Wednesday, June 25, 2014

Shindania Kushinda Kwake




Kushindana na Shetani
Maana ya jina Shetani ni adui, au mpinzani.  Baalam alipopingwa na malaika (Hesabu 22:22), malaika yule alifanya kazi kama Shetani (ingawa hakuwa Shetani, ila kupinga huku ni kama afanyavyo Shetani).  Shetani ni adui anayepinga.  Anapinga Uungu usionekane.  Maahali popote palipo pema atapapinga na kuleta ubaya. Palipo na nuru atapinga na kuleta giza. Palipo na kweli atapinga nakuleta uongo, palipo na uzima atapinga na kuleta mauti.  Maandiko yanasema Mungu alimwondokeshea Sulemani adui mwingine aitwaye Rezoni (1 Wafalme 11:23).  Adui huyu alimpinga Sulemani, kama Shetani afanyavyo.  Roho ya mpinga Kristo (1Yohana 4:3), ni roho ya Shetani, inapingana na Mungu na uungu duniani (2 Wathesalonike 2:3-4).
Yesu  alishamshinda Shetani kwaajili yetu (1Wakorintho 15:57). Amemshinda na ametupa kushinda kwake. Kumshinda Shetani huku ni kushinda ushetani, yaani upingamizi wake. Hata hivyo Adui amebaki na kitu kimoja kinaitwa HILA. Kwa Kiyunani hila ni methodaeias, tafsiri yake ni mbinu za kulaghai na kutega mitego.  Silaha tunazivaa ili kupinga hila na sio nguvu za Shetani, Shetani nguvu hana kwa njia ya Yesu. Yesu alimharibu kabisa msalabani! Hatupigani naye, Yesu alishapigana naye akamshinda.  Sasa tunashindania ushindi wake, tunahakikisha unasimama wakati wote, hatuutafuti tunao, tunashindana usimame wakati wote.
YESU AMESHASHINDA TUNAUSHINDANIA USHINDI WAKE
                                                   Kanunu za Kushindania Ushindi                
1.Kutii na Kupinga : Yakobo 4:7-8, 1Petro 5:7-9
Wakati wote kaa chini ya mamlaka ya Yesu. Tenda asemayo, ishi kwa upendo, Kwa kufanya hivi mamlaka yake itadhihirika kwako ukimpinga Shetani, atakimbia. Ukipinga upingamizi wake atakimbia.
2.Kufahamu uwanja wa Mapambano: 2Wakorintho 11:3, 2Wakorintho 10:3-4
Kanuni moja ya vita ni kujua adui anapigania wapi. Shetani hupingana nasi kwa kupitia mawazo na fikra zetu. Hulenga mfumo wa mawazo. Ukiweza kumshinda katika mawazo yako hataweza kukupata. Akikupata mawazo yako amekupata maisha yako. Mpinge katika mawazo kwa kusema kitu kwa kinywa, si kwa kuwaza neno tu, bali kwa kulisema. Usemapo neno kinywani linashinda mawazoni.
3.Kufahamu Silaha Yako: Waefeso 6:17
Maandiko yameonyesha silaha kadhaa, silaha zote zinamsingi wa Neno la Mungu. Kama vile meli inavyotegemea nanga, wakati wa mawimbi, Neno lisiache kutoka kinywani mwako, wakati wa misukosuko tu, linashinda tu. Luka 4:1 -11, inaonyesha Yesu alidumu kusema Neno la Mungu, Shetani alipokuwa akimjaribu au kumpinga. Alidumu na Neno kinywani mpaka Ibilisi akamwacha, kisha malaika wakamuudumia. Udumupo kusema neno mpinzani atakuacha mbinguni watakuudumia.
4.  Walio Upande Wako: Warumi 8:31, Zaburi 118:7
Katika mawazo yako mwone Mungu yuko upande wako, Shetani anayekuchukia ameshindwa (Zaburi 118:7).  Malaika walio upande wako ni wengi kuliko mashetani. Kanisa la Yesu au waliookoka wako upande wako, wana mamlaka kubwa kuliko Shetani.  Yesu aliye ndani yako ni mkuu kuliko Shetani!
5. Kufahamu Nafasi Yako: Waefeso 2:5-6
Yesu yupo juu ya kila kitu (Waefeso 1:19-23), Upo juu ya kila kitu pamoja naye (Waefeso 2:5-6). Mashetani wote na hila zao zipo chini ya kinywa chako, Yaani neno usemalo.
6. Kukaa katika Roho: Waefeso 6:18, Yohana 4:23
Unamshinda Shetani kwa kukaa katika Roho Mtakatifu. Unapokaa katika ufunuo wa Roho katika kulijua neno, Unapodumu kuomba kwa Roho Mtakatifu, Unapoishi kwa tunda la Roho na si matendo ya mwili.  Unapomwabudu Mungu kwa nguvu za Roho Mtakatifu. Wakati wote unapokuwa na ushirika na Roho kwa kuongea naye, ni wakati kwa kumshinda adui.
7. Kukaa katika Agano: Yohana 10:28, Yohana 6:37
Shetani hawezi kukutoa katika agano lako na Mungu kwa njia ya Yesu.  Upo mikononi mwa Yesu hakuna awezaye kukutoa hata kwa hila, mtazame Yesu aliye ndani yako na kushinda.

1 comment: