vitu vyenye thamani ndogo kuliko wewe navyo ni mali na fedha. Hivi Bwana mwenyewe atatupa, ila hatutajiuza na kumfuata Shetani ili tuvipate..

No comments:

Post a Comment