Friday, April 24, 2015

Huduma ya Malaika



Malaika ni Watumishi Wetu
Katika tafsiri ya Kiyunani neno malaika (angelos) lina maana sawa na mtumishi aliyetumwa. Katika kitabu cha Waebrania imeandikwa maiaika ni roho waliotumwa kuwahudumu wale watakaourithi wokovu (1:14). Watakaourithi wokovu ni kina nani? Ni watu walio na Agano na Mungu kwa njia ya damu ya Yesu. Mtu yeyote aliyempa Yesu maisha yake analo Agano na Mungu kwa damu ya Yesu. Amekuwa mrithi wa Mungu. Malaika wapo ili wamuhudumie. Kama vile watu wasioamini wanavyotegemea mapepo, majini na mizimu ili wafanikiwe, watu wamwaminio Yesu inawapasa wamtegemee Mungu anayetumia malaika zake kuwahudumia.
Wanatumia  Neno la Mungu Kutumika
Malaika hutumia maneno kutenda. Jinsi tunavyoongea ndivyo tunavyohudumiwa na malaika. Malaika wanasikiliza Neno la Mungu na kulitenda (Zaburi 103:19). Wanafanya mapenzi ya Mungu ambayo ni Neno lake (Zaburi 103:20). Roho wa Mungu anapokupa Neno na ukaanza kulisema unawaachilia malaika walitende katika eneo au uhitaji husika . Unapotamka Jina la Yesu wanaachiliwa pia, maana wapo chini ya jina hilo ni watumwa wa jina hili kuu. Wachawi na waganga husema maneno mabaya na pepo huachiliwa kuyatenda. Wewe kama mtu wa Mungu sema maneno mazuri yaliyo sawa na Neno la Mungu na malaika wenye nguvu zaidi ya pepo wataachiliwa.
I.Malaika na Kazi au Biashara
Uzuri wa Mungu ni kibali chake kwetu. Malaika wa Mungu wanaweza kutumika kuachilia kibali au uzuri wa Mungu katika maisha yetu na katika yale tuyatendayo. Wanaweza kuleta kibali kwa wateja, waalimu au kwa mabosi kazini. Pepo wanaharibu kibali, lakini kwa njia ya malaika kibali au uzuri wa Mungu unakuwa juu yetu. Sema hivyo malaika watasikia na kutenda (Zaburi 103:17). Inakupasa kuitamkia kazi, masomo au biashara yako kwamba inathibitika na kusimama, Zaburi 90:17 inaonyesha hivyo. Unapofanya hivyo malaika wataachiliwa kwa kusikiliza maneno yako katika Bwana na kuithibitisha kazi yako kwa nguvu za Bwana.
II.Malaika na Ulinzi
Biblia inasema Bwana atakulinda uingiapo na utokapo, tena mabaya hayatatupata (Zaburi 121:8,91:10-11). Mabaya yoyote kama ni ajali, ujambazi, kupoteza viungo, kuumwa na nyoka nk, katika Bwana hayatupati. Tunapokuwa na tabia ya kuyasema maandiko haya malaika wa Bwana watakuwa kazini kuyatendea kazi na kutulinda. Watakusanyika makundi makundi na kutulinda na mabaya ya aina zote, yakiwemo magonjwa, dumu kusema hivyo usiseme mara moja au mbili (Zaburi  34:7).
III.Malika na Adui Zetu
Watu wanaotuchukia na kututegea mitego, malaika wanaitegua (Zaburi 35:5-8). Malaika wanafuatilia maadui zetu na kuhakikisha kile walichotutegea kwa siri hakisimami, tutamke hivyo tutaachilia malaika. Wanaponda watesi mfano wachawi na kupiga maadui mfano mapepo (Zaburi 89:20-23).
IV.Malaika na Mahusiano
Katika mahusiano kwa mfano ya kuunganisha mke na mume au kupata mchumba malaika wanahusika. Malaika alihusika kumsaidia Yusufu asimwache Mariamu(Mathayo 1:20). Isaka alipata mke kwa njia ya mtumishi wa Ibrahimu kuongozwa na malaika(Mwanzo 24:7). Unapotamka kwa jina la Yesu na kusema malaika wanakusaidia kumpata mwenzi aliyekusudiwa bila shaka utaachilia malaika wanaojenga mahusiano. Hata katika ndoa malaika wanahusika kusimamia ndoa. Unaposema katika jina la Yesu mwenzi wangu hataniacha maana imeandikwa mtu ataambatana na mume au mke malaika watatumia Neno hilo kuboresha ndoa yenu. Wachawi na washirikina hutumia pepo kuharibu ndoa. Mungu hutumia malaika kuiboresha.
V.Malaika na Watoto Wetu
Kuna malaika wanaosimama kwaajili ya watoto wetu(Mathayo 18:10). Yesu alisema kuhusu watoto ufalme wa Mungu ni wao. Ufalme ni haki, amani, furaha na mambo mengine ya Kiungu. Tunaweza kutamka kwa jina la Yesu na kusema malaika wanaachiliwa katika tabia zao wawaongoze katika tabia za kifalme. Pia tunaweza kuamuru mapepo yawaache waende kwa Yesu wakifundishwa na malaika zake tabia njema badala ya kufundishwa na pepo. Usiombe malaika watende hayo, tamka na kumwambia Mungu kwamba malaika wanatenda hayo. Hatuombi malaika tunamwomba Mungu atumiaye malaika. Baada ya hapo tunatamka Neno na malaika hulitenda.
VI.Malaika na Majaribu
Wakati wa majaribu malaika wanakuwa karibu nasi watutie nguvu. Yesu alipokuwa na majaribu malaika walikuwepo kumtia nguvu (Marko 1:13). Wakati wa majaribu tujizoeze kusema Bwana ni nani kwetu; yeye ni Mwokozi, ni ngome, ni kimbilio. Tumsifu kwa matendo yake makuu. Hali kama hii itawaachilia malaika watutie Nguvu na kufungua milango kama ilivyokuwa kwa Paulo na Sila (Matendo 16).
VII.Malaika na Maombi
Kanisa linapoomba malaika huachiliwa. Kanisa lilipomwomba Mungu kwaajili ya Petro malaika alitumwa na Mungu, Petro akafunguliwa. Tunapokutana na vikwazo tuombe kwa bidii huku tukitumia Neno la Mungu. Mungu atatuma malaika zake. Maombi mengi yanajibiwa kwa utendaji wa malaika (Matendo 12:6-7).
VIII.Malaika na Wokovu
Malaika wa Mungu wanashughulikia wagonjwa na wasiookoka wakati wa huduma. Unapohudumu katika mkutano au semina na kuamuru watu wapone na kuwasihi waokoke, malaika huwa pamoja na wewe. Mwinjilisti Filipo katika huduma yake aliambatana na utumishi wa malaika (Matendo 8:26).
IX.Malaika na Damu ya Yesu
Damu ya Yesu ni damu ya Agano. Inayo sauti katika ulimwengu wa roho. Ukiona kuna jambo lolote limefanyiwa agano la damu kwa mfano matambiko au uchawi. Tumia damu ya Yesu kubatilisha agano hilo. Damu itanena kazi yote ya msalaba na ukombozi. Malaika watasimamia ushuhuda huo maana ni watumishi na mashahidi wa kazi ya ukombozi ya Yesu. Kabla hajasulubiwa walikuwa naye(Luka 22:43)alipofufuka walikuwepo(Luka 24:23) inawezekana hata alipokomelewa misumari walikinga damu yake na  wanaifahamu.
X.Malaika Hufunga Mashetani
Unapoamuru na kusema kwa jina laYesu pepo wa udhaifu wa magonjwa au pepo yoyote katika anga afungwe. Malaika wa Mungu ndio hufanya kazi ya kufunga ingawa ni wewe unayeamuru. Malaika wanafunga vitu vibaya tunapoamuru na wanafungulia vitu vizuri tunapoamuru vitokee(Mathayo 18:19, Ufunuo 20:1-2).
Muhimu: Hakikisha umesoma maandiko yote yaliyotajwa hapa. Kisha anza kuamuru utendaji wa malaika. Wewe ni roho, unafanya kazi katika ulimwengu wa roho pamoja na malaika wa Mungu. 

CFM PUBLISHERS
P.O.Box 15634
Arusha. Tanzania
Simu:0784535424
bmwakatundu@yahoo.com

No comments:

Post a Comment