Friday, January 16, 2015

Mtumie Yesu


Mtumie Yesu Kushinda Yote
Wakati wote upitiapo hali yeyote ya kushindana kibinadamu au kishetani, usisahau kutumia Nafsi ya Yesu Kristo, ni msingi wa kushinda. Jaribu ulilonalo ikiwa ni nyumbani, katika huduma au kazini limekuja ili ushinde si uangamie. Watu na Shetani watakuhukumu kwa yale unayopitia na kuona umeshindwa kwa vile waonavyo wao, lakini mwisho utaongea na kuonyesha kushinda kwako!
YESU NI NANI
Yesu ni Kristo Mwana wa Mungu  aliye hai (Mathayo 16:16).  Maneno haya alisema Petro, Akiitija nafsi ya Yesu.  Yesu alimjibu kwa kusema, “Nami nakuambia wewe ndiwe Petro, na juu ya mwamba huu nitalijenga kanisa langu wala milango ya kuzimu haitalishinda” (Msitari wa 18).  Milango ya kuzimu haiwezi kuishinda nafsi ya Yesu Kristo.  Mashauri yote ya kishetani hayawezi kuishinda.  Nyakati za Biblia milangoni palikua ni sehemu ya mipango ya miji na mashauri (Kumbukumbu 16:18, 21:19, Waamuzi 9:35). Baadaye  mabaraza ya wazee waliokuwa wakikaa milangoni na kufanya mashauri na yenyewe pia yaliitwa milango.  Kwa hiyo milango ya kuzimu yaweza kumaanisha mashauri yote, mikakati yote ya kishetani, na hila zote.  Hizi haziwezi kushinda nafsi ya Kristo Mwana wa Mungu aliye hai. 
MANENO YAONYESHAYO NAFSI YA YESU
Usomapo maandiko hasa Injili nne, tafuta maandiko ambayo Yesu alijitambulisha nafsi yake, Kwa mfano “mimi ndimi…” au  Ajae kwangu ….”  “… Yangu” Maneno hayo yanamtambulisha Nafsi yake ikoje, yeye ni nani na ana nini.  Katika hayo Shetani hana kitu wala mashauri yake ya kuzimu.  Unapoombea hali fulani kishetani simama katika kweli, Nafsi ya Kristo Yesu, utamiliki na kushinda, mtaje Yesu ni nani katika tatizo hilo.
YESU ALIFANYA NINI MSALABANI?
Katika Wakolosai 2:15, maandiko yanasema Yesu msalabani alizivua enzi na mamlaka.  Kuzivua kwa tafsiri ya Kiyunani ni “Katargeo”, maana yake ni; kuzifanya sio kitu, kuzifanya sifuri,kuzipoozesha na kuzinyang’anya silaha.  Utendaji wowote wa kishetani katika mawazo, hali zinazokuzunguka, ua watu haziwezi kushinda nafsi ya Kristo aitwaye Yesu aliye ndani yako.  Msalaba umefanya hayo yote yaliyo ya shetani kuwa si kitu.
YESU ALIISHIJE DUNIANI
Yesu aliishije duniani? Aliishi kwa kushinda, alishinda kila hila ya Shetani.  Maandiko yanasema alijaribiwa katika mambo yote bila kufanya dhambi!(Waebrania 4:15).  Shetani alimjaribu katika mawazo yake, hali, na kupitia watu, Yesu hakutenda dhambi.
Adamu na Eva walishindwa kwa tamaa ya mwili, tamaa ya macho na kiburi cha uzima (Mwanzo 3:1-8).  Yesu aliushinda ulimwengu (Yohana 16:33).  Aliushinda na mambo yaliyo ndani yake, yaani tamaa ya mwili tamaaya macho na kiburi cha uzima (1Yohana 2:13-17).
Hii (Tamaaya mwili, tamaa ya macho na kuburi cha uzima).  Ni milango ya hila za kishetani kwenye maisha ya binadamu, Yesu alizishinda pale mlimani wakati wa maombi ya siku arobaini.   Eva  na Adamu walishindwa. 
Katika nafsi ya Yesu tunashinda sasa,Yesu ndiye tafsiri ya kweli katika yote tukutanayo nayo.  Katika yote yanayotutokea, ukweli ni Yesu ni nani katika hali hizo, alifanya nini msalabani na aliishije duniani na kushinda.  Katika hali tukutanazo nazo tuitaje Nafsi ya Kristo na neema ya kushinda uongo itatokea.  Hata kama unaona unakufa huo ni uongo, ukweli ni Yesu ufufuo na uzima (Yohana 11:25).  Hata kama unaona unashindwa ni uongo, ukweli ni kwamba Yesu aliye ndani yako ameshinda ulimwengu na yote yaliyopo ndani yake (Yohana 16:33).
Kipaumbele chako wakati wote ukisahau vitu vyote, Usimsahau Yesu ni nani, aliishije duniani, alifanya nini msalabani, kisha mtaje katika mazingira yako. Ukifanya hivyo Yesu atasimama kama Kuhani wako mbinguni kwa yele uyasemayo duniani.

No comments:

Post a Comment