Kutunza Huduma
“Mwambieni Arkipo,
iangalie sana huduma ile uliyopewa katika Bwana, ili uitimize”
(Wakolosai 4:17)
1. Unachofanya na Tabia
Lolote utendalo linadumu kwa njia ya tabia uliyo nayo. Ikiwa wewe ni mwanafunzi na una akili, tabia
yako inaweza kufuta kila kitu ukaonekana ni mpumbavu. Ikiwa wewe ni mfanyakazi na una ujuzi mkubwa
tabia yako yaweza kukuharibia sifa zako zote za ujuzi. Ikiwa wewe umeokoka au
ni mtumishi wa Mungu tabia yako ndiyo inayoshika huduma kama msingi, sio vipawa
na karama. Paulo alimwambia mtoto wake
wa kiroho Arkipo aiangalie sana huduma aliyopewa katika Bwana. Naamini njia
moja wapo ambayo angeweza kuiangalia ni kwa kujijengea tabia nzuri.
A. Nyumba na Msingi
Kama vile nyumba isivyoweza kusimama bila msingi, kazi yako
au huduma haiwezi kusimama bila tabia.
B.Mti na Mizizi
Kama vile mti hauna maana bila mizizi, huduma yako na ujuzi
wako wote hauna maana kama hujajenga tabia njema inayoambatana nao.
2. Jenga Tabia Kabla ya
Huduma
Kuna watu wakubwa na wenye nguvu na vipawa lakini havikuwasaidia,
hawakudumu kuwepo kwasabadu ya tabia; Mfano Sauli, Samson, Yuda Iskariote, nk (
Waamuzi 13:24-25, 14:1-19, 1Samwel 14:47-48, 1Samwel 15:1-24). Sauli alikuwa mfalme mwenye nguvu, tabia yake ilimwondoa
katika ufalme, kwa kukaidi kufanya alichotaka Mungu. Angeweza kuendelea kuwa
mfalme ikiwa tabia yake ingeendelea kuwa njema. Samson alikuwa na nguvu za
kupigana kwa uwezo wa Mungu, tabia yake ilimponza akatobolewa macho na nguvu
zake zikaisha. Angeweza kuendelea kuwa na nguvu ikiwa tabia yake ingeendelea
kuwa njema.
3.Jinsi ya kujenga
Tabia njema
1. Fahamu udhaifu wako na uuseme wazi mbele za Mungu,
usijifiche wala kujitetea (Waebrania 12:1).
2.Azimia kusema ukweli wakati wote, tabia kubwa ya Shetani ni
uongo (Yohana 8:44).
3.Tambua hakuna siri, chochote ufanyacho, mahali popote
unaonekana (Waebrania 4:13).
4.Watakie watu wote mema tokea moyoni na si kinywani tu
(Mathayo 7:12).
5.Uwe tayari kukosolewa na kurekebishwa(Waebrania 12:7-13).
6.Usiangalie kwa macho yako picha za uchafu, na kusikiliza
vitu vibaya, tabia hujengwa na kitu unachotazama mara kwa mara na kusikiliza
(Zaburi 101:3).
7.Soma Neno la Mungu na kulisikiliza wakati wote (Mithali
4:20-21).
8.Uwe na taadhari na rafiki anayekushusha moyo na kusema vitu
vibaya vya watu kila wakati(1Wakorintho 15:33).
9.Ufikirie mwili wa mtu wa jinsia tofauti nawe kuwa ni nyumba
ya Mungu inayoheshimika (1Wakorintho 3:16)
10. Usidhibitiwe na misukumo ya ndani kama hamu ya kula,
kutaka heshima, kutaka kujamiiana, hii ipo ila iko chini yako, isikuweze
(1Wakorintho 6:12, 10:23).
11.Uwe na nidhamu na tayari kuumia kwaajili ya malengo
uliyojiwekea (1 Wakorintho 9:25-27).
12.Tambua huwezi na hujui kila kitu, unamuhitaji mtu mwingine
(1Wakorintho 12:27)
Ufanyapo Haya na
Mengine atakayokuonyesha Roho Mtakatifu, utajenga tabia njema, kisha utadumu
kuwepo katika yale uyafanyayo, hutaishia njiani, kama ni katika huduma,
biashara au kazi.
No comments:
Post a Comment