Wednesday, February 18, 2015

Yesu ni Mwokozi



Unaokolewa Ukiwa na Yesu
 Nani atakayewahukumu adhabu? Kristo Yesu ndiye aliyekufa; naam, na zaidi ya hayo, amefufuka katika wafu, naye yuko mkono wa kuume wa Mungu; tena ndiye anayetuombea.”
(Warumi 8:34)
Wokovu wetu katika Yesu Kristo unaonekana kwa mambo kadhaa aliyotutendea. Yatupasa kuyatafakari na kuyatamka mara kwa mara, ili kudhihirisha kushinda kwake. Maandiko yaliyotangulia kabla ya hili lililotajwa hapa, yanaonyesha uhusiano wa wateule wa Mungu na Mungu kwa njia ya Yesu. Kisha andiko hili likaanza kwa kuendelea kusema “ ni nani atakayewahukumia adhabu?” Halafu maandiko yanaendelea kusema mambo mengine, hebu tuyatazame kwa undani na tuyaweke wakati wote vinywani mwetu. Mambo haya manne ndiyo wokovu wako na kushinda kwako.
I. KRISTO YESU NDIYE ALIYEKUFA
Yesu alikufa kwasababu ya dhambi (1Wakorintho 15:3): 1. Alisulubiwa ili kuondoa nguvu ya dhambi kwa kusulubisha mwili wa dhambi 2. Damu ilimwagika kuondoa uwepo wa dhambi  3. Alikufa kundoa matokeo ya dhambi, yaani hasira ya Mungu 4. Kwa kifo chake alimwingilia Shetani na kumnyang’anya uwezo wa kutawala watu kwa njia ya mauti.
Sema: Yesu umeniokoa msalabani, Dhambi haina nguvu ya kunitawala, mwili wako uliharibu nguvu hiyo, dhambi haipo ndani yangu, damu yako imeniosha, hukumu haipo juu yangu kifo chako kimelipia hukumu yangu, Shetani hana nguvu kwangu, nguvu yake iitwayo mauti  imeharibiwa na wewe ulipokufa.
II.AMEFUFUKA KATIKA WAFU
Yesu amefufuka kwasababu ya haki (Warumi 4:25): 1.Amefufuka kwasababu ni mwenye haki, aliyeondoa dhambi kwa kifo chake 2. Dhambi haipo juu yake tena 3. Alipofanyika dhambi alikufa kwa dhambi zetu. 3. Alipofufuka anaishi kwa haki yake 4.Katika haki yake kuna uzima si mauti tena.
Sema: Nimekufa na Yesu katika dhambi, nimefufuka naye katika haki. Dhambi hazipo juu yangu tena kwa njia ya Yesu mwenye haki aliyefufuka. Nimefufuka pamoja naye katika haki yenye uzima wa milele, kwa uzima huo mimi ni kiumbe kipya ni mtu wa mbinguni sina dhambi!
III.YUKO MKONO WA KUUME
Yesu ameketi mkono wa kuume kwasababu ya UFALME (Waefeso 1:19-23): Baada ya kufufuka Yesu ameketishwa. Kuketishwa kuume kwa Mungu ni kama kuvishwa vyeo. Yuko juu ya majina yote, pia analo jina kuu kuloko yote. Chotechote chenye nguvu, uwezo, sifa au mamlaka kimewekwa chini yake. Yeye ni mtawala. 
Sema:Nimekaa pamoja na Yesu mkono wa kuume wa Mungu. Nipo juu ya majina yote pamoja na Yesu, ninalo jina kuu kuliko yote. Chochote kiwezacho kutawala mbinguni, duniani au kuzimu kipo chini yangu kwa njia ya Yesu Kristo. Nisemapo habari za Yesu duniani nasema kama mfalme aliyeketi na Yesu mbinguni. NATAWALA KWA USHUHUDA WA YESU DUNIANI NIKIWA MBINGUNI NA YEYE.
IV. NDIYE ANAYETUOMBEA
Yesu ameketi mkono wa kuume kwasababu ya UKUHANI (Waebrania 4:14-16): Yesu ni mwombezi au wakili wetu mbinguni (1Yohana 2:1-3).  Maisha yetu duniani anayawakilisha mbinguni mbele za Mungu. Tunapokuwa dhaifu duniani yeye ni nguvu yetu mbinguni. Yeye ni upatanisho wa maisha yetu na Mungu tukiwa hapa duniani. Ni msimamizi na shahidi wa imani na maungamo yetu mbele za Mungu. Ni shahidi wa kazi aliyoimaliza msalabani mbele za Mungu  kwaajili yetu.
Sema:Yesu ananiwakilisha mbinguni kama Kuhani mbele za Baba, mimi namwakilisha duniani kama kuhani mbele za dunia. Amenipatanisha mbinguni kwa damu, naupatanisha ulimwengu na Mungu kwa injili yake. Neno nilisemalo duniani kwa imani, analisimamia mbinguni kama mwombezi. Ninaye aliyetangulia mbinguni kwaajili ya yangu.
IKIWA UMEMPA YESU MAISHA YAKO WOKOVU WAKO UNAWEZA KUUISHI KATIKA MAENEO HAYA MANNE, YASEME, YAWAZE, YATEGEMEE, NGUVU YAKO YA KUSHINDA IPO HAPO; Kama bado hujampa Yesu maisha yako sema sala hii;
YESU INGIA NDANI YANGU,
KATIKA WEWE NASAMEHEWA DHAMBI NA MUNGU BABA.
NAAMINI ULIKUFA NA KUFUFUKA
KATIKA WEWE NAHESABIWA HAKI.
NAPATA UZIMA WA MILELE, NAOSHWA KWA DAMU YAKO.
NAAMINI IMEKUWA KAMA NILIVYOSEMA,
NI KATIKA JINA LAKO YESU, NIMEOKOLEWA.

No comments:

Post a Comment