Thursday, August 7, 2014

Shika kwa Ndani si kwa Mkono



KATECHO
Jaribuni mambo yote lishikeni lililo jema (1 Wathesalonike 5:21)
Na tulishike sana ungamo la tumaini letu,  lisigeuke; maana yeye aliyeahidi ni mwaminifu (Waebrania 10:23)
Kwa maana tumekuwa washirika wa Kristo, kama tukishikamana na mwanzo wa uthabiti wetu kwa nguvu mpaka mwisho (Waebrania 3:14)
Na zile penye udongo mzuri, ndio wale ambao kwa unyofu na wema wa mioyo yao hulisikia  neno na kulishika; kisha huzaa matunda kwa kuvumilia (Luka 8:15)
KUSHIKA
Kati ya maneno ya Kiyunani yaliyotumika katika Agano Jipya yenye maana ya kushika ni “Katecho”.  Kushika kunakotajwa kwa neno hili huleta matokeo kwa kile tunachotaka kitokee au kizaliwe. Kama unataka kuendelea na wokovu bila kurudi nyuma inakupasa ‘kushika’ jambo fulani.
Kushika huku kunakotajwa hapa ni: Kung’ang’ania, kutunza, Kukaa pale pale au kuwa na mwelekeo ule ule.  Utagundua kwamba kushika huku sio kushika kitu kwa mkono! Ni kuwa na msimamo thabiti wa ndani usioyumba kuhusu jambo fulani.
Andiko la kwanza hapo juu linaonyesha yatupasa kuthibitisha kila jambo (kujaribu) na kulishika lililojema, mfano tunapothibitisha Neno la Mungu linasema nini maishani mwetu, yatupasa kulishika katika fahamu, kuling’ang’ania, kulitunza na kutokubali kulipindisha katika vinywa vyetu, HATA KAMA ZINATOKEA HALI HALALI ZA KULIPINDISHA.
Tunalo tumaini la uzima wa milele katika Yesu Kristo. Yeye kama kuhani wetu ametangulia mbinguni kutuandalia makao na anatuombea. Hata hivyo tutakutana na hali tatanishi ambazo zinaweza kuvunja matumaini ya kumwona Mungu. Maandiko yanaonyesha, Waebrania 10:23, yatupasa kushika ungamo la tumaini letu lisigeuke. Kushika hapa ni kutotoka katika mwelekeo sahihi wa tumaini letu katika imani ya Yesu, kuwa na mtazamo mmoja katika fikra usiogeuka ambao unaongoza kinywa chetu kusema kitu tunachoamini mpaka mwisho bila kugeuka.
Kuokoka ni kuwa washirika wa Kristo, Ili kuendelea na ushirika huo inatupasa kushikamana na ujasiri tuliokuwa nao mwanzo ndani ya Yesu toka tuokoke mpaka mwisho (Waebrania 3:14). Ushirika na Kristo unaendana na kuwa na uthabiti wa imani na ujasiri kwamba tumeokoka na Kristo yupo upande wetu. Hali hii ni chachu ya kutufanya tuendelee kushirikiana naye. Inapaswa ishikwe ndani yetu, tuing’ang’anie hata mwisho, tukifanya hivi ushirika wetu na yeye hautakufa.
Neno la Mungu yatupasa kulisikia au kulielewa na kulishika, huku ni kulipa kipaumbele katika fikra na ndimi zetu, kisha kuwa na subira ya kuona udhihirisho wake. Neno lizaalo matunda ni neno linaloshikwa, linalong’ang’aniwa, linalotazamwa wakati wote katika fikra, linaloshindaniwa kinyume na hali zinazozunguka, kisha kwa ustahimilivu na uvumilivu huzaa matunda.
WAKATI WOTE TEGEMEA NEEMA YA MUNGU KUKUWEZESHA KUSHIKA MAMBO YA KI-MUNGU, KUYA-‘KATECHO’ ILI YAZAE MATUNDA, MBELE ZA UPINZANI NA USHINDANI UNAOKUZUNGUKA. USIYAACHIE YASHIKE.

No comments:

Post a Comment