Tuesday, July 15, 2014

Asante Yesu!




Shukrani
Siku ya Jumamosi (12.7.2014), nilipokuwa naongoza maombi kanisani nilisikia moyoni mwangu tufanye maombi kwaajili ya kanisa zima kinyume na vifo vya  ghafla.  Siku  iliyofuata, yaani jana usiku kama saa sita hivi nilikuwa ninaomba na ghafla nikaanza kutamka kwamba Shetani hataniua.
Nilikuwa nikisema ninalindwa na nguvu za Mungu kwasababu imani yangu ipo kwa Yesu (1Petro 1:13).  Niliomba kwa kushindana na kutamka kwa ujasiri. Pia niliendelea kutamka kwamba Yesu amekuja niwe na uzima (Yohana 10:10).  Nilisema  amekuja awe nuru ya ulimwengu, ili nisikae gizani au katika ‘ushetani’ wowote (Yohana 12:46). Nilitamka na maandiko mengine kadhaa. Baada ya hapo nilienda kulala.
Usiku nikaota naendesha gari langu na nilipokuwa nazunguka “round about” nikagongwa nyuma mkono wa kulia na gari ambalo sikuliona.  Asubuhi, yaani siku ya Jumatatu nilikuwa na safari ya kwenda Moshi kufuatilia shule ya mtoto wangu. Nilipofika Kambi ya Mkaa, mbele kidogo ya Kikatiti, mbele yangu kulikuwa na lori limeharibika na nusu yake liko barabarani, upande wangu wa kulia magari yatokayo Moshi yalikuwa yanakuja, hivyo nafasi ilikuwa ndogo ya kuweza kupita.  Nilipunguza mwendo na nikapata nafasi na kuanza kupita, nyuma yangu kulikuwa na basi linakuja, lakini halikuwa karibu.  Ghafla nilisikia mshindo mkubwa upande wa nyuma ya gari kulia, basi lililokuwa nyuma lilishindwa kupunguza mwendo, bahati!(neema), Nilikuwa nimeshalivuka lori lililokuwa limepaki nikasogea kushoto, bila hivyo ningeweza kubanwa katika lori.  Wakati huo huo kumbe basi hilo liliponigonga liligonga na gari lingine mkono wa kulia lililokuwa limetokea Mererani. Wote tuliogongwa ni wachungaji! Sitamtaja jina mwenzangu, Maana sikumtaarifu nitaandika ushuhuda huu.
Leo jioni baada ya watu kufahamu kwamba nimepata ajali, mtumishi wa Mungu mmoja anayenisaidia kuuza vitabu akaniambia tokea jana alikuwa akiniangalia ananionea huruma na usiku aliniombea kwa uchungu akishindana na roho ya mauti. Roho Mtakatifu alikuwa akifanya kazi ya kuniokoa!
Kwa kweli Mungu ameniokoa! Ilikuwa ajali mbaya itokee ambayo kibinadamu nisingeweza kuikwepa. Hatari kubwa mbili zilikuwepo, gari liminywe kwenye lori au basi la nyuma linipandie. Mungu ameniokoa na kifo cha ghafla.
Kwa Shukrani Ninasema Maneno Haya:
BWANA ATANIOKOA NA KILA NENO BAYA NA KUNIHIFADHI HATA NITAKAPOFIKA UFALME WAKE WA MBINGUNI (2 TIMOTEO 4:18).
NINALINDWA NA NGUVU ZA MUNGU KWA NJIA YA IMANI YANGU KWA YESU KRISTO (1PETRO 1:5).
UHAI WANGU UMEFICHWA NDANI YA KRISTO YESU (WAKOLOSAI 3:3-4).
KAMA YESU ULIVYONIOKOA LEO UTANIOKOA SIKU ZOTE, NAKUOMBA UNAYESOMA UMSHUKURU MUNGU PAMOJA NAMI.

No comments:

Post a Comment