Sunday, June 2, 2019

MEZA YA BWANA::SEHEMU C: I. UMUHIMU WA MEZA YA BWANA


SEHEMU C:
I. UMUHIMU WA MEZA YA BWANA
Kuna mambo kadhaa ambayo yatupasa kuyajua au kuyafikiri na kuyasema tunaposhiriki meza ya Bwana. 
UTII


1. Tunashiriki meza ya Bwana ili kumtii na kumuheshimu Yesu, maana ameagiza tuifanye kama wanafunzi wake, Tunamwonyesha utii wa moja kwa moja. Maana aliagiza kwa kusema tufanye hivyo kwa ukumbusho wake, “Akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema, Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwa ajili yenu, fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (Luka 22:19).

AGANO
2. Agano kati ya Mungu na watu haliwezi kufanyika bila sadaka yenye mwili na damu. Meza ya Bwana ni alama kubwa ya muunganiko wetu na Mungu katika ushirika wetu na Yeye. Ushirika wetu na Mungu ni kwa kupitia mwili na damu ya Yesu, Mungu hukaa nasi kwa agano lake katika mwili na damu ya Yesu. Meza ya Bwana inachochea ufahamu huu, kutoshiriki meza ya Bwana mara kwa mara hutufanya tupoteze ufahamu wa muunganiko wetu na Mungu kiagano kwa mwili na damu, ulio juu ya agano lingine lolote katika ulimwengu wa roho. “kwa maana hii ndiyo damu yangu ya agano, imwagikayo kwa ajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi.” (Mathayo 26:28), “Kikombe nacho vivyo hivyo baada ya kula; akisema, Kikombe hiki ni agano jipya katika damu yangu, inayomwagika kwa ajili yenu” (Luka 22:20).

UKUMBUSHO
3. Yesu alisema tufanye kwa ukumbusho wake. Wakati wa ushirika mtakatifu ni wakati wa kukumbuka kazi yote ya Yesu. Alifanyika dhambi kwa ajili yetu ili sisi tuwe haki kwa njia yake. Alimharibu Shetani msalabani kwa ajili yetu. Ni kuhani wetu tunaposhiriki meza ya Bwana yatupasa tufanye na maombi ya shukrani kwa kumkumbuka aliyetutendea mambo yote vema. Shetani hapendi kitu hiki ndio maana hatumaanishi kuhusu meza ya Bwana. Bila shaka kuna ngome zinatumika katika mawazo kutuzuia tusishiriki mara kwa mara au kabisa, “Akatwaa mkate, akashukuru, akaumega, akawapa, akisema, Huu ndio mwili wangu unaotolewa kwaajili yenu, fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (Luka 22:19). 
TANGAZO
4. Chakula cha Bwana ni tangazo la mauti ya Yesu hata ajapo, “Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo” (1 Wakorintho 11:26). Kifo cha Yesu kilitoa damu ya ukombozi, ikiwa na maana ya kifo cha Yesu kimelipia kifo chetu kilicho tangazwa na torati. Yesu alipokufa alimharibu aliyekuwa na nguvu za mauti juu yetu. Kifo cha Yesu kimefunga agano la kale na kufungua jipya, ishara ilikuwa pazia la hekalu lilipasuka na njia ya kupaingia patakatifi pa patakatifu ikapatikana kwa mwili wa Yesu. Kifo cha Yesu kilimpeleka Yesu kuzimu na akatoka na funguo za mauti na za kuzimu. Kifo cha Yesu kimeleta kufufuka kwa Yesu, haya ni maisha mapya ya agano jipya. Kifo cha Yesu kimeua sheria ya Musa na kuleta imani ya Yesu. Haya yote tunayatangaza tunaposhiriki mwili na damu ya Yesu. Huwezi kuniambia sio muhimu kuyasema haya kwa njia ya kushiriki mwili na damu ya Yesu mara kwa mara. Bila kushiriki mwili na damu mara kwa mara kwa njia ya kuweka imani zetu katika yale Yesu aliyoyasema na kufanya msalabani, maisha ya kanisa yatakuwa ya kawaida. Kwa njia ya kushiriki kutakuwa na nguvu ya kuliendesha kanisa kiagano na kwa ushirika wa Roho Mtakatifu. 

NJIA
5. Yesu alipochukua mkate aliumega, kwa lugha nyingine aliuvunja, aliuharibu. “naye akiisha kushukuru akaumega, akasema, Huu ndio mwili wangu ulio kwaajili yenu; fanyeni hivi kwa ukumbusho wangu” (1 Wakorintho 11:24). Kuharibiwa kwa mwili wa Yesu ni njia pekee ya kumkaribia Mungu tuliyopata, “Basi, ndugu, kwa kuwa tuna ujasiri wa kupaingia patakatifu kwa damu ya Yesu njia ile aliyotuanzia iliyo mpya, iliyo hai, ipitayo katika pazia yaani mwili wake.”(Waebrania 10:19-20). Andiko hili linaonyesha damu na mwili wa Yesu kama njia ya kumkaribia Mungu. Tunamkaribia Mungu kwa damu kupitia mwili wake. Tafsiri ni hii, huwezi kumkaribia Mungu bila kuwa na damu, hapohapo huwezi kwenda na damu bila kupitia mwili wake. Unaposhiriki mwili wa Yesu, uliovunjwa msalabani kwa kutumia damu, unafika Mungu alipo na kupokea alivyonavyo, Pia kutoa ulivyonavyo na kumpa Yeye. Udhaifu ulionao unapeleka kwake, na nguvu alizo nazo anakupa wewe kwa njia ya mwili wa Kristo. Msalabani mwili wake ulikuwa dhaifu kama mwili wako. Alipofufuka mwili wake una nguvu ya kukutia nguvu mwili wako. Mwili wa Kristo ni njia ya kumkaribia Mungu na mabadilishano ya nguvu na udhaifu hutokea.

TUMAINI
6. Yesu alisema hatakunywa mzao wa mzabibu hata ajapo “Maana nawaambia ya kwamba tangu sasa sinywi mazao ya mzabibu hata ufalme wa Mungu utakapokuja” (Luka 22:18). Meza ya Bwana hutupa tumaini kwamba siku moja akirudi atatuchukua na tutaenda kula nae karamu ya Mwana kondoo mbinguni. Hii (meza ya Bwana) ni chombo kinachozishika imani zetu kumngojea. Tunajitakasa na kuishi kama wageni katika dunia hii tukijua siku moja tutamwona na kuishi naye milele. Meza ya Bwana ni chombo cha kumsubiria Yesu.

KWELI
7. Yesu alisema mwili wake ni chakula cha kweli na damu yake ni kinywaji cha kweli (Yohana 6:55). Mwili wa Yesu na damu yake ni chakula cha uhakika, ndani yake hamna uongo. Moja ya sifa kubwa ya Shetani ni baba wa uongo. Mwili na damu ni kweli, inayoonyesha nguvu juu ya uongo wowote wa kishetani katika maisha yetu, uliojificha au ulio wazi. 

MUUNGANIKO
8. Kama vile ulapo chakula cha kawaida kinaunganika na maisha yako na kinaathiri mwili wako wote. Mwili na damu ya Yesu unatuunganisha na Yesu na tunayashiriki aliyonayo yanakuwa sehemu yetu, kwa Imani tayari tumeunganishwa na Yesu na kumshiriki, meza ya Bwana ni kichocheo cha kutukumbusha haya kiimani “Aulaye mwili wangu na kuinywa damu yangu hukaa ndani yangu nami hukaa dhani yake. Kama vile Baba aliye hai alivyonituma mimi, nami ni hai kwa Baba, kadhalika nay eye mwenye kunila atakuwa hai kwa mimi” (Yohana 6:56-57). Uhai wa Yesu ndio uhai wa Mungu Baba, alipokuwa duniani walikuwa mmoja na ni mmoja hata sasa. Uhai wetu na Yesu ni mmoja kwa njia ya mwili na damu ya Yesu, uhai wa kanisa ni katika mwili na damu ya Yesu. Tunaposhiriki mara kwa mara na kusema hivyo, tutakuwa tunaziamsha imani zetu katika muunganiko na Kristo kati yetu wakati wote.

UFUFUO 
9. Yesu anasema aulaye mwili wake na damu yake anao uzima wa milele naye atamfufua siku ya mwisho (Yohana 6: 54). Alama moja kubwa ya injili katika agano jipya ni ufufuo. Ipo siku watu wote watafufuliwa, katika ufufuo wa kwanza wa wenye haki na uufufuo wa pili wa wenye dhambi. Ufufuo wa kwanza ni wa wale walio na imani katika Yesu na kuokolewa. Meza ya Bwana inaonyesha kwa kumwamini Yesu kama Bwana na Mwokozi tuna uzima wa milele ndani yetu, na siku moja tutafufuliwa na Yeye katika uzima wa milele. 

Meza ya Bwana sio mwili na damu ya Yesu halisi, ni alama ambayo inazifanya imani zetu zishike damu halisi na mwili halisi wa Yesu. Ili meza ya Bwana iwe na maana ni lazima, imani iwepo kwa kusikia neno la Kristo kuhusu mwili na damu yake. Tunaitenda kwa kumtii Bwana wetu Yesu , namna yoyote ya kuipuuzia ni kupuuza alichosema Yesu. Tukumbuke aliyesema ni Bwana wa mabwana na Mfalme wa wafalme, hivyo tumtii!

SHUKRANI
10. Ni vema meza ya Bwana iambatane na shukrani na maungamo ya imani kwa ukombozi. Kitu cha kwanza alichofanya Yesu alipouchukua mwili (Mkate) na kikombe (Damu) alishukuru, na kubariki “…Yesu alitwaa mkate, akabariki, akaumega, akawapa wanafunzi wake, akasema, Twaeni, mle; huu ndio mwili wangu.Akakitwa kikombe, akashukuru…”( Mathayo 26:26-27). Mwili na damu ya Yesu ni alama za shukrani mbele za Mungu, kwa ajili ya ukombozi wetu. Tunamshukuru mara kwa mara. Mara nyingi tunaomba sana Mungu atufanyie hili na lile. Namna ya kushukuru sana na vizuri ni kwa kutumia meza ya Bwana. Tunashukuru kwa yale aliyokwisha tufanyia, shukrani hizi zenyewe ni sadaka ni dhabihu (1Petro 2:9). 

Kumbe! wakati wa kushiriki meza ya Bwana ni wakati wa kutoa dhabihu mbele za Mungu, yaani shukrani, Hapa ndipo jina la Eukaristi, lilipotokea, yaani shukrani.

KUFAHAMU
11. Yesu alipokuwa anamega mkate na kushukuru, ndipo macho ya wanafunzi wake yakafumbuka wakamfahamu “Ikawa alipokuwa ameketi nao chakulani, alitwaa mkate, akaubariki, akaumega, akawapa. Yakafumbuliwa macho yao, wakamtambua; kisha akatoweka mbele yao…Nao waliwapa habari ya mambo yale ya njiani, na jinsi alivyotambulikana nao katika kuumega mkate”(Luka 24:30-31,35). Yesu kabla mwili wake haujaharibiwa msalabani mlango wa wanafunzi kumfahamu ulikuwa umefungwa. Alipokufa na kufufuka Roho akaja, hapa ndipo ilikuwa chanzo halisi cha kuanza kumjua. Katika maandiko hayo tuliyoyasoma tunaona hali hiyo ya picha, alipomega mikate macho yao yakafumbuliwa wakamtambua. Meza ya Bwana ni alama ya kumjua Yesu kwa Roho ya ufahamu katika Roho Mtakatifu. Mara nyingine dai kuzidi kumfahamu Yesu kwa ufahamu wa rohoni, pale unapokula mkate yaani mwili wake. 
SHEREHE
12. Yesu alipoanzisha meza ya Bwana ilikuwa ni kipindi sherehe ya pasaka na mikate isiyotiwa chachu (Kutoka 12). Pasaka ilikuwa sherehe ya kukumbuka ukombozi wa Israeli toka ufalme wa Misri. Meza ya Bwana ni sherehe ya kukumbuka ukombozi wetu toka ufalme wa giza hivyo kufurahi na kushukuru. 


Saturday, April 20, 2019

MEZA YA BWANA::SEHEMU B: I. YALIYOMO NDANI YAKE

Meza ya Bwana ina mambo kadhaa ndani yake:

AGANO JIPYA

Agano la Kale lilianzwa kwa damu ya kondoo wa pasaka kumwagika na torati kutolewa katika mlima Sinai. Alama yake kwa Waisraeli ilikuwa ni tohara.

Agano jipya limeanza kwa damu ya Yesu ilipomwagika, na Roho Mtakatifu kuja kwa wanadamu. Alama yake ni kuzaliwa mara ya pili, roho zetu kufanywa upya kwa njia ya Imani zetu kwa Yesu, “Kwa kuwa ninyi nyote mmekuwa wana wa Mungu kwa njia ya Imani katika Kristo Yesu.” (Wagalatia 3:26).

Damu ya Yesu ni damu ya Agano Jipya imwagikayo kwa ajili ya ondoleo la dhambi. Kwahiyo tunaposhiriki mwili na damu ya Yesu twalionyesha Agano Jipya. “kwa maana hii ndiyo yangu ya Agano, imwagikayo kwaajili ya wengi kwa ondoleo la dhambi”(Mathayo 26:28). Tunaposhiriki meza ya Bwana twalionyesha Agano la Ibrahimu na pia Baraka ya Ibrahimu. Hii ni kwa Mataifa yote kwa njia ya Yesu Kristo. Baraka hii inaonekana sehemu mojawapo katika Agano jipya, inaonekana kuwa ni kuepusha dhambi au kumgeuza kwa njia ya Yesu, “Ninyi mmekuwa watoto wa manabii na wa maagano yale, ambayo Mungu aliagana na baba zenu, akimwambia Ibrahim, katika uzao wako kabila zote za ulimwengu zitabarikiwa. Mungu, akiisha kumfufua mtumishi wake Yesu, alimtumakwenu ninyi kwanza ili kuwabarikia kwa kumwepusha kila mmoja wenu na maovu yake” (Matendo 3:25-26). Baraka ya Ibrahimu kwa kupitia Uzao Yesu Kristo imetokea kwa njia ya Yesu kufufuka, kwa Yesu kufufuka tumepata ondoleo la dhambi na tumegeuzwa toka katika dhambi. Yote aliyoyapata Yesu kwa kufufuka ni Baraka aliyoahidiwa Ibrahim, inawafikia Mataifa yote kwa Imani katika huyu Yesu ndani ya neno la injili. Meza ya Bwana imeyashika yote haya, katika Agano Jipya!

Tafrisi nyingine ya neno hili ondoleo la dhambi ni Baraka ya Ibrahim, maandiko yanasema Mungu akiisha kumfufua yesu katika watu alimtuma ili kutubarikia Baraka ya Ibrahimu kwa kumwepusha kila moja wetu na dhambi zake, kitu ambacho damu ya Yesu iondoayo dhambi zote kwa kila amwaminie. Damu hii pia ni ya agano jipya, utimilifu wa Baraka ya Ibrahimu upo Agano Jipya katika mzao Yesu Kristo kwa mwili na damu yake .

KUTANGAZA MAUTI

Mauti ya Yesu msalabani imelipia maisha yetu yote. Imelipia maisha yetu yaliyopita, ya sasa na yajayo. Imemuharibu Shetani kabisa. Hukumu ya dhambi haipo juu yetu tena, Yesu alipouwawa alilipa hukumu yetu ya kifo kwaajili ya dhambi zetu. Tulitakiwa na sheria tufe kwaajili ya dhambi zetu. Yesu akafanyika dhambi zetu akafa badala yetu.

Kutangaza mauti ya Yesu ni kutangaza ushindi wake na ukombozi wake mpaka ajapo. Kuhusu kutangaza mauti yake imeandikwa, “Maana kila mwulapo mkate huu na kukinywea kikombe hiki, mwaitangaza mauti ya Bwana hata ajapo” (1Wakorintho 11:26). Neno kutangaza hapa linamaana ya kuonyesha mauti ya Yesu hata ajapo. Mauti ya Yesu msalabani imetulipia kila kitu, mbele za Mungu, sheria na Shetani. Kuitangaza kila mara ni ujenzi na uthabiti mkubwa wa Imani zetu. Kutotangaza mara kwa mara mauti ya Yesu ni kutojali alichotufanyia. Kutangaza huku kunaambatana na shukrani za mara kwa mara kupitia meza ya Bwana tunayoishiriki mara kwa mara. Andiko hili liliposema kila “mwulapo mkate” kwa tafsiri ya Kiingezera ina maana mara kwa mara muulapo mkate, mwaitangaza mauti ya Bwana. 

Kutangaza mauti ya Kristo ni kutangaza mwisho wa utawala wa Shetani, ni kutangaza mwisho wa utawala wa sheria, ni kufunga mwisho wa utawala wa mwili wa dhambi au tamaa, ni kutangaza kufufuka kwa Yesu katika wafu. Tangazo hili lipo tunaposhiriki meza ya Bwana.

MARA KWA MARA

Kama tulivyoona, Kila mwaka wana wa Israeli walishiriki sikukuu ya pasaka. Hii ilikuwa sura ya ukumbusho wa ukombozi wao. Kwa upande mwingine mara kwa mara walikula mana, ndani ya kila masaa ishirini na nne, picha zote hizi mbili zinabeba meza ya Bwana.

Katika Matendo 20:7 imeandikwa, “Hata siku ya kwanza ya juma, tulipokuwa tumekutana ili kumega mkate, Paulo akawahutubu…”. Siku ya kwanza ya juma ilikuwa ni Jumapili. Inaonekana Kanisa lilikuwa na utaratibu wa kushiriki meza ya Bwana kila siku ya kwanza ya juma. Hapa anasema walikusanyika siku ya kwanza ya juma ili kuumega mkate. Sababu moja wapo ya wao kwenda kukusanyika ilikuwa ni kumega mkate. Kwa maana hii inaonyesha walishiriki mara kwa mara.

Imeandikwa tena, “Wakawa wakidumu katika fundisho la mitume, na katika ushirika, na katika kuumega mkate na katika kusali” (Matendo 2:42). Angalia mambo ambayo kanisa hili lilidumu au lilifanya wakati wote: Fundisho, ushirika, meza ya Bwana, Maombi. Kwa kuongezea angalia na andiko hili, “Na siku zote kwa moyo mmoja walidumu ndani ya hekalu wakimega mkate nyumba kwa nyumba na kushiriki chakula chao kwa furaha na kwa moyo mweupe.” (Matendo 2:46). Angalia na hapa neno hili “sikuzote”, linataka kufanana na lililopita “wakidumu”. Hii inaonyesha walishiriki meza ya Bwana mara kwa mara.

Ni wapi ambapo walishiriki? Walishiriki katika masinagogi na nyumba kwa nyumba. Meza ya Bwana inaweza shirikishwa kanisani au hata nyumbani. Hapa sitoi mwongozo au sheria bali mlango wa mtu kuweza kuitumia mara kwa mara. Agano la Kale sikukuu ya Pasaka ilianzwa kufanyika nyumbani. Baba, yaani kiongozi wa familia ndiye aliyehusika na maandalizi na usimamizi wa sikukuu ya Pasaka na mikate isiyotiwa chachu. Sio kitu kibaya ikiwa nyumbani wote mmeamini na mnaishi katika Bwana kushiriki pamoja mwili na damu ya Yesu.

Somo hili linaendelea, jiunge nasi kila wiki na kila siku kwa masomo mengine mbali mbali katika blog hii. karibu kwa Maswali, Maoni na Wajulishe Wengine, Tujifunze na kukua pamoja. 
Barikiwa.

Sunday, April 14, 2019

MEZA YA BWANA::SURA ZA MEZA YA BWANA

Meza ya Bwana ni alama kubwa ya Agano kati ya Mungu na Kanisa, ni nguzo ya kiimani katika ushirika huu. Kwa msingi uhusiano huu na ushirika umeanzia msalabani, Yesu alipotoa mwili na damu yake. 

Hakuna namna yoyote ya ushirika wa Mungu na watu, ila ni kwa njia ya msalaba tu! Hakuna kitu chochote tuwezacho pata toka kwa Mungu, bila msalaba wa Yesu, ambao ulitoa mwili na damu yake kwa ajili ya ukombozi wa maisha yote ya mwanadamu. Mwili huu na damu hii, twaiona kwa njia ya mkate na divai katika meza ya Bwana.

KAZI ZA MSALABA

Ili tupate mwanga zaidi wa somo hili kwa kifupi nitaelezea kazi za msalaba kwa kupitia mwili na damu ya Yesu, ili uzidi kuona umuhimu wake. 

KIFO

Maandiko yanasema, “Kwa maana mshahara wa dhambi ni mauti…” (Warumi 6:23). Mshahara wa dhambi ni kifo, au malipo ya dhambi ni kifo. Torati ilitaka dhambi ilipiwe kwa kifo. Baada ya kifo kutokea kwaajili ya dhambi torati haina mahali pa kumshika mtu tena na kumshitaki. Yesu alifanyika dhambi, akafa, akailipa Torati malipo ya dhambi.

SHETANI

Kwa njia ya msalaba katika mwili wake Yesu alimharibu Shetani kabisa na kumnyang’anya uwezo wake wote (funguo) wa kutawala mtu. Shetani alipata nafasi ya kutawala ulimwengu kupitia mtu, Adamu. Mungu kwa njia ya msalaba amemharibu Shetani na kumnyang’anya utawala kwa kupitia ‘mtu’ Yesu Kristo, “Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu za mauti, yaani, Ibilisi,” (Waebrania 2:14).

SHERIA

Sheria ya Musa ilionyesha makosa ya watu hivyo kuchochea hasira ya Mungu, “Kwasababu sheria ndiyo ifanyayo hasira; maana pasipokuwapo sheria hapana kosa” (Warumi 4:15). Sheria hii ilitaka malipo ya kifo kwa binadamu wote. Msalabani Yesu alisulubisha sheria na kulipia matakwa yake kwa kufa. Sasa sheria haina cha kushitaki imekwisha nguvu yake kwa mwili wa Yesu. Yesu alipofanyika dhambi alifungwa na sheria afe. Alipokuwa alikuwa huru na sheria, Alitimiza haki ambayo ilitakiwa na sheria yaani kifo. Kwa kuwa Yeye alikuwa ana haki yake na dhambi zetu ndizo alizifia kwa haki hiyo asingeendelea kuwa amekufa! Mungu akamfufua katika wafu, “Kwa kuwa yeye aliyekufa amehesabiwa haki mbali na dhambi.” (Warumi 6:7), “ambaye alitolewa kwaajili ya makosa yetu, na kufufuliwa ili tupate kuhesabiwa haki.” (Warumi 4:25). Msalaba ulifunga agano la sheria lililoleta kifo na kufungua kwa njia ya kufufuka Yesu Agano la Imani liletalo uzima.

MWILI

Mwili au utu wa dhambi ulisulubishwa kwa njia ya Yesu msalabani ili dhambi isitutawale tena. Huu ni mwili usioonekana au kinafsi. Nguvu ya dhambi kutawala ni kwa mwili wa dhambi ambao Yesu aliuua. Huu ni utu wa kale unao asi sheria ya Mungu, “tukijua neon hili, ya kuwa utu wetu wa kale ulisulubishwa pamoja naye, ili mwili wa dhambi ubatilike,tusiitumikie dhambi tena;...” (Warumi 6:6).

Katika mwili unaoonekana Yesu alibeba magonjwa yetu kwa kupigwa, “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti; ili, tukiwa wafu kwa mambo ya dhambi, tuwe hai kwa mambo ya haki; na kwa kupigwa kwake mliponywa.” (1 Petro 2:24).

LAANA

Laana ya Torati ni matokeo yote mabaya Torati iliyoyasema kwa watu wasioitii. Hakuna mtu aliyeweza kuitii Torati ya Musa, kwa sababu hiyo wote wakawa chini ya laana. Yesu alipofanyika dhambi zote alifanyika laana yote ya torati iliyoandikwa katika kumbukumbu la Torati 28. Kila namna ya uharibifu mikosi na balaa Yesu alifanyika juu ya mtu wa msalaba; ikiwemo 1. Magonjwa 2. Umaskini 3. Kushindwa 4. Kutoongezeka 4. Woga 5. Kutawaliwa 6. Kupigwa na maadui 7. Ujinga 7. 8. Upunguani n.k. Imeandikwa, “Kristo alitukomboa katika laana ya torati, kwa kuwa alifanywa laana kwaajili yetu; maana imeandikwa, Amelaaniwa kila mtu aangikwaye juu ya mti”. (Wagalatia 3:15).

KUFA NA KUFUFUKA

Kwa kifupi Yesu msalabani “Alikuwa sisi” alipofufuka, alifufuka “Tuwe yeye”. Kufa kwake kulibeba utumwa wetu wote, kufufuka kwake kukatupa uhuru wake wote. Huu ni ukombozi, ni kulipiwa. Msalaba ulichukua maisha yetu yote na kuyalipia, kufufuka kwa Yesu kumetupa maisha yote ya Yesu!

Meza ya Bwana ni ‘chombo’ cha kiimani cha kuyaona yote aliyochukua Yesu msalabani kwa ajili yetu na kushukuru, kisha kuona yote Yesu aliyotupa alipofufuka katika wafu na kushukuru.

Tunaposhiriki meza ya Bwana tunaionyesha imani yetu kwake, kwa yale aliyotenda kwa ajili yetu. Hapo, Yeye kama Kuhani aliye hai hata milele anayadhihirisha kwetu yote aliyoyalipia msalabani.

SURA ZA AGANO LA KALE

Baada ya kupata muhtasari huu kuhusu msalaba sasa hebu tuendelee kuangalia sura za meza ya Bwana Agano la Kale.

MTI WA UZIMA

Mti wa uzima ulikuwa katikati ya bustani ya Edeni (Mwanzoa 2:9). Kitu kilicho katikati ni mfano wa mhimili au nguzo. Mhimili wa mahusiano ya Mungu na watu ni Yesu Kristo, Muhimili wa mahusiano ya Adamu na Eva pamoja na Mungu bila shaka ulikuwa mti wa uzima. Walipoula siku zote uzima ulikuwa ndani yao. Yesu anasema mtu asiyekula mwili na damu yake hana uzima, “Basi Yesu akawaambia, Amin, amin, nawaambieni, Msioula mwili wake Mwana wa Adamu na kuinywa dmu yake, hamna uzima ndani yenu.” (Yohana 6:53). Mwili na damu yake ni mhimili wa maisha yetu, upo katikati, ni nguzo itupayo uzima. Tunadhihirisha kimwili ya kwamba tupo na mwili na damu kiroho kwa njia ya meza ya Bwana.

DIVAI NA MKATE

Katika mwanzo 14:18 imeandikwa, “Na Melkizedeki mfalme wa Salemu akaleta mkate na divai, naye alikuwa kuhani wa Mungu aliye juu sana.” Maandiko haya yanaonyesha kuhani Melkizedeki akimpa Ibrahimu mkate na divai. Picha ya vitu na watu wanao onekana katika maandiko haya ni kama ifuatavyo: Melkizedeki ni Yesu, “Kwa maana Melkizedeki huyo, mfalme wa Salemu, kuhani wa Mungu aliye juu, aliyekutana na Ibrahimu alipokuwa akirudi katika kuwpiga hao waflme, akambariki; … hana baba, hana mama, hana wazazi, hana mwanzo wa siku zake, wala mwisho wa uhai wake, bali amefananishwa na Mwana wa Mungu; huyo adumu kuhani milele.”(Waebrania7:1,3). Sura ya mkate ni mwili wake na divai ni damu yake. Ibrahimu hapa ni mfano wa kanisa lililopewa na Yesu (Melkizedeki) divai na mkate yaani mwili na damu. Kwa njia ya mwili na damu yake amekua kuhani wetu milele, kama alivyoonekana Melkizedeki.

SIKUKUU YA PASAKA

Katika maandiko, imeandikwa sikukuu ya pasaka iliendana na mikate isiyotiwa chachu, ilipaswa ifanyike kama ukumbusho katika vizazi vyote vya Israel ( Kutoka 12:14). Yesu alisema, Meza ya Bwana Yesu ifanyike kwa ukumbusho wake (Luka 22:19) . Hii inadhihirisha kuwa kondoo wa pasaka, mikate isiyotiwa chachu na mambo yote kwa ujumla yaliyotokea Israeli walipotoka Misri ni sura ya Kristo na Kanisa. Kutoka 12, imeanza kwa kuuelezea mwezi wa Abibu, kuwa ni mwezi wa kwanza wa kalenda ya Wayahudi. Siku ya kumi ya mwezi huu kila familia iliwapasa wawe na mwana kondoo asiye na hila (Mfano wa Yesu, hakuwa na hila 1 Petro2:22). Jioni ya siku ya kumi na nne mwanakondoo alichinjwa (Yesu pia alisulubiwa siku hii mwezi huo huo!). 

Damu ya mwanakondoo huyo ilipakwa pande mbili za mlango na juuu ya mlango (Ukiunganisha sehemu hizi tatu msalaba unatokea!). 

Israeli walitakiwa wale nyama ya kondoo huyu wa pasaka wakiwa wamevaa viatu, na nguo, tayari kwa safari, ilikuwa ni pasaka ya Bwana. Mungu aliwaambia Israeli watakapokula kondoo wa pasaka, na kupaka damu juu ya miimo ya milango na pembeni, angepita juu yao (Angewafunika). Malaika wa mauti asingewadhuru, bali angewadhuru Wamisri tu (Hii ni sura ya Yesu, katika yeye hakuna hukumu ya adhabu wala mauti kwa walio ndani yake). 

Kipindi hiki hawakutakiwa kula mikate yenye chachu (Hii ni alama ya utakaso na utakatifu kwa njia ya Yesu Kristo kondoo wa pasaka). Ni alama inayoonyesha Yesu atakuja kuondoa chachu/dhambi kabisa kwa sadaka yake msalabani.

Sikukuu hii ya pasaka na mikate isiyotiwa chachu iliwekwa na Mungu kama kumbukumbu ya ukombozi wa Israeli toka Misri katika maisha yao yote. Yesu alisema meza ya Bwana tuifanye kwa ukumbusho wake, tukumbuke yote aliyotufanyia katika ukombozi na wokovu. Meza ya Bwana haitupi kumbukumbu ya kazi ya ukombozi tu, bali hutukumbusha kujitenga na uchafu wote yaani chachu kwa njia ya sadaka ya ukombozi huo, yaani Pasaka wetu Yesu, “Basi, jisafisheni, mkatoe ile chachu ya kale, mpate kuwa donge jipya, kama vile mlivyo hamkutiwa chacu. Kwa maana Pasaka wetu amekwisha kutolewa kuwa sadaka, yaani, Kristo”(1 Wakorintho 5:7).

AGANO LA KALE NA AGANO JIPYA

Agano la kale lilianza wana wa Israeli walipotoka Misri kwa damu ya Kondoo wa pasaka na kupewa torati katika mlima (Waebrania 8:9). Agano jipya limeanza Yesu aliposulubiwa msalabani akafufuka katika wafu na kumtuma Roho Mtakatifu, katika huyo sheria ya Mungu ya upendo imeandikwa ndani ya waaminio. 

Maagano yote mawili yana kifo, damu, na sheria, ila sasa tunalo agano bora lililo hai. Meza ya Bwana ni kichocheo kinachotukumbusha yote haya na kuzisimamisha imani zetu katika hayo. Ishara ya kwamba Wana wa Israeli wameondoka Misri, ilikuwa ni kumla kondoo wa pasaka walimla huku wamesimama, wamevaa mavazi viatu na mikanda. Meza ya Bwana, Agano jipya inatukumbusha sisi ni wasafiri tuna agano na ahadi ya kuingia Yerusalemu mpya. 

MANA

Mungu aliwalisha mana wana wa Israeli kwa muda wote wa safari yao jangwani. Hiki kilikuwa chakula cha kimwili kilichoanzia rohoni (Mbinguni). Mungu aliye Roho aliwalisha walio mwili chakula cha kimwili tokea mbinguni (Yohana 6:31). Yesu alisema chakula cha kweli ni mwili wake na damu yake. Mana ya jangwani ilipoliwa iliwawezesha kuishi muda mfupi na baadaye walikufa. Lakini mwili na damu yake inatufanya tuishi milele. Ukisoma Yohana 6:31-58, Yesu aliongea kwa upana kuhusu mana, ambayo ni picha ya Agano la kale inayomwonyesha Yesu wa agano jipya. Kitu cha msingi kuhusu mana ni kwamba Wana wa Israeli waliitegemea kuishi jangwani bila hiyo wangekufa. Agano jipya tunategemea mwili na damu ya Yesu tuishi milele. Meza ya Bwana ni ishara kwetu kuwa Yesu ndiye mshika uzima na uhai wetu, bila yeye hatuwezi kuishi. Picha hii pia yatuonyesha, Israeli walikula mana mara kwa mara muda wote wa safari. Meza ya Bwana ni kitu kinacho takiwa kutumiwa na kanisa mara kwa mara, kuonyesha Yesu ni Uhai na uzima wetu wakati wote.

Somo hili linaendelea, jiunge nasi kila wiki na kila siku kwa masomo mengine mbali mbali katika blog hii. karibu kwa Maswali, Maoni na Wajulishe Wengine, Tujifunze na kukua pamoja. 
Barikiwa.